Habari za Punde

Wananchi Watakiwa Kubadili Mfumo wa Maisha Kwa Kufanya Mazoezi Ili Kujikinga na Magonjwa

 
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dkt. Hussein Ali Mwinyi amewataka wananchi kubadili mfumo wa maisha kwa kufanya mazoezi ili kujikinga na magonjwa mbalimbali yasioambukiza ukiwemo ugonjwa wa moyo.

Alisema hatua hiyo imethibitishwa na wataalamu wa afya kupitia utafiti walioufanya unaoonesha moja ya hatua muhimu ya kukabiliana na magonjwa hayo ni kufanya mazoezi.

“Nawasihi nyote muendelee kushiriki kwenye kambi mbalimbali za upimaji wa magonjwa na matembezi kama haya, kwani ni muhimu kwa afya zenu, kila mtu huko anakoishi atambue kufanya mazoezi ni kinga muhimu katika kuepuka magonjwa mengi hasa yasio ambukiza, kwa hiyo sote tuhimizane tujenge utamaduni wa kufanya mazoezi na kupima afya zetu mara kwa mara ili kubaini mapema kama tuna matatizo ya kiafya, kuchukue hatua za matibabu” Alishauri Dk. Mwinyi.

Rais Dk. Mwinyi aliyasema hayo viwanja vya Amani, Zanzibar alipofunga kambi na kampeni za upimaji na tembea na taasisi ya moyo Jakaya Kikwete (JKCI).

Alisema taifa linatumia pesa nyingi za kigeni kugharamia matibabu ya moyo na magonjwa mengine nje ya nchi. Hivyo aliipongeza taasisi ya JKCI kwa kubunifu mikakati mbali mbali ya kinga na tiba ya maradhi ya moyo nchini.

Aidha, aliishukuru taasisi hiyo kwa kuwajengea uwezo watumishi wa afya wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na kuwasihi kuendeleza utamaduni huko kwa watumishi wa Pemba.

“Nawasihi JKCI mfike na Pemba kwa ajili ya uchunguzi na kuhamasisha ufanyaji wa mazoezi kama njia bora ya kuimarisha afya, bila ya shaka wananchi wa Pemba nao wanahitaji huduma zenu na elimu hii kama mlivyofanya hapa Unguja” Alishauri Dk. Mwinyi.

Katika hatua nyengine Rais Dk. Mwinyi aliitaka  taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete kuongeza huduma zao kwenye maeneo mbalimbali ya nchi na kueleza kuwa kuwepo kwao kutasaidia kupambana na matatizo mbali mbali ya afya ambayo jamii wanakabiliana nayo.

Alieleza hatua hiyo itasaidia kuongeza uwezo na wataalamu watakao wahudumia vizuri wananchi na kupunguza madhara ya magonjwa haya ambayo yanaongezeka kila siku.

Alisema tokea kuanzishwa kwa taasisi hiyo, mwaka 2015 tayari imesaidia wagonjwa wengi wakiwemo waliotibiwa kwa dawa na waliofanyiwa upasuaji na kufanikiwa kwa kiasi kikubwa, hivyoa aliitaka taasisi hiyo kuimarisha utendaji wao na kuongeza tija kwa watu wengi kunufaika na huduma zao.

“Nafahamu kuwa taasisi hii imekuwa na utendaji mzuri sana tokea ilipoanzishwa. Hata hivyo, bado kuna nafasi ya kufanya vizuri zaidi ili kuyafikia malengo ambayo Tanzania tumejiwekea, katika kuimarisha afya za wananchi kwa kutoa huduma bora na zenye kiwango cha kimataifa”. Alieleza.

Akizungumza kwenya hafla hiyo, Waziri wa Afya, Nassor Mazurui alisema serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar watashirikiana na taasisi ya JKCI, kuongeza wataalam wa matatizo ya moyo Zanzibar kutokana na uhaba wa wataalamu hao ambapo alieleza kwasasa wapo wawili tuu.

Alisema alisema Zanzibar kwa sasa ina madaktari bingwa wawili tuu wanaoshughulikia matatizo ya moyo.

Naye, Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI), Dkt. Peter Richard Kisenge, alisema taasisi yao kwa kushirikiana na Wizara ya Afya Zanzibar, kupitia hospitali kuu ya Mnazi Mmoja wataendeleza matibabu ya moyo kwa kutoa huduma za kuvimba kwa moyo na upasuaji mkubwa wa moyo kwa wananchi ili kudumisha ushirikiano wao kwa vitendo.

Alisema kampeni walioidanya wiki nzima Unguja alieleza walifanikiwa huwahudumia wagonjwa 718, wakubwa 627 na watoto 91 ambao walifanyiwa vipimo vya matibabu ya moyo, sukari na magonjwa mengine.

Dk. Kisenge aliongeza kati ya watu wazima 627 waliopimwa matatizo ya moyo, 549 waligunduliwa wana ugonjwa wa moyo alieleza katika hatua hiyo walitoa vifaa 75 kwa baadhi ya wagonjwa na kueleza kuwa 46 walipewa watu wazima na vifaa 29 walipewa watoto.

Kampeni ya upimaji ya magonjwa yasiyoambukiza ya (JKCI) iliadhimishwa kwa kauli mbiu yao TEMBEA NA TAASISI YA MOYO JAKAYA KIKWETE (JKCI) na WIZARA YA AFYA, LINDA AFYA YA MOYO WAKO”

IMETAYARISHWA NA DARA YA MAWASILIANO, IKULU ZANZIBAR.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.