Habari za Punde

Uzinduzi wa Jengo Jipya La Mkemia Mkuu wa Serikali na Maabara ya Vinasaba vya DNA Maruhubi Zanzibar.


Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dk. Ali Mohamed Shein, akiondoa kipazia kuashiria kuweka Jiwe la Msingi la Jengo Jipya la Wakala wa Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali na Maabara ya Vinasaba vya DNA, Maruhubi Zanzibar, ikiwa ni shamrashamra za kuadhimisha miaka 55 ya Mapinduzi ya Zanzibar. 

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein ameutaka uongozi wa Wakala wa Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali na Maabara ya Uchunguzi wa Vinasaba (DNA) kujidhatiti katika ubunifu ili ziweze kutoa huduma bora na za kisasa zaidi, zitakazokwenda na wakati uliopo,  

Dk. Shein aliyasema hayo katika hafla ya uzinduzi wa jengo la Wakala wa Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali na Maabara ya Uchunguzi wa Vinasaba (DNA), lililopo Maruhubi, Mkoa wa Mjini Magharibi ikiwa ni miongoni mwa shamrashamra za miaka 55 ya Mapinduzi ya Januari 12, 1964.

Alisisitiza kuwa uongozi wa Wakala wa Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali na Maabara ya Uchunguzi wa Vinasaba (DNA), ni lazima uweze kujikita katika suala zima la ubunifu kwa lengo la kwenda mbele zaidi na kupata mafanikio katika kutoa huduma za afya zikiwemo zile za uchunguzi.

Alieleza kuwa ubunifu ni jambo muhimu na kubainisha kuwa pale unapopewa cheo ni pazima uwe mbunifu, badala ya  kubaki  ukitegemea mambo yaliobuniwa na wengine, ikiwa ni pamoja na njia  na mikakati sahihi.

Alieleza haja ya Bodi ya Wakala na Maabara hiyo kutoa msaada katika kuisaidia Maabara hiyo kubuni mipango mbali mbali na kueleza kuwa kila siku kumekuwa kukibuniwa mambo mapya duniani, hivyo ni vyema na wao wajiweke tayari katika mabadiliko hayo, kwa vile tayari wamekuwa wakifanya kazi na wataalamu wengine wa Afrika Mashariki na sehemu nyengine duniani.

Rais Dk. Shein alisema kuwa DNA ina mambo mengi inayoyafanya na sio kama inavyokuzwa hivi sasa na baadhi ya watu, akibainisha   kazi  zinazofanywa Maabara hiyo husika ni za kitaalamu ambazo zenye taratibu zake.

Alieleza kuwa Zanzibar ina vifaa na mashine nyingi muhimu za utoaji huduma za afya kupitia Wizara ya Afya ikiwa pamoja na mashine ya uchunguzi ya MRI ambayo ni muhimu katika huduma za afya.

Dk. Shein alisema kuwa Mapinduzi ni mabadiliko ikiwa ni pamoja na kupanga mipango ya maendeleo kwa nchi na wananchi wake  na ndio maana ASP ilipaswa kufanya Mapinduzi kutokana na dhulma kubwa iliyokuwepo kwa muda mrefu ambapo haki haikuwa  ikitendeka kwa Wazanzibari.


Aliongeza kuwa wakati wa ukoloni palikuwa na ubaguzi mkubwa wa kutoa huduma za afya ambapo watu waligawiwa kwa makundi  katika kutoa huduma  hizo kulingana na uwezo na nasaba zao.

Alisema kuwa kabla ya Mapinduzi matibabu yalikuwa kwa ubaguzi na ndio maana mara tu baada ya Mapinduzi mnamo  Machi 3, 1965 Marehemu Mzee Karume alitangaza matibabu bure ambapo hata hivyo kabla ya Mapinduzi Maabara hiyo kazi zake zilifanywa kwa ubaguzi.

Pamoja na hayo, alisema kuwa Maabara hiyo imepita katika mikondo migumu na ndio sababu Serikali ikaipa kipaumbele tokea Awamu zilizopita na viongozi wengine waliofuata huku akisisitiza kuwa na yeye kwa upande wake aliweza kutoa  mchango wake wa kuimarishwa taasisi hiyo.

Aidha, Rais Dk. Shein alieleza kuwa Maabara ya Viwango, Maabara ya Vyakula na Vipodozi pamoja na Maabara  ya Mkemia Mkuu na Maabara ya Uchunguzi wa Vinasaba (DNA) ni muhimu sana ambapo kila moja ina kazi zake na Sheria na taratibu zake hivyo kazi zao haziingiliani.

Akieleza juuu ya kazi za Maabara ya Uchunguzi wa Vinasaba (DNA), Rais Dk. Shein alisema kuwa katika uchunguzi unaofanywa katika Maabara hiyo hatimae kesi zinazoletwa zinakwenda Mahakamani, hivyo taasisi hizo ni lazima ziwe na watu wenye taaluma kubwa  na kuwataka kuwa makini katika utendaji wao wa kazi.

Alieleza kuwa wale wanaoshutumiwa ndio watakaokuja katika Maabara hizo wakiwemo wale waliofanya matokeo mbali mbali maovu wakiwemo waliobaka, hivyo umakini lazima uwepo ili kuweza kupata ukweli juu ya uchunguzi utakaofanywa.

Alisema kuwa Wizara ya Afya imefanya mambo makubwa katika Awamu ya Saba, chini ya uongozi wake ikiwa ni pamoja na kuwepo kwa huduma ya Benki ya Damu ambayo hapo nyuma haikuwepo.

Rais Dk. Shein alisema kuwa wakati anaingia madarakani, Novemba 3 mwaka 2010 Serikali ilikuwa inakusanya TZ Shilingi Bilioni 13.5 kwa mwezi lakini hivi sasa fedha zinazokusanywa na Serikali ni TZ Shilingi Bilioni 65 kwa mwezi.

Alisema kuwa licha ya Zanzibar kuwa nchi masikini lakini imeweza kufanya mambo mengi makubwa ambayo kuna nchi nyengine haziwezi kufanya kama ilivyofanya Zanzibar.

Dk. Shein alizitaka Maabara zote tano za hapa Zanzibar waanzishe Jumuiya yao ya Maabara kama ilivyo kwa nchi nyengine hasa ikizingatiwa kuwa Zanzibar ina wataalamu watu wengi.

Alisema kuwa iwapo watafanya hivyo itasaidia hasa katika kufanya kazi zao huku akiwataka  kuunda Jumuiya zao za Kitaalamu ili awe na nguvu za Kitaalamu na kuweza kushiriki mambo kadhaa duniani kwani tayari Zanzibar imekuwa ikijulikana.

Alisema kuwa Zanzibar inajiuza kwa jina lake, na kuwataka kuitumia nafasi hiyo kuendelea kuijenga nchi, Mapinduzi na Muungano kwani Mapinduzi yameleta Muungano ambao umeleta nguvu kwa wananchi wake.

Alisisitiza kuwa ni lazima wafanyakazi wajikite kwenye uzalendo kama walivyokuwa wakifanya kazi wao katika Wizara hiyo na kusisitiza kuwa lengo ni kwenda kwenye taaluma za kisasa zaidi ili kuweza kutoa huduma za kitaalamu zinazokwenda na wakati uliopo.

Aidha, alieleza kuwa fani hiyo ya uchunguzi wa mambo ya jamii hukumu yake haiishii hapa duniani bali yanaishia kwa Mwenyezi Mungu hivyo, aliwataka wafanyakazi wa Maabara hiyo kufanya kazi kwa umakini, kuwa waadilifu na wakweli pale wanapotoa matokea.

Aliongeza kuwa kazi hiyo ni kazi ambayo matokeo yake hayaishii hapa ni kazi ambayo ina lawama hivyo aliwataka kufanya kazi vizuri ili matokeo yawe mazuri na kwani wananchi wote wa Zanzibar wanaitegemea sana Maabara hiyo iwasaidie katika uchunguzi wa DNA.

Nae Kaimu Waziri wa Afya Rashid Ali Juma, alisema kuwa jengo hilo linakidhi nafasi ya vyumba vya maabara pamoja na nafasi na kueleza kufarajika kwa kupata jengo hilo ambalo litandoa changamoto ya nafasi na kuwafanya watendaji kufanya kazi kwa ufanisi.

Watafanya kazi ya kutoka huduma ya uchukungu zi kitaifa na kimafaita, ni shemu ambayo imeanza 1908 ambapo hivi sasa itatizomiza 111.

Maabara kwa kipndi kirefu ilifanya kazi zake katika chumba kimoja katika Wizara ya Afya, na baadae kuhamishwa na kupatiwa nafasi ya muda katika jengo la Living stone pamoja na kuwa na watumishi wachache na hivi sasa idadi ya watumishi imeongezeka .

Mnamo mwaka 1964 ilihamishiwa Wizara ya Afya ambyo ipo hadi hivi sasa ambapo ilipandishwa hadhi ya kuwa Idara kamili pamoja na kupatiwa jengo huko Mwanakweekwe ambapo miongoni mwa kazi zake ni uchunguzi wa vyakula, dawa za kuevya, sumu na pombe.

Alieleza kuwa hatua hiyo ni mafanikio makubwa ambayo yamepatikana katika uongozi wake  ikiwa ni pamoja na kupitishwa Sheria namba 10 ya mwaka  2011 na kutoka Idara hadi kuwa Wakala ambayo ndiyo matuda mema katika sekta ya afya.

Waziri Rashid alisisistiza kuwa hiyo ni Taasisi muhimu katika nyanja za kiuchimi na kijamiii, ambayo ina kazi ya kufanya uchunguzi na kutoa matokea kwa jamiii na hiyo ni sehemu ya utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM hasa katika kuimarisha uchunguzi kwa wananchi.

Katika maelezo yake, Waziri huyo alimuomba Rais Dk. Shein kuendelea na utamaduni wake wa  kuzilea taaasisi hizo ili Maabara hiyo iendelee na kazi zake za uchunguzi na kusisitiza imani yake katika kuhakikisha huduma muhimu zinatolewa.

Kaimu Waziri huyo wa Afya alitumia fursa hiyo kuwapongeza wafanyakazi kwa taaluma zao walizonazo pamoja na kuupongeza uogozi wa Idara hiyo sambamba na kupongeza mashirikiano makubwa yaliopo kati ya watendaji wa Wakala huyo.

Mapema , Katibu Mkuu Wizara ya Afya Asha Ali Abdalla alisema  kuwa kuwepo kwa mashine za uchunguzi wa vinasaba kutapelekea pamoja na mambo mengine kupatikana kwa ushahidi wa kitaalamu utakaowezesha kutatuwa utata wa kesi nyingi hasa zinazohusu udhalilishaji wa kijinsia pamoja na kihalifu.

Alisema kuwa hatua hiyo itasaidia kufanya tafiti za magonjwa mbali mbali na pia, kuwezesha kutambuwa miili ya wahanga pale inapotokea ajali na wahanga kushindikana kutambuliwa kwa sura.

Katibu Mkuu huyo alisema kuwa mpaka hatua zilizofikiwa za ujenzi wa jengo hilo mradi huo wa Kuimarisha Maabara ya Wakala wa Mkemia Mkuu wa Serikali umegharimu jumla ya TZ Shilingi Bilioni 2.8.

Alisema kuwa jengo hilo limejenga na Mkandarasi mzalendo kutoka Zanzibar anaeitwa (Millenium Engineering Company) ambae amejitahidi kulijenga kwa kiwango kilichohitajika na amefanya kazi hiyo chini ya usimamizi wa Wataalamu Wahandisi na Wasarifu wa Majengo wa Wizara ya Afya.

Sambamba na hayo, Katibu Asha alitoa shukurani kwa Rais Dk. Shein kwa jitihada kubwa aliyoionesha katika kufanikisha kuwepo kwa jengo hilo la Maabara ya Wakala wa Mkemia Mkuu wa Serikali “Tusingelifika hapa kama si nia yako safi na ya dhati pamoja na azma ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuimarisha huduma za maabara za uchunguzi ili kuleta maendeleo chanya kwa wananchi na Zanzibar kwa jumla”,alisema Katibu Asha.

Mapema Dk. Shein alitembelea jengo hilo na kupata maelezo juu ya shughuli zinazofanywa katika Maabara hiyo ya uchunguzi ya DNA pamoja na kupata maelezo juu ya utendaji kazi wa vifaa vilivyomo ambavyo ni vya kisasa.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.