WANANCHI wa Mkoa wa Kaskazini Unguja wamempongeza Rais wa
Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Alhaj Dk.Ali Mohamed Shein kwa
kuendelea kuwathamini na kuwatekelezea ahadi alizowaahidi ikiwa ni pamoja na
kuwatengenezea barabara yao inayotoka Bububu hadi Mkokotoni.
Akitoa neno la
shukurani kwa niaba ya Alhaj Dk. Shein, Mkuu wa Mkoa wa Kaskazini Unguja Vuai
Mwinyi katika futari maalum aliyowaandalia wananchi pamoja na viongozi mbali
mbali wa dini, vyama vya siasa na serikali wa Mkoa huo, hafla iliyofanyika katika viwanja vya Ikulu ndogo
ya Mkokotoni iliyopo katika Mkoa huo.
Mke wa Rais wa
Zanzibar Mama Mwanamwema Shein nae aliungana pamoja na wananchi pamoja na
viongozi mbali mbali wa Mkoa huo katika futari hiyo maalum.
Wananchi hao wa Mkoa
wa Kaskazini Unguja walizipongeza juhudi za Rais Dk. Shein na kueleza jinsi
wanavyothamini maendeleo yote aliyowapelekea pamoja na juhudi zake za
kuwatengenezea barabara hiyo ambayo kwa maelezo ya Mkuu huyo wa Mkoa ujenzi
wake utaanza rasmi hivi leo.
Barabara hiyo yenye urefu wa kilomita 31 inajengwa na
Kampuni ya Kimataifa ya Ujenzi na Uhandisi wa Majengo (CCECC) kutoka nchini
China.
Walieleza kuwa
mshikamano mkubwa umepatikana ndani ya Mkoa huo kutokana na uongozi wa Rais Dk.
Shein ikiwa pamoja na kuendelea kuwepo kwa amani, utulivu, umoja na mshikanao.
Wananchi hao wa Mkoa
wa Kaskazini Unguja walieleza kuridhika kwao kwa amani pamoja na mashirikiano
makubwa yaliopo katika Mkoa huo ambayo yamepelekea kuendelea kupata mafanikio
katika nyanja zote za maendeleo na za kijamii.
Aidha, Mkuu huyo wa
Mkoa wa Kaskazini Unguja kwa niaba ya Rais Dk. Shein aliwapongeza wananchi wa
Mkoa huo kwa kuitikia mwaliko wa Rais na kuungana nae pamoja katika futari hiyo
maalum aliyowaandalia.
Walimpongeza kwa
juhudi zake kubwa kwa kuviimarisha vijiji vikubwa vitatu vya Mkoa huo vikiwemo
Mgonjoni, Mbuyumaji na Mlilile ambapo kwa upande wa kijiji cha Mgonjoni tayari
huduma za maji, umeme, skuli na kituo cha
afya zimeshawafikia.
Akieleza kwa upande wa
kijiji cha Mgonjoni alisema kuwa tayari skuli pamoja na kituo cha afya
vimeshajengwa pamoja na huduma za maji na kinachosubiriwa hivi sasa ni bajeti ya mwaka
huu inayoanza mwezi wa Julai kwa ajili ya kumalizia barabara yao ambayo imebaki
asilimia 20 kumaliza. katika kijiji hicho.
Akielezea kuhusu
kijiji cha Mbuyumaji, Mkuu huyo wa Mkoa alieleza kuwa tayari huduma zote muhimu
za maendeleo alizoagiza kufikishiwa wananchi wa kijiji hicho zinaendelea
kupelekwa ambapo asilimia 95 ya ujenzi wa skuli ya kijiji hicho imefikiwa na
asilimi 90 ya matengezo ya hospitali nayo imefikiwa.
Kwa upande wa kijiji
cha Mlilile ambacho Dk. Shein alikitembelea wakati wa ziara yake katika Mkoa
huo, alieleza kuwa tayari yale yote
aliyoelekeza kufanywa katika kijiji chicho yametekelezwa ikiwemo ujenzi wa
skuli, kituo cha afya pamoja huduma za maji na umeme.
Aidha, walieleza kuwa
mradi wa Maji katika Mkoa huo unaendelea vizuri na tayari mradi huo wameshakabidhiwa
na wataalamu kutoka china na hatua iliyoendelea hivi sasa ni ya usambazaji na
kueleza kuwa si muda mrefu tatizo hilo litapatiwa ufumbuzi na wananchi waweze
kupata huduma hiyo.
Wakitoa neno la
shukurani wananchi hao wa Mkoa wa Kaskaznini walimpongeza, walimshukuru na
kumuombea dua Rais Dk. Shein kwa mema yote aliyowafanyia ikiwemo futari hiyo
adhimu aliyowaandalia.
Alhaj Dk. Shein atahitimisha
utaratibu na utamaduni wake aliojiwekea wa kufutari pamoja na wananchi wa Mikoa
yote ya Unguja na Pemba ambapo hapo kesho anatarajia kufutari pamoja na
wananchi wa Mkoa wa Mjini Magharibi pamoja na viongozi mbali mbali katika
viwanja vya Ikulu Mjini Zanzibar.
Rajab Mkasaba, Ikulu
Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax:
024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment