Habari za Punde

Bopar kutekeleza agizo la serikali



 Na Hafsa Golo
KAMPUNI ya Bopar Enterprises Limeted ambayo ndiyo iliyoingiza unga mbovu kupitia bandari ya Zanzibar imesema itatekeleza agizo la  serikali la kuuondoa unga huo.

Wiki iliyopita, Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar, Maalim Seif Sharif Hamad alitoa mwezi mmoja kwa kampuni hiyo kuundoa unga huo ambao tayari umeanza kutoa harufu mbaya.

Hata hivyo kampuni hiyo imetaka kampuni ya uwakala wa mizigo bandarini kutoa mchango wake ili unga huo uondoke katika bandari hiyo kwa kuwa ndiyo iliyozembea hadi kusababisha unga huo uharibike.

Meneja wa kampuni hiyo, Said Nassir Nassor amesema kama kampuni hiyo ya uwakala wa mizigo itakataa kutoka ushirikiano, kampuni yake itauondoa unga huo na baadae kuchukua hatua nyengine za kisheria.


Alisema  hakuna sababu ya kupinga amri ya serikali kwani kampuni yake inaheshimu maamuzi hayo hasa ikizingatia kwamba  serikali ndio muhimili mkuu katika nchi.

Meneja huyo alisema unga huo ulinunuliwa ukiwa bado haujaharibika, lakini ulikaa muda mrefu baharini na kusababisha kuharibika.

Alisema makontena yenye unga huo yaliondolewa nchini Uturuki Disemba 4, 2011 na kufika bandari ya Dar es Salaam Januari 3, 2012 lakini ulifikishwa bandari ya Zanzibar mwezi Mei mwaka 2012.

"Joto na hali ya hewa ya bahari lazima unga uharibike miezi minne unga upo baharini mimi nawalaumu wenye meli na hili mlibaini kwani unga wa ngano hauwezi kustahamili na kawaida unaishi kwa muda wa miezi tisa zaidi ya hapo unaharibika,"alisema.

Gazeti hili ilipata ‘bill of lading’ yenye namba MSCUOS 001680 ambayo imeainisha  tarehe uliotoka  unga huo nchini Uturuki.

Meneja wa kampuni ya Mediterranean shiping tawi la Zanzibar, Abdurazak Omar Tahir, alisema  wao hawahusiki na uondoshaji wa makontena ya unga huo  kwani sio kazi yao.

Aidha alisema kutokana na dalili zilizojitokeza unga huo  ulipakiwa tayari ukiwa umeanza kuharibika na kutokana na masafa marefu ya usafiri na kuchelewa kwa taratibu za ufungaji  gati na upakuaji katika wa bandari ya Dar -es Salaam , unga huo ulizidi kuharibika.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.