Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dkt. Ali Mohamed Shein, Akutana na Mwakilishi Mkaazi wa (UNIDO)

Rais wa Zanzibar na Mweyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein (kulia) alipokuwa akisalimiana na Mwakilishi Mkaazi wa Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshuhulikia Maendeleo ya Viwanda (UNIDO) Bw.Stephen B.Kargo   alipofika Ikulu Mjini Unguja leo
Rais wa Zanzibar na Mweyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein (kulia) alipokuwa akizungumza na mgeni wake  Mwakilishi Mkaazi wa Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshuhulikia Maendeleo ya Viwanda (UNIDO) Bw.Stephen B.Kargo   alipofika Ikulu Mjini Unguja leo
Rais wa Zanzibar na Mweyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein (kulia)  akifuatana  na mgeni wake   Mwakilishi Mkaazi wa Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshuhulikia Maendeleo ya Viwanda (UNIDO) Bw.Stephen B.Kargo baada ya mazungumzo yao alipofika Ikulu Mjini Unguja leo,[Picha na Ikulu.] 17/10 /2017.
STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
Zanzibar                                                                                                                 17.10.2017
---
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein ameeleza haja kwa Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia Maendeleo ya Viwanda (UNIDO) kuendelea kuiunga mkono Zanzibar katika kuimarisha sekta ya viwanda hatua ambayo itawasaidia hata vijana kujipatia ajira pamoja na kukuza pato la taifa.

Dk. Shein aliyasema hayo leo Ikulu mjini Zanzibar wakati alipokuwa na mazungumzo na Stephen Kargbo Mwakilishi Mkaazi wa Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia Maendeleo ya Viwanda (UNIDO).

Katika mazungumzo hayo, Dk. Shein alimueleza Mwakilishi Mkaazi huyo kuwa kwa kutumia uzoefu na utaalamu wa Shirika hilo, ni vyema likaishauri na kuisaidia Zanzibar katika kutekeleza azma yake ya kuimarisha sekta ya viwanda hasa vidogo vidogo sekta ambayo iwapo itatiliwa mkazo itasaidia kukwamua changamoto ya ajira kwa vijana.

Dk. Shein alitumia fursa hiyo kumueleza Mwakilishi huyo Mkaazi mikakati pamoja na malengo ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ikiwemo Dira ya Maendeleo ya 2020, MKUZA III, katika kupambana na umasikini sambamba na tatizo la ajira kwa vijana.

Dk. Shein alilipongeza Shirika hilo la Umoja wa Mataifa ambalo limekuwa na historia kubwa ya mashirikiano kati yake na Zanzibar kwa kuendelea kuiunga mkono Zanzibar katika kuimarisha sekta zake za maendeleo.

Aidha, Dk. Shein alieleza haja ya kuungwa mkono wakulima wa zao la mwani kutokana na zao hilo kuwa na bei ndogo jambo ambalo limekuwa likiwarejesha nyuma wakulima wa zao hilo ambalo  kwa upande wa Zanzibar nchi ya tatu duniani kuzalisha zao hilo.

Kutokana na uzoefu wa Shirika hilo, Dk. Shein alieleza haja kwa UNIDO kushirikiana na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kupitia Taasisi zake ili kuweza kusaidia mbinu na maarifa katika kufanikisha sekta hiyo ya viwanda.

Pamoja na hayo, Dk. Shein alimueleza Mwakilishi huyo kuwa katika kutekeleza Uchumi wa Bahari, Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imo katika hatua ya kuanzisha Kampuni ya uvuvi, ambapo Serikali itaanza kwa kununua meli mbili za uvuvi, hatua ambayo pia itatekeleza malengo ya Jumuiya ya nchi zilizopakana na Bahari ya Hindi (IORA).

Sambamba na hayo, Dk. Shein alieleza kuwa Serikali imekuwa ikiimarisha sekta ya utalii, ikiwa ni mbadala wa sekta ya kilimo, sekta ambayo itapata mafanikio mazuri iwapo sekta ya viwanda itaimarika zaidi kwani utalii umeweza kuchangia fedha za kigeni kwa asilimia 80.

Nae Mwakilishi Mkaazi wa Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia Maendeleo ya Viwanda (UNIDO), Stephen Kargbo alimueleza Dk. Shein kuwa kipaumbele kikubwa kilichowekwa na Shirika hilo hivi sasa ni uimarishaji wa viwanda hasa kwa nchi za bara la Afrika, na kuahidi kuiunga mkono  Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika sekta hiyo.

Katika maelezo yake Mwakilishi huyo Mkaazi alimueleza Dk. Shein hatua na mikakati iliyowekwa na Shirika hilo katika kusaidia sekta za maendeleo ikiwemo sekta ya viwanda na kueleza hatua zitakazochukuliwa na Shirika hilo kwa upande wa Zanzibar.

Aliongeza kuwa UNIDO ina mipango kabambe katika kuiunga mkono Zanzibar ili iweze kupiga hatua katika azma yake ya kuimarisha sekta ya viwanda.

Wakati huo huo, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein alikutana na Balozi wa Uganda nchini Tanzania Richard Mabonero, Ikulu mjini Zanzibar ambapo katika mazungumzo yao viongozi hao walisisitiza haja ya kuendeleza na kuimarisha uhusiano na ushirikiano wa kihistoria uliopo.

Katika maelezo yake Dk. Shein alimueleza Balozi huyo kuwa Uganda imekuwa na mashirikiano mazuri na Tanzania hasa katika sekta ya elimu kwani nchi za Afrika Mashariki ikiwemo Tanzania kabla ya kuwa na vyuo vyake vikuu Watanzania walio wengi wamepata elimu yao ya juu kutoka Chuo Kikuu cha Makerere cha nchini humo.

Aidha, aliipokea rai ya Balozi Mabonero ya Zanzibar kuisaidia nchi hiyo katika kuiimarisha lugha ya Kiswahili kwa kuwapatia walimu huku Dk. Shein akisisitiza haja ya kuwepo kwa mashirikiano katika kubadilishana uzoefu na utaalamu kati ya vyuo vikuu vya Uganda na vyuo vikuu vya Zanzibar kikiwemo chuo Kikuu cha Taifa cha Zanzibar (SUZA).

Dk. Shein alisema kuwa kuwepo kwa usafiri wa ndege kati ya Uganda na Zanzibar kutaimarisha sekta ya utalii kwa pande zote mbili huku Rais Dk. Shein akitumia fursa hiyo kumpongeza Rais Yoweri Kaguta Museven kwa kufanikisha nchi yake kutoa mafuta na gesi.

Nae Balozi huyo wa Uganda nchini Tanzania Richard Mabonero alitoa pongezi kwa Dk. Shein kwa mafanikio makubwa yaliopataikana hapa Zanzibar na kueleza kuwa nchi yake itaendeleza uhusiano na ushirikiano wa kihistoria uliopo kati yake na Tanzania ikiwemo Zanzibar.

Balozi huyo alisisitiza haja ya kuwepo kwa mashirikiano ya pamoja kati ya Zanzibar na Uganda hasa katika usafiri wa ndege sambamba na kutoa ombi maalum la kutaka kusaidiwa kukiendeleza na kukikuza Kiswahili nchini mwao kwa kupata wakufunzi kutoka Zanzibar kwa kutambua kuwa Zanzibar ndio chimbuko la lugha ya Kiswahili.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk


No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.