Habari za Punde

Hatimaye Ligi Kuu Zanzibar Yapata Mdhamini


Ni Grand Malt Kuidhamini kwa Miaka mitatu

Na Abdi Shamnah

VILABU vinavyoshiriki ligi kuu ya Zanzibar, vimetakuwa kusimamia na kuweka mbele suala la nidhamu, sambamba na kuepuka malumbano na migogoro isio na tija katika soka.

Changamoto jhiyo imetolewa jana na Waziri wa Habari, utamaduni, Utalii na Michezo, Said Ali Mbarouk katika ukumbi wa hoteli ya Bwawani katika hafla ya uzinduzi wa Udhamini wa Ligi kuu ya Zanzibar, itakayojuilikana kwa jina la ‘Grand Malt Premier League’.

Kampuni ya Kinywaji baridi kisicho na kilevi cha Grand Malt, imedhamini Ligi kuu ya Zanzibar, kwa mkataba wa miaka mitatu kwa gharama ya shilingi Milioni 140, ukijikita katika suala la utoaji huduma katika nyanja za usafiri, malazi, chakula na zawadi kwa klabu zitakazoshiriki ligi hiyo.
Akizungumza na katika hafla hiyo iliowashirikisha viongzoi wa Wizara ya Habari,Utamaduni,Utalii na Michezo,BTMZ, ZFA na wale wa klabu za soka, Waziri Mbarouk, alisema nidhamu ni nyenzo muhimu katika uendelezaji wa soka, kwa kuzingatia kuwa hakuna mdhamini atakaefurahia kudhamini ligi ambayo daima inakabiliwa na migogoro.


Alisema njia pekee ya kuwatia moyo wadhamini hao pamoja na wengine wenye azma ya kuidhamini ligi hiyo ni kudumisha nidhamu na kuepuka migogoro.

Alisema Wizara yake na Serikali kwa jumla itatoa kila aina ya ushirikiano katika kufanikisha mchakato ulioanza wenye lengo la kulikomboa soka la Zanzibar kufikia katika maendeleo.
Aidha aliliagiza BTMZ kuweka utaratibu madhubuti kuona fedha zinazotolewa na wadhamini hao zinatumika kama zilivyokusudiwa.

Katika hatua nyingine Mbarouk alisisitiza msimamo wa Serikali na wananchi kuwa  kwa mujibu wa silka na utamaduni wa watu wake, vinywaji vya pombe havitaruhusiwa  kudhamini michezo hapa nchini.
“Najua kuna kampuni nyingi zilikuwa na hamu kuona wanakuwa wadhamini wa michezo hapa Zanzibar kupitia pombe wanazotengeneza , hilo ni muhali na haliwezekani’, alisema.

Alisema kampuni zinazotenegenza vinywaji visivyo na kilevi kama ilivyo Grand Malt vinaruhusiwa na vinakaribishwa kwa mikono miwili kudhamini katika aina za michezo tofauti.

Alimpongeza Waziri Jihad (aliekuwa Waziri wa Wizara hiyo kabla yake) kwa juhudi kubwa alioifanya hadi kukamilika kwa mchakato wa kumpata mdhamini huyo.

Mapema Meneja Masoko wa Grand Malt, Fimbo Mohammed, alisema kuwa mkataba huo unaoanza Augost, mwaka huu ukiwa ni asilimia 70 ya mahitaji ya bajeti yote, hivyo kutoa fursa kwa wadhamini wengine kuweza kumalizia asilimia 30 zilizobaki.

Alifafanua kuwa mkataba huo, utakuwa ukifanyiwa mapitio kila mwaka, na kutoa uwezekano wa fedha hizo kuongezeka kutegemea na ufanisi utakaopatikana.

Aliwataka wadau wa soka kushirikiana pamoja ili kuhakiksha mabadiliko ya kweli katika soka yanafikiwa.
Alisema Kampuni yake inaona fahari na heshima kubwa kudhamini ligi hiyo, na kuzitaka kampuni nyengine kujitokeza ili kuleta mapinduzi ya kweli katika soka la Zanzibar.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.