Habari za Punde

Chikawe ataka Panya Road wasifanywe mradi

Na Augusta Njoji, Dodoma
WAZIRI wa Mambo ya Ndani, Mathias Chikawe, amelitaka jeshi la polisi kupanga mikakati thabiti kuhakikisha amani na utulivu uliopo unaendelea kuimarishwa hasa wakati wa kampeni na upigaji kura ya maoni ya katiba inayopendekezwa.

Kauli hiyo aliitoa jana mjini hapa alipokuwa akifungua mkutano mkuu wa mwaka wa maofisa wakuu wa jeshi la polisi nchini ambao umefadhiliwa na benki ya NMB.

"Kwa mwaka huu nchi yetu ina matukio mawili makubwa ya kihistoria na uzoefu unaonesha matukio ya upigaji kura na chaguzi mbalimbali mara nyingi huwa yanaambatana na vitendo vya uvunjifu wa amani ikiwemo vurugu, uharibifu wa mali na wakati mwingine husababisha vifo,” alisema.

Hata hivyo, alitahadharisha kuongezeka kwa mitandao ya uhalifu wa kimataifa na ugaidi na kusema endapo haitadhibitiwa mapema inaweza kujipenyeza katika sekta mbalimbali ikiwemo kufadhili watafuta uongozi.


Alisema watu hao wanatafuta uongozi kwa kutumia fedha zao ili kujiwekea kinga na kujenga misingi ya kuendeleza uhalifu wao, hali inayohatarisha utawala wa sheria, mfumo wa demokrasia na upatikanaji wa haki nchini.

"Jeshi hili naliaagiza kutovumilia watumishi wa aina hiyo na lisisite kuwachukulia hatua za kinidhamu na kisheria watumishi watakaojiingiza katika ushirikiano wa aina hiyo ambao unahatarisha amani na usalama wa nchi,"alisema.

Akizungumzaia kuhusu kuibuka makundi ya kihalifu kama Panya road, Waziri huyo alisema hali hiyo haikubaliki na kulitaka jeshi hilo kutimiza wajibu badala ya kusubiri matukio yatokee.

"Wananchi wa Dar es Salaam wanahoji inakuwaje baada ya taharuki ya Panya road jeshi la polisi linakamata watu zaidi ya 1,200? Je jeshi la polisi lilikuwa linawafahamu kabla? Wananchi wanalituhumu jeshi la polisi kanda maalum ya Dar es Salaam kuwa baada ya kuwakamata vijana wengi limefanya mradi kwa kauli kuwa kuingia bure kutoka kwa pesa,"alisema.

Alisema iwapo malalamiko hayo ni ya kweli basi baadhi ya askari wasiowaaminifu wametumia fursa hiyo kujinufaisha na kuwanyanyasa wananchi na kuagiza hatua stahiki zichukuliwe endapo ikithibitika kuna ukiukwaji wa maadili mema ya jeshi la polisi.

Kwa upande wake, Mkuu wa Polisi, IGP, Ernest Mangu, alisema jeshi linaweka mkakati kwa kushirikiana na vyama vya siasa, Msajili wa Vyama na Tume ya Taifa ya Uchaguzi ili kudhibiti matukio ya uvunjifu wa amani katika uchaguzi mkuu ujao na zoezi la upigaji kura ya maoni kwa ajili ya upatikanaji wa katiba.


Aidha alisema takwimu za uhalifu wa jinai za mwaka 2014 zinaonesha kushuka kwa asilimia 5.7 ikilinganishwa na asilimia 1.1 kwa mwaka 2013 na jeshi hilo limetenga shilingi milioni 500 kwa ajili ya kuwazawadia wananchi watakaotoa taarifa zitakazosaidia kukamatwa silaha, risasi na miripuko isiyo halali.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.