Hutuba ya Mhe Waziri
wa Afya Nd. Mahmoud Thabit Kombo kwa Waandishi wa Habari Katika Maadhimisho ya
Siku ya Malaria Dunia
Zanzibar, 22/04/2016
Mheshimiwa Naibu
Waziri wa Afya
Katibu Mkuu Wizara ya
Afya
Naibu Katibu Mkuu
Wizara
Wakurugenzi wa Idara
mbali mbali za Wizara ya Afya
Nd. Waandishi wa
habari pamoja na wadau wengine wa Afya; Assalam Alaikum
Kabla ya yote napenda kwa kuanza kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa
kutujaalia afya njema na ni Imani yangu kuwa sote ni wazima. Aidha nachukua
fursa hii kuwashukuru waandishi wote mliofika hapa kuungana nasi katika
harakati za kumaliza ugonjwa wa malaria Zanzibar. Karibuni sana.
Ndugu Waandishi,
Tukiwa tunaelekea kwenye maadhimisho ya siku ya malaria duniani
ambapo kilele cha maadhimisho haya hufanyika kila ifikapo terehe 25 Aprili,
Zanzibar tunaadhimisha siku hii kwa kujivunia mafanikio makubwa tuliyoyapata
katika kupambana na ugonjwa wa malaria. Takwimu za Wizara ya Afya zinaonesha
kuwa tokea mwaka 2007, tatizo la malaria limepungua kwa kiwango cha chini ya asilimia moja.
Aidha, vifo vinavyotokana na malaria pia vimepungua. Mwaka jana (2015) watu
….walifariki kwa malaria. Mwaka huu hadi mwezi huu wanne hakuna mtu aliefariki
kwa ugonjwa huu. Haya ni mafanikio makubwa ambayo si rahisi kuyapata nchi
nyengine ya Afrika.
Lengo kuu la maadhimisho haya ni kuwakumbusha wananchi katika
ngazi zote kuendelea kupambana na malaria kwa kufuata maagizo ya wataalam kwani
ugonjwa wa malaria bado upo Zanzibar. Napenda kuwakumbusha wananchi kwamba
ugonjwa huu unashamiri zaidi mara tu baada ya mvua za masika kumalizika
kutokana na kutengenezwa mazalio ya mbu katika maeneo yote yanayotuwama maji ya
mvua. Mtakumbuka kua mwaka huu tumepata mvua kubwa na sehemu nyingi maji
yametuwama. Kutokana na hali hii uwezekano wa kuongezeka mazalio ni mkubwa na
hatimae ugonjwa kuenea sehemu zote.
Nd. Waandishi,
Katika maadhimisho ya mwaka huu wa 2016, Wizara ya Afya imepanga
kuendelea kutoa taaluma kwa jamii juu ya njia mbali mbali za kijikinga na
malaria pamoja na maradhi mengine ya kuambukiza. Aidha ifikapo tarehe
24/04/2016 Wizara Afya imepanga kufanya matembezi ya hiari yatakayowajumuisha
viongozi wa Wizara ya Afya,Viongozi wa Mikoa na Wilaya, Vikundi mbali mbali vya
mazoezi pamoja na viongozi wa Taasisi za Chama na Serikali. Matembezi haya
yanakwenda sambamba na kauli mbiu ya maadhimisho hayo ya malaria duniani
isemayo ‘Maliza Malaria Kabisa’.
Ndugu Waandishi kazi ya kumaliza malaria si wajibu wa Wizara ya
Afya peke yake, ila ni wajibu wetu sote kwa kila mtu na nafasi yake. Kwa
mantiki hiyo nachukua nafasi hii kukualikeni nyote mlokuepo na waliokua hawapo
nasi kwa muda huu kujumuika nasi katika maadhimisho hayo muhimu siku ya
Jumapili.
Matembezi haya ya hiari yanategemewa kuanzia……………. Mnamo saa 12
asubuhi na kuishia katika kiwanja cha mpira cha Kikosi cha Kikosi cha Kuzuia
Magendo (KMKM) Maisara ambapo mgeni rasmi atakua kiongozi wetu Makamo wa Raisi
wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar Mheshimiwa Balozi Seif Ali Iddi. Mhe,
Balozi atawahutubia washirika wa matembezi hayo kwa kuwapa nasaha washiriki na
wananchi kwa jumla juu ya ugonjwa huu na hatua zilizofikiwa za kumaliza ugonjwa
Unguja na Pemba.
Ndugu Waandishi
Kwa kuwa leo nimepata fursa ya kukutana nanyi, sina budi
kuwajuilisha kwa mukhtasari kuhusu ugonjwa huu ikiwa tumo kwenye maadhimisho
haya ili muwajuilisha wananchi. Wizara ya Afya inasisitiza kua malaria bado ipo
Zanzibar na katika mikoa yote na zaidi ni Wilaya ya Magharibi A na B, Wilaya ya
Kati na Micheweni Pemba.. Kwa maelezo hayo Wizara inawaka wananchi kwa ujumla
kuendelea kuchukua tahadhari za kujikinga
ikiwemo kutumia vyandarua vilivyotiwa dawa, kusafisha mazingira
tunayoishi ili kuondosha mazalio, kufunika maji ndani ya mahodhi, mapipa na
sehemu nyengine ili kumnyima nafasi ya kuzaliana adui mbu waenezao malaria.
Aidha, tunatoa wito kwamba mtu yeyote ndani ya familia anapojihisi homa aende
kituo cha afya cha karibu ili kuchunguzwa kama ana homa ya malaria. Usitumie
dawa ya malaria kutokana na ishara na dalili za malaria – chunguza damu.
Ndugu Waandishi
Ni vizuri kuwajuilisha kuwa katika mkakati huu wa kumaliza
malaria Zanzibar, tunakabiliwa na changamoto kadhaa ikiwemo maambukizi ya
malaria kutoka kwa wasafiri wanaotoka nchi za jirani pamoja na Watanzania
kutoka mikoa mbali mbali wanaokuja kuishi au kutembelea Zanzibar. Takwimu za
Wizara ya Afya za mwaka 2015 zinaonyesha kua asilima 60 ya wagonjwa
walioripotiwa kuwa na malaria walikua na historia ya kusafiri nje ya
Zanzibar.
Ndugu waandishi – kali mbiu
niliyoitaja awali inaisisitiza jamii umuhimu wa kufuata maelekezo ya wataalamu
pamoja na kutumia kinga kama vile chandarua kilichotiwa dawa kila siku wakati
wa usiku na zaidi mtu anapotembelea Nchi, Mkoa, Wilaya au kijiji ambapo ugonjwa
wa malaria ni tatizo kubwa. Wizara ya Afya bado itaendelea kutoa elimu ya Afya
juu ya kinga ya malaria kupitia redio, television pamoja na matangazo katika
viwanja vya ndege na bandarini ili kuwapata tahadhari wasafiri.
Ndugu waandishi ni Imani yangu kuwa taarifa hii mtaifikisha kwa
jamii ili kutimiza wajibu wenu ulivyo wa kuwahabarisha wananchi taarifa sahihi
kuhusu ugonjwa huu. Aidha, napenda kuwakumbusha tena kuuungana nasi siku ya
Jumapili na kuweza kupata maoni kutoka kwa washiriki wa matembezi hayo juu ya
juhudi za Serikali katika kuondosha ugonjwa huu.
Nawatakia kazi njema na ahsanteni kwa kunisikiliza.
No comments:
Post a Comment