Habari za Punde

Bunge larekebisha kanuni kuwaruhusu wajumbe walio nje ya nchi Kupiga kura


Benedict Liwenga, Dodoma.

BUNGE Maalum la Katiba limepitisha marekebisho ya Kanuni ili kuliwezesha kufikia hatua ya mwisho ya upigaji kura kuanzia tarehe 29 Septemba hadi tarehe 2 Oktoba mwaka huu.

Hatua hiyo ililenga kumaliza vikao vya Bunge hilo kwa muda uliopangwa kwa mujibu wa Sheria wa tarehe 4 Oktoba mwaka huu.

Kauli hiyo imetolewa leo na Mwenyekiti wa Bunge Maalum la Katiba, Mhe. Samuel Sitta wakati alipokuwa akitoa maelezo ya utangulizi kuhusu uwasilishwaji wa azimio la kupitisha Marekebisho ya Kanuni za Bunge hilo.

Mhe. Sitta amesema kuwa inakadiriwa kuwa wajumbe wasiopungua 480 wanatarajiwa kupiga kura na kutokana na kanuni zilivyokuwa kabla ya mapendekezo ya mabadiliko hayo ingechukuwa siku nyingi kukamilisha zoezi la upigaji kura kwa kupitia kifungu kwa kifungu.

“Kanuni zilivyo hivi sasa kama hatutafanya mabadiliko itachukua kwa wastani wa dakika kama mbili kwa kila mjumbe kupiga kura kwa kila kifungu ambapo kwa siku tutamia wastani wa dakika 960 kwa ibara moja, tunatarajia ibara zitakuwa 300…ameongeza kwa ibara hizo tungehitaji siku 300 kukamilisha zoezi hilo ambao muda huo utakuwa kinyume na utaratibu uliopangwa tutakuwa tunamaliza ibara moja kwa siku moja”, alisema Sitta.

Amesisitiza kuwa marekebisho yaliyanyika yalilenga kuhakikisha kazi ya upigaji kura inakuwa rahisi na inamalizika katika muda uliopangwa wa kisheria wa siku 60.

Awali akiwasilisha maelezo ya marekebisho ya Kanuni za Bunge Maalum za Mwaka 2014 kwa niaba ya Mwenyekiti wa Kamati ya Kanuni na Haki za Bunge Maalum Amon Mpanju alisema kuwa Kanuni zilifanyiwa mabadiliko ni ya 36 na 38.

Amesema kuwa marekebisho hayo yatamwezesha mjumbe aliye nje ya maeneo ya Bunge kwa ruhusa ya maandishi ya Mwenyekiti wa Bunge Maalum la Katiba kupiga kura ya wazi na siri kwa njia ya nukushi na mtandao.

Mpanju ameongeza hatua nyingine ni kumwezesha mjumbe kupiga kura katika muda usiozidi siku saba kwa urahisi na ufanisi.

Akitoa ufafanuzi wa wajumbe walioko Hijjah, Sheikh Norman Jongo amesema mjumbe anayetekeleza ibada hiyo hakatazwi kupiga kura ili mradi hajafikia hatua za mwisho wa ibada hiyo.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.