Habari za Punde

Dk Shein: Azma ya serikali kutekeleza miradi yake mipya ipo pale pale


STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
Zanzibar                                    19.09.2016
---
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein leo amefanya ziara ya kutembelea eneo litakalojengwa soko la samaki, Malindi, ujenzi wa mradi wa hoteli ya Bwawani  pamoja na kutembelea eneo linalotaka kujengwa Ofisi za Benki ya Watu wa Zanzibar huku akieleza azma ya Serikali katika kutekeleza miradi yake mipya iliyopangwa.

Katika ziara yake hiyo, Dk. Shein alipata maelezo juu ya uendelezaji wa miradi hiyo muhimu na kupongeza hatua zianazoendelea kuchukuliwa huku akisisitiza haja ya kuharakishwa ili kumaliza kwa wakati uliopangwa sambamba na kuwepo kwa mashirikiano ya pamoja kwa taasisi husika za Serikali.

Dk. Shein akiwa ameongozana na viongozi mbali mbali, alieleza azma ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuhakikisha miradi  hiyo inatekelezwa kwa wakati uliopangwa ikiwa ni pamoja na ukarabati wa Chelezo ili eneo hilo liweze kuvutia.

Mapema Dk. Shein alitembelea eneo litakalojengwa soko jipya la Samaki, Malindi na kupata maelezo kutoka kwa uongozi wa Wizara ya Kilimo, Maliasili, Mifugo na Uvuvi pamoja na taasisi nyengine zikiwemo Shirika la Umeme Zanzibar (ZECO), Mamlaka ya Maji Zanzibar (ZAWA) na Mamlaka ya Mji Mkongwe Zanzibar.

Kwa upande wa Wizara husika ya Kilimo,  Maliasili, Mifugo na Uvuvi, Waziri wa Wizara hiyo Hamad Rashid alimuhakikishia Dk. Shein kuwa tayari Bunge la Japan limeshatoa baraka zake kwa kuahidi kutoa fedha taslim kwa ajili ya ujenzi wa mradi huo na kueleza kuwa fedha hizo ziko tayari.

Nae Mkurugenzi wa Idara ya Uvuvi Mussa Aboud Jumbe alimueleza Rais hatua zilizofikiwa katika ujenzi wa soko hilo linalojengwa kwa mashirikiano ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar pamoja na Serikali ya  Japan chini ya Shirika la Maendeleo la Japan (JICA).

Akitoa maelezo Mkurugenzi huyo alieleza kuwa soko hilo linalotarajiwa kuaza ujenzi wake mapema mwakani litakuwa la kisasa ambalo pia litakuwa na sehemu ya maegesho ya vyombo vya uvuvi vikiwemo vinavyovua bahari kuu, maeneo maalum kwa ajili wavuvi na wafanya biashara nyenginezo.

Aidha, Dk. Shein alipita njia ya Ras Al Khaimah, Malindi Funguni na kupata maelezo juu ya diko lisilo rasmi katika eneo hilo kutoka kwa uongozi wa Wizara ya Ujenzi, Mawasiliano na Usafirishaji pamoja na Wizara ya Kilimo, Maliasili Mifugo na Uvuvi.

Dk. Shein aliendelea na safari yake iliyoelekea hadi hoteli ya Bwawani ambako alipata maelezo kwa wakandarasi wanaoshughulikia mradi wa ujenzi wa Hoteli ya Bwawani ambapo alisisitiza haja ya kufanyia haraka ujenzi wa mradi huo.

Akiwa katika eneo hilo, Dk. Shein alipata maelezo kutoka kwa  Msimamizi wa ujenzi huo Syed Mansoor Hussain kutoka Kampuni ya “Stone Town Village Lmt” ambaye alieleza kuwa ujenzi wa mradi huo utakuwa wa awamu tatu ambao tayari awamu ya kwanza imeshaaza.

Alieleza kuwa awamu ya kwanza itahusisha ujenzi wa ukumbi wa Salama, hoteli pamoja na eneo la hoteli hiyo  ambapo ujenzi wa awamu hiyo unatarajiwa kukamilika mwishoni mwa mwaka ujao.

Kwa upande wa awamu ya pili ya ujenzi huo utahusisha maduka makubwa na madogo pamoja na mambo mengine muhimu yaliyomo katika mradi huo.

Dk. Shein pia, alipata fursa ya kutembelea eneo litakalojengwa Makao Makuu ya Benki ya Watu wa Zanzibar hapo Malindi Mjini Zanzibar na kupata maelezo kutoka kwa uongozi wa Benki ya Watu wa Zanzibar PBZ, ambao ulimueleza kuwa ujenzi huo unatarajiwa kuanza mwishoni mwa mwaka huu na unatarajiwa kugharimu Tsh.  Bilioni 3.8 hadi kumalizika kwake.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.