Habari za Punde

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mhe,.Hemed Suleiman Abdulla Azindua Fiscope Tanzania 2023 Kwa Niaba ya Rais wa Zanzibar

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mhe.Hemed Suleiman Abdulla akizindua Ripoti ya Utafiti Finscope Tanzania 2023 kwa upande wa Zanzibar, akimuwakilisha Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk.Hussein Ali Mwinyi, uzinduzi huo uliofanyika katika ukumbi wa Hoteli ya Golden Tulip Uwanja wa Ndege Zanzibar.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dkt Hussein Ali Mwinyi amesema Serikali itaendelea kuweka mazingira rafiki  na wezeshi ya kiuchumi ili kukuza Sekta ya Fedha nchini.

Ameyasema  hayo katika hotuba yake iliyosomwa kwa niaba yake na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Hemed Suleiman Abdalla katika Uzinduzi wa ripoti ya Utafiti Finscope Tanzania 2023 kwa  upande wa Zanzibar katika ukumbi wa Hotel ya  Golden Tulip Uwanja wa Ndege jijini Zanzibar.

Rais Dkt Mwinyi amesema kuwa Serikali itaendelea kuweka mazingira rafiki ya kiuchumi ikiwemo kuunda Sera zinazozingatia mahitaji ya sekta, kuweka mfumo na kanuni wezeshi za udhibiti pamoja na kushirikiana kwa karibu na wadau wote wa sekta ya fedha ili kushuhulikia changamoto zinazokwamisha mafanikio kwenye utendaji.

Amesema kuwa wakati Serikali ikiendelea kuweka mikakati jumuishi pamoja na kuboresha miundombinu ya Msingi, FSDT ina wajibu wa kupanua wigo wa huduma za kifedha, kusaidia ukuwaji wa kampuni na Sekta binafsi pamoja na kuchangia ukuaji wa uchumi na maendeleo ya nchi.

Aidha Rais Dkt Mwinyi amesema Ripoti ya FinScope itasaidia katika kubuni mbinu zitakazotumika katika  utekelezaji wa Dira ya Maendeleo ya Zanzibar (2023-2050) Mpango Mkakati wa Taifa wa huduma jumuishi za fedha (2023- 2028) na mipango mengine yakimaendeleo pamoja na kutatua changamoto zilizopo, hivyo amesema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imejipanga kuhakikisha kuwa maendeleo ya sekta ya fedha na hali ya huduma jumuishi za fedha nchini ziinaimarika.

Dkt. Mwinyi amesema bado kuna kazi kubwa ya kuhakikisha Wazanzibari wenye umri wa kufanya kazi, hususan wanawake, wanafanikiwa kupata kipato binafsi ili kupunguza hali tegemezi na kuongeza matumizi ya bidhaa na huduma mbalimbali za fedha ili kuboresha ustawi wa maisha yao ya kila siku pamoja na kukuza uchumi wa nchi.

Sambamba na hayo amewataka wadau wa Sekta ya fedha kuendelea kuunga mkono jitihada za Serikali za kuboresha hali ya huduma ya  jumuishi za kifedha kama zilivyoainishwa katika Dira ya Maendeleo ya Zanzibar na kuwahakikishia kuwa Serikali iko tayari kushirikiana na wadau wa maendeleo nchini kwa lengo la kukabiliana na vikwazo vya maendeleo katika sekta ya fedha kwa kuzingatia Sera, kanuni na miongozo ya nchi.

Nae Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, fedha na Mipango Dkt Saada Mkuya Salum  amesema  bado kuna matumizi finyu  ya bima ya afya nchini hivyo Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imeona umuhimu wa kuanzisha mfuko wa bima ya afya Zanzibar pamoja na kuyataka mabenki kutafuta utaratibu mwengine wa kufungua huduma za fedha kwa jamii ili kurahisisha upatikanajiwa  kuweka fedha benki kwa urahisi na kupunguza gharama.

Dk. Mkuya amesema katika kutekeleza hilo kuna haja ya kusambaza matokeo ya utafiti  huu kupitia njia sahihi ili kuhakikisha kunafanyika maamuzi na kubuni bidhaa na huduma zinazopatikana kirahisi, kwa gharama nafuu, na kuzingatia  mapendekezo na matakwa ya watumiaji ili kuwafikia watu wengi zaidi.

Kwa upande wake Kaimu Mkurugenzi mfuko wa  kuendeleza sekta ya fedha Tanzania Ndugu Erick Masinde amesema ripoti hii  imekuwa na lengo la kuikuza sekta ya fedha na kuimarisha upatikanaji wa huduma za fedha ili kuwa jumuishi na endelevu na hatimae kurahisisha shughuli za kiuchumi, kuboresha maisha ya watanzania na kupunguza umasikini.

Mapema watoa mada katika uzinduzi wa riport hio wamesema kupitia ripoti hio kutazisaidia Serikali zote mbili kukuwa kiuchumi na kimaendeleo hivyo wameiomba serikali ya Zanzibar kuitumia ripoti hio kama ni kielelezo kikubwa cha kuondoa upatikanaji wa fedha kwa wananchi wake sambamba na kukuwa kwa maendeleo endelevu nchini.

Ripoti kama hii imekuwa ikitolewa kila baada ya miaka minne (4) kwa kushirikiana na wadau mbali mbali wa fedha  hivyo ripoti hii  inataarifa muhimu zinazohusu Zanzibar na upatikanaji wa wa fedha.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.