STATE
HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF
THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
Zanzibar 27.07.2018
RAIS wa Zanzibar
na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amesema kuwa uhusiano
na ushirikiano kati ya Malawi na Zanzibar una historia ya muda mrefu hivyo kuna
haja ya kuuendeleza ikiwa ni pamoja na kushirikiana katika sekta za maendeleo
ikiwemo sekta ya utalii.
Dk. Shein aliyasema
hayo leo, Ikulu mjini Zanzibar wakati alipofanya mazungumzo na Balozi wa Malawi katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,
Bi Hawa Olga Ndilowe aliyefika Ikulu kwa
ajili ya kuaga baada ya kumaliza muda wake wa kazi hapa nchini.
Katika mazungumzo
hayo, Dk. Shein alimueleza Balozi Hawa Ndilowe kuwa Zanzibar na Malawi zina mambo mengi ya kushirikiana kwa pamoja
ambayo yanaweza kuleta mafanikio makubwa kwa pande zote mbili yakiwemo
mashirikiano katika sekta ya utalii.
Dk. Shein alieleza
kuwa uhusiano na ushirikiano wa
kihistoria uliopo kati ya Zanzibar na Malawi ni njia moja wapo kubwa
itakayopelekea kuimarika zaidi kwa sekta ya utalii ambapo wananchi wa Malawi
watapata fursa ya kuitembelea Zanzibar na wananchi wa Zanzibar nao watawatembelea
ndugu zao wa Malawi.
Aidha, Dk. Shein
alimueleza Balozi Hawa kuwa Zanzibar na Malawi zote kwa pamoja zina mambo mengi
ya kujifunza kwa kila upande ikiwa ni pamoja na namna ya kuendeleza na
kuimarisha sekta ya utalii hasa ikizingatiwa kuwa Zanzibar imeanza kupata
mafanikio makubwa katika sekta hiyo.
Rais Dk. Shein alisisitiza
kuwa mashirikiano katika sekta ya utalii yatazidisha na kuimarisha uhusiano huo
wa kihistoria uliozishwa na waasisi wa nchi mbili hizo akiwemo Marehemu Mzee
Abeid Amani karume ambaye alitembelea Malawi mnamo mwaka 1958 na Marehemu Dk.
Kamuzu Banda alifika Zanzibar mnamo mwaka 1959.
Dk. Shein aliongeza
kuwa mbali ya mashirikiano katika sekta za maendeleo yaliokuwepo wakati huo
pia, viongozi hao waliweza kujenga urafiki kupitia vyama vyao vya siasa
kikiwemo chama cha ASP kwa upande wa Zanzibar na Chama cha MCP cha Malawi.
Aliongeza kuwa, kwa
upande wa sekta ya biashara pande hizo mbili zinaweza kuimarisha na kuendeleza
sekta hiyo ambayo itaimarisha uchumi na kukuza uhusiano wa watu wake.
Akieleza kuhusu
mashirikiano katika sekta ya elimu, Rais Dk. Shein alieleza kuwa ipo haja kwa
kuendeleza mashirikiano kati ya vyuo vikuu vya nchi hiyo na vile vya Zanzibar
kikiwemo Chuo Kikuu cha Taifa cha Zanzibar (SUZA) sambamba na kushirikiana
katika sekta ya michezo na utamaduni hasa ikizingatiwa kuwa michezo hukuza
urafiki na maelewano.
Pamoja na hayo, Rais
Dk. Shein alieleza haja ya kuendeleza mashirikiano katika kuwajengea uwezo
wafanyakazi kwa pande zote mbili.
Dk. Shein alieleza
kuwa mbali ya mashirikiano ya sekta hizo mbili muhimu, nchi hizo zinaweza kuimarisha
ushirikiano katika sekta ya elimu, afya pamoja na kubadilishana utaalamu kwa
vyuo vikuu hatua itakayopanua wigo wa kitaalamu na kimaendeleo kwa manufaa ya
pande mbili hizo.
Nae Balozi wa Malawi katika
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Bi Hawa Olga Ndilowe alimueleza Dk. Shein kuwa Malawi
itaendelea na dhamira yake ya kuimarisha zaidi uhusiano wa kidugu uliopo kati
yake na Tanzania ikiwemo Zanzibar ambao umejengwa kwa muda mrefu.
Balozi Hawa alitumia
fursa hiyo kumpongeza Rais Dk. Shein kwa mashirikiano makubwa aliyoyapata hapa
Zanzibar katika kipindi chake chote alichofanya kazi akiiwakilisha Malawi hapa
Tanzania huku akisisitiza kuwa nchi hiyo itaendeleza ushirikiano wake na kukuza
uhusiano wa kihistoria na kidugu uliopo.
Katika maelezo yake
Balozi Hawa alimueleza Dk. Shein, haja ya kuendeleza ushirikiano katika sekta
ya utalii kati ya pande mbili hizo hasa ikizingatiwa sekta hiyo ina umhimu
mkubwa katika kukuza uchumi.
Alieleza kuwa kwa
upande wake ameona kuna faida nyingi zinaweza kupatikana katika sekta ya
biashara iwapo mashirikiano yataimarishwa zaidi ambapo tayari hivi sasa
mafanikio yameanza kupatikana kati ya Malawi na Tanzania kutokana na makubalizo
ambayo yameanza kufanyiwa kazi kwa sekta hiyo na sekta nyengienzo.
Aidha, Balozi Hawa
alieleza kuwa mashirikiano katika sekta ya biashara kati ya nchi yake na Tanzania yanaedelea
vizuri na kueleza haja ya kuimarishwa kwa manufaa ya pande mbili hizo.
Aliongeza Malawi na
Zanzibar zinaweza kushirikiana katika sekta kadhaa za maendeleo ikiwemo elimu,
biashara, afya, kuwajengea uwezo wafanyakazi, utalii, michezo na utamaduni
pamoja na sekta nyenginezo.
Balozi Hawa aliongeza kuwa
Malawi imekuwa na mashirikiano na Tanzania katika sekta mbali mbali za
maendeleo ikiwemo sekta ya elimu ambapo baadhi ya vyuo vikuu vya Tanzania kiikiwemo
Chuo Kikuu cha Sokoine, Chuo Kikuu cha Dar-es-Salaam na vyo vikuu vyenginevyo
vimenza kushirikiana.
Rajab
Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax:
024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment