Habari za Punde

Walimu wa Vituo Vya Elimu Mbadala Zanzibar Watakiwa Watakiwa Kuwa Wabunifu.




Na. Suleiman Juma
MKURUGENZI wa Idara ya Elimu Mbadala na Watu Wazima Zanzibar, Bi Mashavu Ahmad Fakih amesema Walimu wa Vituo vya Elimu Mbadala wanahitaji kujengewa uwezo ili waweze kuwa wabunifu katika shughuli mbalimbali ikiwa ni pamoja na uandaaji wa zana kulingana na mazingira ambapo wataweza kufanikisha dhana nzima ya ufundishaji na ujifunzaji.

Alieleza hayo wakati wa ufunguzi wa mafunzo maalumu kwa walimu wa Kituo cha Elimu Mbadala Mtemani Wingwi Pemba.

Alisema, mafunzo watakayopatiwa yatawajengea uwezo walimu hao kuandaa zana za kufundishia na kujifunzia na kuweza kwenda sambamba na mtaala husika, pamoja na kuongeza ubunifu wa vitu vipya katika kukidhi mahitaji.

“Mafunzo haya yataweza kubuni mbinu na kuandaa zana husika katika suala zima la ufundishaji, lakini vilevile itakuwezesheni kufundisha kwa mujibu wa mtaala tulionao” alieleza.

Sambamba na hilo alisema kuwa, walimu ni viongozi hivyo wanapaswa kujua mbinu mpya za uongozi, utawala, na uendeshaji na kuongeza uwezo katika masuala ya uratibu na usimamizi.

Alisema, mafunzo ya walimu hujikita katika masuala ya muhimu ambayo ni utendaji kazi na matatizo kazini kwani walimu hukutana na matatizo mengi yanayokwamisha wepesi  na ufanisi wa mwalimu kiutendaji hasa katika ufundishaji.

“Mafunzo yatawezesha kukabiliana na mahitaji na mabadiliko yote katika mazingira ya ufundishaji yatakayojitokeza, kwaiyo yatakupeni upeo mzima wa kuona tumefikwa na changamoto hii tuweze kuitatua kwa kiasi gani” aliongeza.

Mapema akimkaribisha mgeni rasmi, Mkuu wa Divisheni Elimu Mbadala na Watu Wazima Bi Halima Tawakal Hairallah aliwataka walimu hao kuyafanyia kazi mafunzo hayo ili waweze kufundisha kwa wepesi na ufanisi.

Wakitoa michango yao baadhi ya walimu wa kituo hicho walimshukuru Mkurugenzi huyo kwa kuwaandalia mafunzo hayo na kuahidi kuyafanyia kazi.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.