Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk Ali Mohamed Shein, akihutubia wakati akifungua Mkutano wa Jukwaa la Tisa la Biashara Zanzibar katika ukumbi wa Sheikh Idrisa Abdulwakil Kikwajuni Zanzibar.
Rais wa
Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein, amewataka
wadau wa sekta binafsi nchini, kuweka mkazo katika utoaji wa huduma bora ili
ziweze kukidhi viwango na ubora, kulingana na malengo na matarajio ya wananchi.
Dk. Shein
amesema hayo leo katika ukumbi wa Sheikh Idrissa Abdulwakil Kikwajuni Mjini
hapa, alipofungua Jukwaa la Biashara la tisa
(9) Zanzibar.
Jukwaa hilo ambalo
limewashirikisha viongozi wa serikali na wadau mbali mbali wa sekta binafsi, limeambatana na kauli mbiu isemayo
“mashirikiano baina ya sekta ya umma na Sekta binafsi katika kukuza Ajira kwa
Vijana”
Akizungumza
katika jukwaa hilo, Dk. Shein alisema kumekuwepo na malalamiko kutoka miongoni
mwa wananchi kuwa baadhi ya sekta binafsi zimekuwa zikiendesha shughuli za
utoaji wa huduma, zisizokidhi mahitaji halisi pamoja na malengo ya taifa ya
muda mfupi na mrefu.
Alisema kwa
kiwango kikubwa malalamiko hayo yamekuwa
yakielekezwa katika sekta za Afya na elimu, hivyo ametaka juhudi
zifanyike kwa kuweka mkazo katika uimarishaji wa huduma bora.
Aidha, aliwataka
wadau wa sekta hizo kuliangalia kwa kina suala la kuwajengea uwezo wafanyakazi wao,
akibainisha kutokuwepo msukumo wa kutosha katika kuwasomesha wataalamu wa sekta
hizo na badala yake kutegemea zaidi wataalamu waliosomeshwa na serikali.
“Hatua ya
sekta binafsi kuajiri wataalamu walio na majukumu muhimu serikalini, kunaathiri
utoaji wa huduma katika maeneo wanayoyatumikia, lazima muwe tayari kugharamika
kwa ajili ya kuwajengea uwezo wafanyakazi wenu”, alisema.
Alisema sio
jambo jema kwa maendeleo ya taifa kwa kuwa na wataalamu wengi wasiopenda
kufanyakazi katika sekta binafsi, kwa sababu ya ugumu wa kujiendel;eza.
“Natowa wito
kwa waajiri katika sekta binafsi kuwa na mipango imara ya kuwaendeleza
wafanyakazi wenu’, alisisitiza.
Dk. Shein akazipongeza sekta binafsi kwa
kushirikiana na Serikali katika kuimarisha maslahi ya wafanyakazi, hususan kwa
hatua yao ya kuitikia wito wa Serikali wa kupandisha mishahara ya kima cha
chini kuambatana na miongozo iliyotolewa.
Aidha, aliwataka
waajiri wa sekta binafsi kuhakikisha wanafikisha michango ya wafanyakazi wao
katika mfuko wa Hifadhhi ya jamii (ZSSF), ili kuwajengea wafanyakazi mustakbali
mwema wa maisha yao na utulivu kazini.
Alieleza
kuwa sekta binafsi ina mchango mkubwa katika kufanikisha azma ya serikali ya kuwa na uchumi wa kati kwa
kutumia fursa kadhaa ambazo bado hazijafikiwa.
Alizitaja
baadhi ya fursa hizo kuwa ni pamoja na ile ya uvuvi wa bahari kuu, uendelezaji
wa shughulli za kilimo na ufugaji kwa njia za kisasa pamoja uwekezaji katika
sekta za nishati na viwanda.
“Tuwe na
ujasiri wa kuwekeza katika sekta mpya ili kuepuka ushindani usio na lazima,
bado hatujaanzisha miradi mipya kwa njia ya ubia kama wafanyavyo wenzetu katika
nchi mbalimbali duniani’, alisema.
Alisema kuimarika
kwa sekta binafsi kutapanua wigo wa soko la ajira na kuwapatia vijana kazi za
staha kupitia sekta mbali mbali na hivyo kupata uwezo wa kuendesha maisha yao.
Aidha,
alipongeza juhudi zinazoendelea kuchukuliwa za kuimarisha ushirikiano kati Serikali
na sekta binafsi, kwa amslahi ya Taifa na wnanachi wake.
“Ushahidi mzuri
wa jambo hili ni ufanisi wa kupigiwa mfano ulioonekana katika maonyesho ya
Utalii Zanzibar yaliofanyika hivi karibuni, tumeweza kuitangaza nchi kwa
mafanikio makubwa’, alisema.
Kuhusiana na
uimarishaji wa Mazingira ya Biashara, Dk. Shein alisema Serikali imeanzisha sheria
namba 10 ya mwaka 2017 kwa lengo la kuhakikisha kunakuwepo utaratibu bora na
madhubuti katika uendeshaji wa biashara nchini.
Alisema
Wafanyabiashara na wawekezaji hupenda kuwekeza katika nchi ambazo zimeweka
mazingira mazuri ya kufanyia biashara, hivyo akaomba kuitumia mikutano na
majukwaa kujadili namna bora ya kuimarisha na kurahisisha maendeleo katika
sekta ya biashara.
“Utoaji wa
huduma unaotegemea vitendo vya rushwa na uenyeji huzorotesha kasi ya biashara
na uwekezaji, endelezeni shughuli zenu kwa kuzingatia mabadiliko ya teknolojia
na mahitaji halisi ya wananchi’, alisema.
Mapema, Waziri
wa Biashara na Viwanda, Balozi Amina Salum Ali alisema uanzishaji wa mabaraza
ya Vijana utaongeza kasi ya kuzitafutia ufumbuzi changamoto mbali mbali
zinazowakabili vijana, hususan ya ukosefu wa ajira.
Alisema
jukwaa hilo litajadili na kupata majibu ya mazingira bora yanayopaswa kuwepo ili kuleta maendeleo ya kibiashara sambamba
na kukuza uchumi wa taifa.
Aidha, alisema
ukosefu wa bajeti na chombo cha kuuunganisha sekta hizo mbili ni miongoni mwa
changamoto zinazokwaza kupatikana kwa ufanisi.
Nae,
Mwenyekiti wa jumuiya ya wafanyabiashara, wenye viwanda na wakulima, Taufiq
Salim Turky akitoa salamu kutoka jumuiya hiyo kwa niaba ya sekta binafsi,
alisema chini ya Uongozi wa Dk. Shein sekta ya utalii imepata mafanikio makubwa
hususan katika suala la ujio wa watalii nchini.
Alisema
katika kipindi cha miaka minane ya Uongozi wake, ujio wa watalii umeongezeka
kutoka ule wa watalii 150,000 uliodumu kwa takriban miaka 20 na kufIkia zaidi
ya watalii 350,000 hivi sasa, huku kukiwa na matumaini makubwa ya kuongezeka kiwango
hicho hadi kufikia 500,000 ifikapo mwaka 2020.
Alisema Rais
Dk. Shein amerejesha uelewa uliokosekana kwa kipindi kirefu, kuwa Serikali na
sekta binafsi zina malengo ya aina moja.
Katika jukwa
hilo, mada mbali mbali mbali ziliwasilishwa na kujadiliwa.
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax:
024 2231822
E-mail: abdya062@gmail.com
NA ABDI SHAMNAH, IKULU
No comments:
Post a Comment