Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk Shein Alihutubia Baraza la Eid Fumba leo.

STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
Zanzibar                                                                  01.09.2017
---
OFISI ya Mufti na viongozi wa dini hapa nchini wametakiwa kushirikiana na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kufanikisha utekelezaji wa Mpango Kazi wa Zanzibar wa miaka mitano wa kupambana na vitendo vya ukatili na udhalilishaji dhidi ya wanawake na watoto.

Hayo yameelezwa leo na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Alhaj Dk. Ali Mohamed Shein, katika hotuba yake ya Baraza la Idd el Hajj, aliyoitoa huko Fumba, Wilaya ya Magharibi ‘B’, Mkoa wa Mjini Magharibi Unguja katika eneo la nyumba za mradi wa Makampuni ya Said Salim Bakhressa.

Hafla ambayo ilihudhuriwa na viongozi mbali mbali akiwemo Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan, Makamu Pili wa Rais Zanzibar Balozi Seif Ali Idd na viongozi wengine wa dini na Serikali pamoja na wananchi.

Alhaj Dk. Shein alisema kuwa Ofisi ya Mufti ni vyema iwe inavifuatilia kwa karibu vyuo vyote vya Qur-an ikiwemo kuvijua mahali vilipo, walimu wanaofundisha katika vyuo hivyo pamoja na kujua sifa zao.

Alieleza kuwa hatua hiyo itasaidia kuwadhibiti walimu wachache wanaokiuka misingi na maadili mema wakati wa utekelezaji wa majukumu yao na kutoa nasaha kwa Mashehe na Maimamu wote kufanya juhudi za kuielimisha jamii juu ya Mpango huo kupitia mawaidha wanayotoa misikitini na katika hotuba za sala ya Ijumaa.

Kadhalika, Dk. Shein alieleza kuwa viongozi wa dini nyengine nao wana jukumu la kuwaelimisha wafuasi wa dini zao na jamii nzima kwa jumla juu ya umuhimu wa kufuata maadili mema na kuepuka vitendo viovu vya udhalilishaji wanawake na watoto.

Katika jitihada za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar za kupambana na vitendo vya udhalilishaji, wiki iliyopita tarehe 26 Agosti, 2017, Dk. Shein alizindua Mpango Kazi wa Zanzibar wa miaka 5 wa Kupambana na Vitendo vya Ukatili na Udhalilishaji dhidi ya Wanawake na Watoto unaoanza mwaka huu hadi mwaka 2022.

Aidha,  Alhaj Dk. Shein alisema kuwa jamii kwa pamoja ina wajibu wa kuchukua hatua kwa kushirikiana na Masheha pamoja na vikundi vya ulinzi shirikishi na vyombo vya ulinzi na usalama ili kuhakikisha vitendo vya vijana kuwasumbua wananchi hasa wanawake kwa kuwavamia na kuwanyanganya vitu vyao, vinakomeshwa.

Aliongeza kuwa zipo taarifa za kuongezeka kwa vitendo vya wizi wa mifugo, mazao pamoja na uchimbaji ovyo wa mchanga katika maeneo yasioruhusiwa, vitendo ambavyo vinafanywa na vijana waliokosa maadili bora na malezi mema vinahatarisha amani na usalama wa wananchi na mali zao pamoja na uharibifu wa mazingira.

Kwa upande wa ukusanyaji wa mapato hapa nchini, Alhaj Dk. Shein ameendelea kusisitiza haja kwa wafanyabiashara kutoa risiti na wananchi nao kudai risiti wakati wa kuuza na kununu bidhaa kwani hivyo ndivyo ilivyo sheria.

Alisema kuwa Uislamu umehimiza uadilifu katika biashara kwa hivyo utoaji wa risiti sahihi ni kitendo cha kufanya uadilifu kati ya muuzaji na mnunuzi,  na kutoa wito kwa Bodi ya Mapato Zanzibar (ZRB) na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) kutoa elimu kwa wafanyabiashara juu ya umuhimu wa kutoa risiti kwa mauzo wanayoyafanya.

Pamoja na hayo, Dk. Shein alitumia fursa hiyo kuwapongeza wananchi wa Mikoa yote kwa juhudi wanazozichukua katika kuijenga nchi yao, kuimarisha mshikamano pamoja na kudumisha amani na utulivu hali ambayo aliiyona katika ziara yake hivi karibuni.

Aidha, aliwapongeza viongozi walioshiriki katika kuifanikisha ziara hiyo katika Mikoa yote na Wilaya za Unguja na Pemba kuanzia Agosti 12 hadi 26 kwa madumuni ya kuona na kufahamu juhudi za utekelezaji wa Ilani ya CCM ya Uchaguzi Mkuu ya mwaka 2015-2020 na mipango mengine ya Maendeleo iliyopangwa kuwatumikia wananchi na kuwaletea maendeleo.

Alhaj Dk. Shein alitumia fursa hiyo kutoa pongezi kwa vyombo vya habari kwa kufuatilia kwa karibu zaidi ziara za Mikoa na kuwapa wananchi taarifa kwa wakati juu ya matukio mbali mbali ya ziara za mikoa alizozifanya.

Alhaj Dk. Shein, alitoa pongezi kwa uongozi wa Mkoa wa Mjini Magharibi na Wilaya zake, taasisi na vyombo vya ulinzi na usalama na wananchi wote kwa jitihada zinazochukuliwa katika kusimamia amani na utulivu.


Akitoa nasaha zake kwa wananchi, Alhaj Dk. Shein alitaka jitihada hizo ziwe za kudumu na wananchi waendelee kushirikiana na Serikali kwani jukumu la kusimamia amani na usalama ni la kila raia mwema na sio viongozi wa serikali na vyombo vya ulinzi peke yao.

Alisisitiza kuwa Serikali zote mbili ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar zote kwa pamoja zitaendelea kuhakikisha kuwa wananchi na mali zao na wageni wanaoitembelea Tanzania wapo salama na wanaendelea kufanya shughuli zao bila ya hofu.

“Bila ya amani hakuna maendeleo, bila ya amani watu watashindwa hata kufanya ibada jambo ambalo tumekuwa tukikumbusha kila tunapopata wasaa kutokana na umuhimu wake…tumuombe Mwenyezi Mungu aendelee kutukirimu neema”,alisema Alhaj Shein.

Aidha, Alhaj Dk. Shein alieleza kuwa Serikali itaendelea kuchukua hatua madhubuti katika kudhibiti na kupambana na uingizaji, usambazaji na utumiaji wa dawa za kulevya na kuwaomba wananchi kuendelea kushirikiana na vyombo husika ili kuzidi kuwaokoa vijana wanaoathirika na dawa za kulevya na ukimwi.

Alhaj Dk. Shein alisisitiza haja ya kuongeza jitihada katika kupeana elimu sahihi juu ya maambukizo ya virusi vya UKIMWI, kutoa huduma nzuri kwa walioathirika, kukomesha unyanyapaa pamoja na kuzilinda haki za waathirika.

Aliongeza kuwa bado tatizo la UKIMWI lipo ambapo Zanzibar hivi sasa ina watu 15,122 wanaoishi na virusi vya UKIMWI, idadi ambayo inakadiriwa kuwa sawa na asilimia 1 ya idadi ya Wazanzibari wote.

Mapema asubuhi aliungana na Waumini wa dini ya Kiislamu katika  sala ya Idd el Hajj katika uwanja wa mpira Dimani, Wilaya ya Magharibi ‘B’, Mkoa wa Mjini Magharibi na baadae alikutana na kusalimiana na Mashekh pamoja na viongozi mbali mbali katika ukumbi wa moja wapo ya nyumba za mradi wa Makampuni ya Said Bakhressa na kumpongeza mfanyabiashara huyo kwa kukubali eneo hilo kufanyika shughuli hizo.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449.  Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.