Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein kushoto)akiwa na ujumbe wake jana baada ya kumalizika kwa mkuutano wa kwanza wa Nchi zinazopakana na Bahari ya Hindi (INDIAN ASSOCIATION-IORA) akimuwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano Dkt John Pombe Magufuli,mkutano huo ulifanyika jana katika ukumbi wa Balai Sindang Mjini Jakarta Indonesia,(kushoto) Rais wa Sychells Mhe,Danny Faure, [Picha Ikulu.]
STATE
HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF
THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
Zanzibar 08.03.2017
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la
Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amefanya mazungumzo na Makamo wa Rais wa
Indonesia Muhammad Jusuf Kalla ambapo katika mazungumzo hayo viongozi hao
wamekubaliana kuzidisha uhusiano na ushirikiano kati ya Indonesia na Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania ikiwemo Zanzibar hasa katika sekta za maendeleo ikiwemo
kilimo.
Viongozi hao walifanya
mazungumzo katika ukumbi wa Mkutano wa Balai Sidang mjini Jakata, Indonesia ambao
uliofanyika Mkutano wa Kwanza wa Wakuu wa nchi na Serikali wa Jumuiya ya nchi
zinazopakana na Bahari ya Hindi (IORA).
Katika mazungumzo hayo
Makamo huyo wa Rais wa Indonesia alisisitiza haja ya kukuza na kuimarisha
uhusiano uliopo kati ya Tanzania na Indonesia na kueleza kuwa kwa upande wa nchi
yake utaendelezwa.
Makamo huyo wa Rais,
Bwana Kalla, alieleza kuwa nchi yake inathamini sana uhusiano na ushirikiano
huo na kueleza kuwa iko tayari kuviunga mkono vipaumbele vyote vilivyowekwa na
Tanzania ikiwemo Zanzibar katika sekta za maendeleo.
Alisisitiza kuwa Jumuiya
ya Nchi zilizopakana na bahari ya Hindi (IORA), imeweza kusaidia kwa kiasi
kikubwa kuziweka karibu nchi wanachama wake hatua ambayo itachangia kwa kiasi
kikubwa kukuza na kuimarisha uhusiano na ushirikiano huo kati ya Indonesia na
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Aidha, kiongozi huyo
aliongeza kuwa Indonesia inatambua kuwa Zanzibar ni nchi mshirika miongoni mwa
nchi zinazozalisha karafuu kwa wingi duniani, karafuu ambazo zina sifa
kimataifa, hivyo azma ya kushirikiana katika sekta ya biashara na kilimo ina umuhimu
wake mkubwa hasa ikizingatiwa kuwa nchi hizo zimefanana kimazingira.
Pamoja na hayo, Kiongozi
huyo alieleza kuwa katika suala zima la biashara hivi sasa soko kubwa lipo
katika nchi za Afrika, hivyo kuwepo kwa mashirikiano hayo kutarahisisha
upatikanaji wa bidhaa kwa pande mbili hizo.
Kwa upande wake Dk.
Shein, alitumia fursa hiyo kutoa pongezi kwa Indonesia kwa kufanikisha Mkutano
huo mkubwa kwa mashirikiano ya pamoja kati ya nchi hiyo na nchi wanachama wa
Jumuiya ya (IORA).
Dk. Shein alimueleza
Makamo huyo wa Rais wa Indonesia kuwa Tanzania inajivunia kwa kiasi kikubwa
uhusiano na ushirikiano wa kihistoria uliopo baina ya pande mbili hizo ambao
umeasisiwa na viongozi wakuu wa nchi hizo tokea miaka ya sitini na kuahidi kuwa
utaendelezwa.
Aidha, Dk. Shein alieleza
kuwa kutokana na uhusiano na ushirikiano huo mkubwa kuna haja ya kuuendeleza na
kuuimarisha kwa lengo la kunufaika kwa pande zote hasa katika sekta za
maendeleo, kiuchumi na kijamii.
Dk. Shein alieleza haja
ya kuwepo kwa mashirikiano kati ya nchi hiyo na Zanzibar hasa katika sekta za
maendeleo ikiwemo sekta ya afya, biashara na viwanda, uwekezaji, kilimo,
usafiri na usafirishaji, miundombinu, uvuvi, mafuta na gesi pamoja na sekta
nyengine muhimu.
Katika maelezo yake Dk.
Shein alisema kuwa miongoni mwa vipaumbele vikubwa kwa upande wa Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania ni kuimarisha sekta ya viwanda na juhudi za makususdi
zinaendelea kuchukuliwa katika kuhakikisha sekta hiyo inaimarika.
Hivyo, Dk. Shein
alisisitiza haja ya nchi hiyo kuimarisha mashirikiano na Tanzania ikiwemo
Zanzibar katika kuimarisha sekta ya viwanda pamoja na biashara ambapo kwa
upande wa Indonesia sekta hizo zimepata maendeleo makubwa na kupiga hatua kubwa.
Akieleza kwa upande wa
sekta ya kilimo, Dk. Shein alieleza haja ya mashirikiano katika kuimarisha
sekta hiyo hasa katika eneo la utafiti na mafunzo katika sekta hiyo sambamba na
kuendeleza hatua zilizochukuliwa kwa pamoja na nchi hizo hapo siku za nyuma.
Katika sekta ya mafuta
na gesi, Dk. Shein alieleza kuwa Tanzania inatambua hatua zilizofikiwa na nchi
hiyo katika kuimarisha sekta hiyo na kueleza kuwa Tanzania iko tayari kupanua
wigo wa mafanikio hayo.
Sambamba na hayo, Dk.
Shein alieleza juhudi zinazochukuliwa katika kuimarisha sekta ya utalii nchini
Tanzania na kueleza haja ya kukuza ushirikiano katika kuazisha usafiri wa anga
kwa kutumia makampuni ya ndege kati ya nchi mbili hizo.
Pamoja na hayo, Dk.
Shein alimueleza kiongozi huyo kuwa sekta ya utalii ni miongoni mwa sekta
muhimu zinazochangia uchumi wa Zanzibar kwa kiasi kikubwa na ndio sababu sekta
hiyo imepewa kipaumbele katika Dira ya 2020.
Dk. Shein anatarajiwa
kurejea nchini kesho tarehe (9 Machi, 2017) baada ya kumaliza Mkutano wa Kwanza
wa Wakuu wa nchi na Serikali wa Jumuiya ya nchi zinazopakana na Bahari ya Hindi
(IORA), uliofanyika mjini Jakarta Indonesia ambapo alimuwakilisha Rais wa
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk. John Pombe Magufuli.
Mkutano huo wa siku tatu
ulianza Jumaapili ya tarehe 05 Machi na kufikia kilele tarehe 07 Machi mwaka
huu, mjini Jakarta Indonesia kwa kuanza na vikao vya Mawaziri na wadau wengine
kutoka nchi wanachama wa Jumuiya hiyo ya nchi zinazopakana na Bahari ya Hindi
(IORA) na hatimae Mkutano wa viongozi wakuu ulifanyika jana (Machi 7, mwaka
huu).
Sambamba
na Mkutano huo, Dk. Shein alishiriki katika utiaji saini wa Mkataba unaoainisha
mikakati, mipango na maazimio yanayolenga kuongeza kasi ya maendeleo ya Jumuiya
hiyo.
Katika
mkutano huo Dk. Shein alifuatana na Mke wa Rais wa Zanzibar Mama Mwanamwema
Shein, Waziri wa Biashara, Viwanda na Masoko, Balozi Amina Salum Ali, Waziri wa
Nchi, Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Issa, Haji Ussi Gavu,
Waziri wa Kilimo, Maliasili, Mifugo na Uvuvi, Hamad Rashid Mohammed, Naibu
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afika Mashariki, Dk. Susan Alphonce
Kolimba.
Wengine
ni Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya
Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Ramadhani Muombwa Mwinyi na
Mshauri wa Rais Masuala ya Ushirikiano wa Kimataifa, Uchumi na Uwekezaji Balozi
Mohamed Ramia Abdiwawa pamoja na watendaji wengine wa Serikali ya Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar.
Rajab
Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax:
024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment