Habari za Punde

DK. SHEIN AIVAMIA NGOME YA CUF PEMBA.

Wana CUF Kusini Pemba wasema ndiye chaguo lao

Na Suleiman Rashid, Pemba

HALI si shwari kwa wafuasi wa CUF wa mikoa miwili ya Pemba ambao inadaiwa kuwa mvutano unaokaribia kukipasua chama hicho ambacho kiko katika kampeni za kuwania utawala wa nchi.

Habari kutoka kisiwani humo zinaeleza kuwa wafuasi wa chama hicho wa Mkoa wa Kusini na Kaskazini Pemba, wamekuwa wakivutana kila mmoja kutaka mzawa wa Mkoa huo apewe ridhaa ya kuongoza Zanzibar baada ya uchaguzi mkuu.

Wafuasi wa chama hichi Mkoa wa Kusini Pemba, wanamekuwa kwenye kampeni ya kutaka mgombea wa CCM, Dk. Ali Mohammed Shein apewe ridhaa ya kuiongoza Zanzibar ambaye anatokea mkoa huo.

Kwa upande wa mkoa wa Kaskazini, wafuasi wa chama hicho nao wanavuta upande wao wakitaka kura zote apewe Seif Sharif Hamad ambaye ni mzawa wa kijiji cha Mtambwe kilioko mkoa huo.

Mvutano huo wa chini kwa chini unadaiwa kuibuka mara tu baada ya Halmashauri Kuu ya CCM kumpitisha, Dk. Ali Mohammed Shein kuwania kiti cha Urais wa Zanzibar kupitia chama hicho.

Baada ya CCM kulipitisha jina hilo wananchi wa Mkoa wa Kusini Pemba ambapo wengi wao ni wafuasi wa CUF, wamekumbwa na hisia kali na damu kuwachemka kwa kuunga mkono Dk. Shein aliyezaliwa Chokocho.

Mpasuko huo ambao upo wazi wazi ambapo huku uchaguzi mkuu ukikaribia, ufa wake unazidi kuonekana ingawaje hakuna mwanasiasa aliyekuwa tayari kueleza hali hiyo.

Uchunguzi uliofanywa na mwandishi wa habari hizi, umegundua kuwa wananchi wa Mkoa Kusini Pemba wamekuwa hawashabikii sana huku hamasa waliyonayo huko nyuma kwa chama cha CUF ikishuka kama ilivyozoeleka.

"Ngoja nikwambie wewe angalia katika mikutano ijayo ukiacha huu wa ufunguzi hakutakuwa na watu wengi kama ulivyozoea, ila usije sema nimekwambia", alisema mzee mmoja alilieleza gazeti hili.

Kauli ya mzee huyo ilithibitika wiki iliyopita pale Maalim Seif Sharif Hamad aliposhindwa kuzungumza na kuahirisha mkutano katika uzinduzi wa kampeni kwenye kiwanja cha Banda Taka.

Baadhi ya wakaazi wa Chokocho kijiji alichozaliwa Dk. Shen waliozungumza na Gazeti hili walisema ingawa wao ni wafuasi wa Chama cha wananchi, lakini mara imewachanganya kwani damu nzito kuliko maji.

"Unajua siasa ni siasa na familia ni familia inapobidi siasa unaiweka pembeni unafinya jicho unagugumia mmm unaokoa familia" alisema moja wa mkazi wa Mkanyageni aliejitambulisha kwa jina la Malim Shaali.

Alisema walivyojipanga wao Rais wa awamu ya saba atakayeviongoza visiwa vya Zanzibar atatoka Chokocho jambo ambalo litakipa heshima kijiji hicho.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.