Habari za Punde

Rais wa Zanzibar Dk. Shein Azungumza nac Uongozi wa Wizara ya Fedha Zanzibar.

STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
  Zanzibar                                                                                                                           26.10.2017
---
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein,  ameeleza kuwa Uchumi wa Zanzibar unazidi kuimarika siku hadi siku kutokana na uongozi uliopo kuwa na mashirikiano ya pamoja katika kutekeleza mikakati iliyowekwa na Serikali.

Dk. Shein aliyasema hayo leo, Ikulu mjini Zanzibar alipokutana na uongozi wa Wizara ya Fedha na Mipango wakati ilipowasilisha utekelezaji wa Mpango Kazi wa Mwaka 2016/2017, Mpango Kazi wa Utekelezaji kwa mwaka 2017/2018 na Utekelezaji wake kwa  kipindi cha robo ya kwanza ya Julai hadi Septemba, 2017.

Dk. Shein alieleza kuridhishwa na hatua zinazoendelea kuchukuliwa na uongozi wa Wizara hiyo katika kuhakikisha mapato yanaimarika na nchi inaendelea kupata maendeleo endelevu na kutumia fursa hiyo kuzipongeza juhudi hizo.

“Endeleeni na juhudi zenu, mmejitahidi sana na kila mmmoja ametekeleza wajibu wake, na kwa vile mmefanya kazi wka pamoja mmeona matokeo yake”alisema Dk. Shein.

Aliongeza kuwa leo Zanzibar inasifiwa duniani kote kwa kuanzisha Penjeni jamii kwa wananchi wake waliokusudiwa, ambapo kila mwezi kiwango cha fedha maalum kimetengwa kwa ajili ya malipo hayo.

Alieleza kuwa katika kipindi hichi Serikali imetangaza kuondoa michango ya wazee kwa watoto wao skuli, kutokana na Setikali kujipanga vyema kifedha ikiwa ni pamoja na kuendeleza juhudi zile zile zilizochukuliwa katika ununuzi wa meli ya MV Mapinduzi II jambo ambalo limewezekana.

Aidha, Dk. Shein alisisitiza kwua Serikali itahakikisha inapata mafanikio ikiwa ni pamoja na kuhakikisha inaendelea kuyatekeleza yale yote yaliyoasisiwa na Marehemu Mzee Abeid Amani Karume ikiwa ni pamoja na kuhakikisha afya pamoja na elimu vinatolewa bure.
Pamoja na hayo, Rais aliuagiza uongozi wa Wizara ya Fedha kulishughulikia suala la msongamano wa wananchi katika kupata huduma za Benki jambo ambalo limekuwa likilalamikiwa na wananchi kwa kipindi kirefu na tayari ameshaawahi kulitoa agizo katika hotuba zake mbali mbali.

Dk. Shein alisisitiza kuwa licha ya changamoto chache zilizopo katika sekta ya afya na elimu lakini bado Zanzibar imeweza kupiga hatua kubwa katika sekta hizo ikilinganishwa na nchi nyenginezo za bara la Afrika.

Alieleza kuwa suala zima la utegemezi wa Bajeti ya Zanzibar imeweza kupata mafanikio na hivi sasa utegemezi umefikia asilimia 7.2 ikilinganishwa na wakati anaingia madarakani mwaka 2010 ambapo utegemezi ulikuwa asilimia 32.

Pamoja na hayo, Dk. Shein  alisisitiza haja ya kufanywa utafiti na iwapo Wizara itafanya utafiti itasaidia kwa kiasi kikubwa kupata majibu ambayo huwa magumu kupatikana na ndio maana Serikali ikaunda Idara ya Mipango Sera na Utafiti kwa kila Wizara kwa lengo la kupanga mipango ya maendeleo.

Nae Katibu Mkuu Kiongozi na Katibu wa Baraza la Mapinduzi Dk. Abdulhamid Yahya Mzee aliipongeza Wizara hiyo pamoja na taasisi zake zote kutokana na mafanikio makubwa iliyoyapata huku akisisitiza haja ya kuviangalia viinua mgogo.  

Waziri wa Wizara ya Fedha na Mipango Dk. Khalid Salum Mohamed alieleza kuwa uchumi wa Zanzibar umeendelea kuimarika mwaka hadi mwaka sambamba na kasi ya ukuaji uchumi kuimaika zaidi na kufikia asilimia 6.3 ikilinganishwa na kasi ya ukuaji wa asilimia 5.2 kwa kipindi kama hicho cha robo mwaka ya kwanza ya mwaka 2016.  

Aliongeza kuwa hali hiyo imetokana na kuimarika zaidi kwa sekta ya huduma hususan katika sekta ndogo ndogo ya huduma za hoteli na mikahawa kutokana na kuongezeka kwa idadi ya watalii walioingia nchini.

Dk. Khalid alieleza kuwa  Wizara inaendelea na jitihada zake za kuimarisha ukusanyaji wa mapato ya ndani, kusimamia vyema Sheria ikiwemo Sheria mpya za Fedha za Umma na Ununuzi na Uondoshaji wa Mali za Serikali na kusimamia matumizi ya fedha hizo za umma.

Wizara pia, itaendelea kufuatilia utekelezaji wa Miradi ya maendeleo na kushauri hatua za kurekebisha pale zinapojitokeza kasoro.

Waziri Khalid alieleza kuwa Wizara inashukuru sana imani inayoendelea kupata kutoka kwa  Rais Dk. Shein pamoja na Makamo wa Pili Balozi Seif Ali Idd na kuongeza kuwa miongozo ya Serikali  imeendelea kurahisiaha utekezaji wa majukumu ya Wizara.

Sambamba na hayo, uongozi huo ulieleza kuwa tayari umeshaanza kulishugulikia tatizo la msongamano wa watu katika kupata huduma za Benki kwa kuchukua hatua mbali mbali ikiwa ni pamoja na kuimarisha huduma za malipo kwa njia za mitandao ya simu, pamoja na kukamilisha taratibu zitakazowesha huduma hizo kutolewa na mawakala wa huduma za simu.


Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.