Habari za Punde

Maulid Khamis Ahmed ( Lidi) mpiga picha alieweza kujikwamua

 Maulid Ahmed Khamis maarufu kama Lidi akiwa kazini akiwajibika
 Maulid Khamis Ahmed alipokutana na mwandishi wa habari hizi hivi karibuni
Na Zuhura Juma, PEMBA


“MTAJI wa masikini ni nguvu zake mwenyewe’’

Huu ni msemo maarufu sana uliotumika zama za karne nyingi nyuma, ambapo mpaka sasa unaendelea kutumika.
Sio kama kila mwenye nguvu ameshajiwekea mtaji wake, hapana…, lakini msemo huu, hutumika pale unapojikuta unajituma kufanya jambo ambalo litaweza kukukwamua na hali ngumu ya maisha.

Maana hivi sasa vijana wengi wameamua wakijiajiri wenyewe katika nyanja tofauti, kwa ajili ya kujitafutia riziki ili kuona nao wanapata maisha bora

Kama mwandishi wa makala hii alipokutana mjasiriamali maarufu katika mji wa Wete, ambae hujishughulisha na mambo mbali mbali yanayomkwamua na umasikini, ikiwemo ya uchukuaji picha (shooting).

Ni kijana mtanashati mwenye umri wa miaka 28, mkaazi wa Utaani Wete ndani ya kisiwa cha marashi ya karafuu cha Pemba, ambapo ni miaka saba sasa tokea kuanza kazi ya uchukuaji picha.

Ni Maulid Khamis Ahmed (LIDI) aliyevutika na fani ya uchukuaji picha za video, ambayo kwa sasa ni shughuli yake kubwa inayompatia kipato.

“Fani hii ndio shughuli yangu kubwa ambayo inanipatia tija kwa ajili ya kuendesha maisha yangu”, alidakiza mjasiriamali huyo.

Lidi alijikita katika kazi hiyo baada ya kushindwa kuendendelea na masomo ya chuo kikuu mwaka 2009.

“Nilipomaliza kidatu cha sita mwaka 2009 skuli ya Utaani, sikupata kuendelea na Chuo kikuu, kutokana na familia yangu kuwa na uwezo mdogo kifedha, hapo niliamua nitafute kitu chakufanya”, alieleza Lidi.

Kabla ya kujiingiza katika kazi hiyo, Lidi alijiunga katika chama cha malezi bora ‘Umati’ tawi la Pemba, ambapo alikaa hapo na kutoa  elimu kwa vijana wenzao kuhusiana na Ukimwi pamoja na malezi bora.

Huku akiwa yumo katika chama chicho, hakukaa kujipweteka (kutulia) tu, bali aliutumia muda wake mwengine kwenda kujifunza uchukuaji wa picha za ‘movie ’ hapo hapo mjini Wete
.
Ilipofika mwaka 2013 alianza kujichimbia kuisomea kazi ya kupiga picha kwa siku 90, aliielewa vyema ingawa aliamua kujiendeleza na kujichukulia umaarufu ndani na nje ya mji wa Wete.

“Sikukaa tu nikajituliza Umati, bali niliamua nikajifunza uchukuaji wa picha na sasa nashukuru maana huitwa sehemu mbali mbali katika shughuli kama za harusi”, alieleza
Aliwataja walimu waliomfundisha fani hiyo kuwa ni Sultan Ali Yussuf (Chani) na Saleh Mkubwa Mjaa (Tizo), wote wakiwa wakaazi wa Wete Pemba, ambao aliwashukuru sana kwa elimu waliyompa

“Baada ya kuijua kazi hiyo, sikuwa mchoyo nikaona jambo la msingi nifundishe vijana wenzangu, ninao wanafunzi wawili ambae ni Bashir Talib Khamis na Seif Bomoa”, alieleza huku akitabasamu.

Huku ukiwa uso wake unaonesha furaha kaka huyo, kwa sasa ameanzisha kampuni yake alioipa jina la ‘MSUO VIDEO PRODUCTION WETE PEMBA’  yenye makao makuu yake Chupa la soda mjini Wete, ambapo amewaajiri na wanafunzi wake.

Anasema ingawa hutegemeana na mwenye shughuli kama ya harusi au maulidi, lakini hujipatia kati ya shilingi 80,000 hadi shilingi 100,000 ambapo bei hiyo inaweza kubadilika.

Pamoja na kujikita katika fani hiyo, alivutika zaidi pale alipokuwa anachukua picha za uigizaji wa filamu huko Wete.
“Nilipoanza kuchukua picha za filamu, fani hii ilizidi kunivutia sana, kwani zimeweza kutoka na nyengine zinaendelea”, alisimulia.

Lidi baada ya kazi ya kupiga picha za video kumuingia magegoni, sasa ameshatanua mbawa zake, na kuaminiwa hadi kushuti hata michezo ya kuigiza.

“Kila nikichukua picha za harusi, maulidi, sherehe za kuzaliwa au mikutano, ndio napata umaarufu na fani imenikaa hasa moyoni na niko ‘fiti’, alijigamba.

Filamu ambazo aliweza kuzishuti ni pamoja na ‘NENO SAMAHANI, SABABU MAISHA YANGU, UCHUNGU WA MWANA KWA MZAZI, TAMIMA NA THE STRESS (MAWAZO)  ambazo tayari zimeshatoka na cd zake kuuzwa.
Filamu nyengine ambayo anaendelea nayo kuishuti  kwa muda huu ni pamoja na ‘PENZI LA MUUNGANO’ ambapo waandaji wa mchezo huo ni waigizaji kutoka vikundi tofauti vya mji wa Wete.

Lidi anaeleza kuwa kuna tofauti ya kushuti filamu za mikutano au harusi, kwani filamu unatumia aina ya picha nzima ‘long short, au kipiande ‘medium na za ukaribu mno ‘close up’, ambapo mikutano na harusi unapiga picha nzima ‘long short’.

Tabu anayoipata Lidi wakati wa kushuti mchezo wa kuigiza ni ukaidi kwa wasanii wakati wa kuongoza na kuchelewa kufika kwenye maeneo (location) wanayotumia.

“Wasanii baadhi yao wanakuwa wakaidi wakati wa kuongoza, kwani unapomwambia fanya hivi….. yeye anaona kama unamuhangaisha”, alieleza.

Kushuti mchezo mmoja wenye sehemu mbili (part one na two) huchukua muda wa wiki mbili ingawa inategemea wepesi wa wasanii au mpiga picha mwenyewe.  

Utaalamu kwa vile ni jambo la lazima popote, nae Lidi anasema, unatumika katika kushuti mchezo au jambo jengine, ikiwa ni pamoja na kuangalia kamera mara kwa mara.

Jengine la msingi anaona ni kuangalia kila wakati aina ya picha ili usiirudie kwa mtendo moja, kufahamu kipande au sehemu wanayoigiza wanapokuwa jukwaani (sini) na kupiga shoti kila sini.

Kijana huyo anasema wakati mzuri wa kushuti mchezo ni muda wa asubuhi kabla ya jua kuwa kali, au jioni jua linapoanza kuzama taratibu.

“Au inategemea muongozo wa sini unazotaka kuzishuti kwa sababu pengine wanapenda kipande kionekane jua kali au mvua”, anaeleza.

Yeye anaposhuti michezo lazima aandae muongozo (script), kwani humsaidia na kumrahisishia kazi yake hiyo bila ya matatizo.

Anafahamisha kuwa, anaporudi kushuti mchezo (filamu) huhifadhi kazi yake katika kompiyuta, ambapo pia humo ndimo anapotengenezea kazi yake hiyo.

Pamoja na hayo, lidi hakuacha kusema tatizo analoliona kwa wasanii wakati wa kushuti, kuwa ni pale wanapoongea vile walivyopangiwa mwanzo na wakati wa kushuti kubadilisha maongezi.

Lidi anasema kushuti mchezo hadi kumalizika ni wastani ni shilingi 800,000 (ahilingi laki nane) ingawa kwa Pemba ni kinyume chake kwani yeye hulipwa chini ya kiwango hicho.

Kuna mafanikio mbali mbali aliyoyapata Maulid katika fani hiyo ikiwa ni pamoja na kupata fedha za kujikimu na maisha, kupata umaarufu, kutembea sehemu tofauti nje ya Zanzibar ikiwemo Tanga, Dar-es-salaam, Arusha na Nairobi.

Kila penye mafanikio hapakosi kuwa na matatizo, Lidi anakabiliwa na changamoto ya upungufu wa vifaa vya kufanyia kazi, jambo ambalo linamkwaza katika kazi yake.

Changamoto nyengine inayomkabili ni kukosa usafiri wa kwenda katika shughuli yenyewe, ambapo hutembea masafa marefu mpaka kufika sehemu yenye shughuli
.
“Sehemu nyengine hazina usafiri hivyo hulazimika kupiga mguu, pia ni unaweza kupata mtetemo (shoti) wakati wa kupanga vifaa na wakati mwengine kugombana na wateja kwa malipo”, alieleza Lidi.

“Mtu anakwita ukamchukulie picha katika shughuli yake, lakini cha kushangaza wakati wa malipo wanakuwa wagumu mno, jambo ambalo linarejesha nyuma’’,alifafanua.

Katika siku aliyokuwa hatoisahau maishani yake kwenye fani hiyo, ni pale alipopata hitilafu ‘short’ ya umeme katika Ukumbi wa Jamhuri Wete wakati wa kupanga, ambapo alipata majeraha ya kuungua ingawa sio sana.

Kijana huyo alitoa hisia zake kuwa, malengo yake ya baadae ni kukikuza zaidi kipaji chake hicho na kuona kwamba anapata maisha mazuri ya baadae.

Pamoja na kazi ya uchukuaji picha, Lidi pia ni mjasiriamali,  muigizaji wa filamu za Kiswahili na  muelimishaji rika katika chama cha malezi bora ‘Umati’ tawi la Pemba.

Alitoa wito kwa vijana wenzake kuwa, waweze kujiajiri wenyewe bila ya kutegemea serikali, kwani haina uwezo wa kuajiri watu wote nchini.

Muigizaji Rabia Suleiman Salum mkaazi wa Jadida Wete anasema Lidi ni mpiga picha mzuri, ambaye wanampenda sana katika kikundi chao cha uigizaji cha ‘Msuo Group’

Bashir Talib Khamis ambae ni mwanafunzi wa Lidi alimsifu mwalimu wake kwa ushirikiano anaouonesha wakati alipokuwa akiwafundisha na hata sasa katika utendaji wa kazi zao.

“Mwalimu wetu yuko vizuri sana, katufundisha kwa nia njema kabisa na sasa ametuajiri katika kampuni yake ya MSUO tunafanyakazi kwa pamoja” alisifu Bashiri.  

Mmoja wa mwalimu aliyemsomesha Lidi, Sultani Ali Yussuf (Chani) anasema kijana huyo alimsomesha fani ya uchukuaji picha kwa muda mdogo sana, ambapo kwa sasa anafanya shughuli zake bila kuongozwa.

“Lidi ni kijana mzuri sana, mstahamilivu na mimi mpaka sasa nikiwa na kazi yangu naweza kumtuma na wala hakatai, hilo nimejivunia kama mwalimu”, alijinadi mwalimu huyo.

Chani aliiomba serikali iwaangalie vijana wanaojitolea kama Lidi na kuwawezesha kwa kuanzisha taasisi ambazo zitaweza kuwakwamua na umasikini kwa kupewa mikopo.

Lidi ni mzaliwa wa Mtambwe Kele shehia ya Mtambwe Kaskazini Wilaya ya Wete Pemba, akiwa mtoto wa pili kuzaliwa katika familia ya watu wanne.

Amepata elimu yake ya msingi katika skuli ya Uondwe Mtambwe na kufaulu michepuo, ambapo alijiunga katika skuli ya sekondari Utaani na kumaliza kidatu cha sita.

Alipofika umri wa miaka 31, Lidi alilihama jumba la upweke, na kufunga ndoa na mwandani wake kutoka wilaya ya Mkoani, na leo Allah ameshampa mtoto mmoja wa kike.

Kwa sasa anaishi mtaa wa Kipangani mji maarufu kwa halua, wa Wete na anasema hulala jicho moja na la pili kusikiliza wapi kuna shuguli za kupiga picha za video ili nae mkono uwende kinywani.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.