Habari za Punde

Balozi wa China nchini akutana na Rais Dk Shein kujitambulisha

STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
  Zanzibar                                                                                                              27.11.2017
---
SERIKALI ya Jamhuri ya Watu wa China imeahidi kuendelea kuiunga mkono Zanzibar katika kuendeleza miradi mikubwa ya maendeleo ukiwemo ukamilishaji ujenzi wa jengo jipya la abiria la uwanja wa ndege wa Abeid Amani Karume pamoja na ujenzi wa bandari mpya ya Mpigaduri ili kukuza uchumi wa Zanzibar.

Balozi wa  Jamhuri ya Watu wa China nchini Tanzania Mhe. Wang Ke, aliyasema hayo leo wakati alipofika Ikulu mjini Zanzibar kwa ajili ya kujitambulisha pamoja na kufanya mazungumzo na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein.

Katika mazungumzo hayo, Balozi Wang Ke alimueleza Dk. Shein kuwa Serikali ya Jamhuri ya Watu wa China itahakikisha inatoa ushirikiano katika kutekeleza miradi hiyo mikubwa katika taratibu zote zilizopangwa kwa lengo la kuendeleza na kukuza uhusiano na ushirikiano wa kihistoria uliopo kati ya Zanzibar na Jamhuri ya Watu wa China.

Balozi huyo alimueleza Dk. Shein kuwa nchi yake itahakikisha mradi wa ujenzi wa jengo la abiria katika uwanja wa ndege wa Kimatifa wa Zanzibar unakamilika katika kipindi kifupi kijacho huku akisisitiza kuwa mradi wa ujenzi wa bandari ya Mpigaduri nao utatekelezwa kama ulivyopangwa.

Aidha, Balozi Wang Ke, alimuhakikishia Dk. Shein kuwa China itaendelea kuisaidia na kuiunga mkono Zanzibar katika kuimarisha uchumi wake ikiwa ni pamoja na kuahidi kuleta wawekezaji kwa ajili ya kujenga viwanda vinavyotokana na rasilimali za bahari kwa lengo la kukuza sekta ya uvuvi na sekta ya viwanda hapa nchini.

Pamoja na hayo, Balozi huyo alimuhakikishia Dk. Shein kuwa mara baada ya kumalizika kwa miradi hiyo nchi yake itakuwa tayari kuunga mkono katika kuanzisha miradi mipya mengine mikubwa hapa Zanzibar kwa siku za usoni kwa ajili ya kuimarisha uchumi na maendeleo endelevu hapa Zanzibar.

Pia, Balozi huyo alitumia fursa hiyo, kumpsa salamu Dk. Shein zinazotoka kwa Rais wa Jamhuri ya Watu wa China Rais Xi Jinping, zinazompongeza Rais Dk. Shein pamoja na wananchi wa Zanzibar huku akiahidi kuendelea kuiunga mkono Zanzibar katika sekta mbali mbali za maendeleo.

Balozi Wang Ke, alipongeza mashirikiano yaliopo katika kuimarisha sekta ya afya ambapo nchi yake imesaidia ujenzi wa Hospitali ya Abdalla Mzee huko Pemba, kuendelea kuleta Madaktari kwa awamu kutoka nchini humo na kuahidi kuendeleza mashirikiano katika sekta za elimu, kilimo, uvuvi, miundombinu,viwanda na nyenginezo.

Nae Rais Dk. Shein kwa upande wake alimpongeza Balozi Wang Ke pamoja na nchi yake na kusisitiza kuwa Zanzibar itaendelea kufuata misingi iliyowekwa na waasisi wa nchi hizo akiwemo marehemu Maotse Tung, Marehemu Mwalimu Julius Nyerere na Marehemu Mzee Abeid Amani Karume ambao bado juhudi zao zinathaminiwa.

Dk. Shein alisema kuwa ni miaka 54 tokea Zanzibar na China zianzishe ushirikiano na uhusiano wao wa kihistoria Zanzibar ambapo mafanikio makubwa yameweza kupatikana huku akieleza kuwa kukamilika kwa jengo hilo la abiria katika uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Zanzibar kutaimarisha uchumi na kukuza sekta ya utalii.

 Katika mazungumzo hayo Dk. Shein alisema kuwa China imekutoa mchango mkubwa katika kufanikisha sekta za maendeleo ikiwemo sekta ya afya, viwanda, kikiwemo kiwanda cha sukari, elimu, michezo, kilimo cha mpunga na kueleza haja ya kwa nchi hiyo kuanzisha viwanda vitakavyotokana na rasilimali ya bahari hapa Zanzibar.

Aliipongeza Serikali ya China chini ya kiongozi wake Rais Xi Jinping kwa kuendelea kuisaidia na kuiunga mkono Zanzibar katika kuendeleza miradi mbali mbali ya maendeleo na kuipongeza nchi hiyo kwa mafanikio inayoendelea kuyapata.

Wakati huo huo, Rais Dk. Shein alikutana na  Balozi wa Tanzania nchini Misri Jenerali Issa Suleiman Nassor na Balozi Tanzania nchini Zambia Mhe. Abrahman Kaniki, waliofika Ikulu mjini Zanzibar kwa ajili ya kuaga.

Katika maelezo yake Rais Dk. Shein aliwasisitiza Mabalozi hao kulipa kipaumbele suala zima la uchumi wa kidiplomasia hasa kwa vile Tanzania ikiwemo Zanzibar imejikita katika kukuza uchumi wake kupitia sekta ya viwanda.

Pia, alitilia mkazo makubaliano ya  mkutano wa Jumuiya ya Nchi zinazopakana na Bahari ya Hindi (IORA) uliofanyika mjini Jakata Indonesia mnamo mwezi Machi mwaka huu ambao ulisisitiza juu ya uchumi wa Bahari ikiwa ni pamoja na kuanzisha viwanda vinavyotokana na rasilimali za bahari kwa nchi wanachama ambapo Zanzibar nayo imo katika mikakati ya kuelekea huko.

Aidha, Dk. Shein aliwasisitiza viongozi hao kuchukua juhudi za makusudi za kuwavutia wawekezaji ili kuja kuekeza Tanzania sambamba na kuitangaza Tanzania ikiwemo Zanzibar kiutalii kutokana na vivutio vingi vilivyopo pamoja na kuyashajiisha Makampuni ya ndege likiwemo Shirika la ndege la Misri ‘Egytian Air’ kufanya safari zake na Zanzibar kwa lengo la kukuza sekta hiyo ya utalii.

Nao Mabalozi hao, waliahidi kutekeleza vyema kazi zao watakapokuwa vituoni mwao na kusisitiza kuwa watahakikisha wanatoa mchango wao mkubwa katika kuitangaza Tanzania kiutalii, kuwavutia wawekezaji, kuimarisha na kukuza uhusiano na ushirikirikiano kupitia Reli ya TAZARA ambayo ipo kati ya Tanzania na Zambia.

Dk.Shein pia, alikutana na Jaji Mkuu wa Tanzania Profesa Ibrahim Hamis ambaye alifika Ikulu mjini Zanzibar kwa ajili ya kujitambulisha pamoja na kufanya nae mazungumzo.

Katika mazungumzo hayo, Dk. Shein alieleza kuwa anafarajika na utendaji kazi wa mihimili  yote mitatu mikuu ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ambayo inafanya kazi ikiwa huru na kwa mujibu wa Katiba zote za Serikali hizo tena kwa mashirikiano makubwa ambapo alisisitiza haja ya kuimarishwa kwa pande zote mbili.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.