Habari za Punde

Hatimae 'Paka wa binti hatibu' aingia mitaani


Ø  Chauza kama njugu
Ø  Kuingia Ulaya, Japan na Marekani  kuanzia wiki ijayo

Na: Ali O. Ali

Kile kitabu  cha ‘PAKA WA BINTI HATIBU’ ambacho kilikuwa kikisubiriwa kwa hamu na shauku kubwa hatimaye kimeingia mitaani tayari kufikisha ujumbe na kutoa burudani kwa jamii iliyokusudiwa.

Akizungumza na mwandishi wa habari hii, mtunzi wa kitabu hicho Mhadhiri Yussuf Hamad, wa Chuo kikuu cha London, SOAS nchini Uingereza, amethibitisha kupokea taarifa na ithibati rasmi kutoka kwa mchapishaji wa kazi hiyo, The Jomo Kenyatta Foundation Educational Publishers ya Nairobi nchini Kenya.

“Ninaweza kukuthibitishia ndugu mwandishi pamoja na kuwathibitishia wapenzi, washabiki na wasomaji wangu kwa ujumla kuwa kitabu hivi sasa kipo madukani na kinapatikana kwa bei nafuu kabisa.’ Alisema Bwana Yussuf.

Kitabu cha Paka wa Binti hatibu, kilitarajiwa kutoka mapema mwezi Novemba mwaka jana lakini kutokana na matatizo ya kiufundi, kitabu hicho kilichelewa kutoka hadi mwezi Machi mwaka huu ambapo kinapatikana maduka yote ya vitabu hasa hasa katika duka la The Jomo Kenyatta Book Distribution Center, iliyopo  Kijabe  Street, jijini Nairobi.

Akitoa ufafanuzi juu ya namna gani kitabu hicho kinaweza kuwafikia walengwa nchini Tanzania na nchi nyengine za Ulaya, Afisa wa shirika hilo la Uchapishaji Bibi Anne alisema;

“Kwa sasa kitabu kinapatikana hapa Nairobi. Lakini tumekuwa tukipata ‘order’ kutoka sehemu za Ulaya kama  vile Uingereza, Japani  na Marekani na ijapokuwa tulikuwa hatujajipanga kwa hilo tunatafuta utaratibu wa kukifikisha huko pia muda si mrefu. Hadi sasa kuna order ya kopi 100 ambazo zimeagiziwa kutumwa Uingereza. Tunajaribu kutafuta njia za kuwafikia wasomaji wetu wa huko na muda si mrefu tutaweza kuwafikia.’

Alipoulizwa kuhusu vipi kitabu kitawafikia wasomaji waliopo Tanzania na visiwani Zanzibar, Bibi Anne alisema;
“ Kwa sasa hatuna wakala nchini Tanzania. Isipokuwa wateja walioko Tanzania wanaweza kuwasiliana na kampuni ya Dar es Salaam Printers Limited ambao wataweza kuagizia vitabu hivyo na kuwafikishia Watanzania. Tunawashauri wateja wetu walioko huko kufanya mawasiliano na kampuni hiyo ili waweze kukipata kitabu hicho”

Wakati huo huo, Kampuni binafsi ya uchapishaji na usambazaji  ya JC PRESS iliyoko jijini London nchini Uingereza, imeeleza nia yake ya kutaka kuwasiliana na kampuni ya Jomo Kenyatta Foundation ili kuweza kushirikiana katika kukisambaza kitabu hicho kwa urahisi katika nchi za Ulaya na hususan kwa njia ya mauzo mtandaoni ambayo ni rahisi katika nchi nyingi za Ulaya na Marekani.  Kwani kufanya hivyo kutarahisisha kupatikana kwa kitabu hiki kwa wepesi zaidi hasa ukizingatia kuwa ni kitabu ambacho kimevuta na kugusa hisia za wasomaji wengi.
Aidha, naye mkuu wa Idara ya masomo ya Kiafrika wa chuo kikuu cha London SOAS, Bibi Alena Rettova amesema kuwa Idara yake imejipanga kukifanyia kitabu hicho uzinduzi rasmi baada ya mapumziko ya pasaka.
Kitabu cha Paka wa Binti Hatibu ni kazi ya kwanza ya mwandishi Yussuf Shoka HAMAD kutoka Visiwani Zanzibar. Kitabu hicho kina hadithi fupi saba ambazo zimebeba dhima na dhamira mbali mbali za kijamii. Alipoulizwa kuhusu ubora wa kazi yake hiyo ya awali Bwana Hamad alisema;
‘Hii ni kazi yangu ya kwanza kuchapishwa. Ninazo kazi nyingine nyingi hivi sasa. Lakini hii ni ya kwanza. Na kama mjuavyo Waswahili husema; ‘Kipya kinyemi, ingawa kidonda!’ Naamini nimejitahidi kadiri niwezavyo kuifanya kazi hii iwe na bora mlioutarajia. Ila kama mnavyofahamu, kazi ya Binadamu haiachi kuwa na makosa. Kwa vile ni kazi ya mwanzo, basi makosa madogo madogo ya hapa na pale yanaweza kujitokeza. Mimi si malaika. Ni binaadamu mwenye mapungufu. Ila, pamoja na hayo, nawaahidi makubwa wasomaji wangu watakaokisoma kitabu hiki.”
PICHA NA MAELEZO


Gamba la Kitabu cha PAKA WA BINTI HATIBU: Kulia anaonekana Binti Hatibu na Paka wake. Kushoto ni wageni waliomtembelea ili kujua kadhia ya Paka huyo!


Mwandishi wa ‘PAKA WA BINTI HATIBU’ Bwana Yussuf Shoka HAMAD akiwa ofisini kwake SOAS, jijini London mapema wiki hii

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.