Habari za Punde

Wananchi watakiwa kubuni miradi ya kimaendeleoili iwaletee tija

Habiba Zarali ,Pemba.

WANANCHI kisiwani Pemba, wametakiwa kuendelea kubuni miradi mbali mbali ya kimaendeleo inayoendana na mabadiliko ya tabia nchi, ili miradi hiyo iweze kuwaletea tija na mafanikio wananchi hao .

Kauli hiyo ilitolewa na Naibu  Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamo wa Rais Muungano na Mazingira wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Luhaga Joelson Mpina, alipokuwa akikaguwa mradi wa kuvuna maji ya mvua na mradi wa tuta la kuzuwia maji chumvi inayotekelezwa na mfuko wa hifadhi ya jamii Tanzania (TASAF 3) kisiwani Pemba.

Akikaguwa Tuta la kuzuwia maji ya mvua lenye ukubwa wa mita 200 lilioko Ndagoni Wilaya ya Chake chake, Mpina aliwapongeza Tasaf 3 kuibuwa miradi inayoendana na mabadiliko ya tabia nchi na mazingira na kusema itawawezesha  wananchi kupambana na umaskini kwa kudhibiti maji chumvi kutoingia katika mashamba hayo.

“ Mradi huu utawasaidia  nyinyi  wananchi wa Ndagoni kwa kuwaokolea mashamba yenu na maji ya chumvi ambayo maji haya  kila uchao yanasogea katika makaazi yenu jambo ambalo linaleta athari kubwa,”alisema.    

Akikaguwa mradi wa kuvuna maji ya mvua ulioko Kibokoni Vitongoji Wilaya ya Chake chake Pemba, Mpina alisema bwawa hilo litaleta tija na mafanikio makubwa kwa wakulima na wafugaji wa vitongoji.

“Kutokana na ardhi hii ya Vitongoji mumefanya jambo la busara kubuni mradi huu kwani kilimo na mifugo yenu itapata kunawiri kupitia bwawa hili”,alisema.

Alisema miradi hiyo haina ubaguzi wa aina yoyote na dhamira yake ni kuhakikisha watu wote wako sawa katika kipato chao, ili kila mmoja aweze kujikimu na maisha yake ya kila siku.

Mapema akitowa taarifa fupi ya mradi wa Tassaf 3, Kisiwani Pemba,  Mratibu wa Tasaf 3, Mussa Saidi Kisenge, alisema malengo ya mradi huo ni kuhakikisha unapomalizika wananchi wote wanaweza kujitegemea wenyewe katika kujipatia kipato ndani ya maisha yao.

Alisema miradi yote iliyotekelezwa imekamilika  na inafanya kazi kama ilivyokusudiwa na kuwaomba walengwa wa miradi hiyo kujiekea malengo ya kujiekea akiba kama yalivyo malengo ya miradi hiyo.

“Miradi hii kisiwani Pemba, inaendana na mahitaji husika ya wananchi wenyewe na eneo husika kwani kila sehemu inahitaji mradi kulingana na eneo lilivyo,”alisema .

Kwa upande wake Mkuu wa wilaya Chake chake, Salama Mbarouk Khatib, alisema lengo la mradi huo ni kuhakikisha kaya maskini wanajipatia kipato na kuondokana na Umaskini.

Aliwataka wananchi kushirikiana pamoja kwa kuwahimiza watoto wao kusoma pamoja na kuwapeleka watoto Klinik ili azma ya Serikali ya watoto kusoma na kuhudhuria Klinik iweze kufikiwa.


Hivyo wananchi walio faidika na miradi hiyo waliishukuru Serikali ya Muungano kwa kuona umuhimu wa kuwaletea wananchi miradi mbalimbali ambayo ni msaada katika kuendesha maisha yao.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.