Habari za Punde

Kutoka Bungeni Jijini Dodoma Serikali Kufanyia Kazi Mbagala Kuwa Mkoa wa Kikodi

Naibu Waziri wa Fedha na Mipango, Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji (Mb)
Na. Saidina Msangi na Josephine Majura, WFM, Dodoma
Serikali imesema kuwa inafanyia kazi ombi la Mbunge Mbagala la kuifanya Mbagala kuwa Mkoa wa kikodi ili kurahisisha ulipaji wa kodi ikiwemo ya Majengo.
Hayo yameelezwa bungeni Jijini Dodoma na Naibu Waziri wa Fedha na Mipango, Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji (Mb) alipokuwa akijibu swali la nyongeza la Mbunge huyo , Mhe. Issa Ali Mangungu, aliyetaka kujua ni lini Serikali itaifanya Mbagala kuwa Mkoa wa Kikodi ili kuwalahisishia wananchi kulipa kodi.
Dkt. Kijaji alisema kuwa, suala la Mbagala kuwa Mkoa wa Kikodi linafanyiwa kazi ili kuhakikisha shughuli za ukusanyaji wa kodi zinafanywa kwa ufanisi na kwa urahisi.
Alisema kuwa Mamlaka ya Mapato Tanzania- TRA ilikusanya takribani Sh. Bilioni 3.7 katika mkoa wa kikodi wa Temeke katika mwaka wa fedha 2017/2018, ikiwa ni matokeo ya  marekebisho ya sheria ya fedha ya Mamlaka ya Serikali za Mitaa kufanyika kupitia sheria ya fedha ya mwaka 2016.
“Mkoa wa kikodi temeke umekusanya kodi kwa asilimia 60 ya lengo la kukusanya takribani Sh. Bilioni 6.1,”alieleza Dkt. Kijaji.
Kwa upande mwingine Dkt. Kijaji, amezitaka Benki zote nchini kuwahudumia walemavu wanapofika kupata huduma za fedha na pia kurekebisha miundombinu ya kuingia ATM ili kukidhi mahitaji ya walemavu.
Akijibu swali la Msingi la Mbunge wa Viti maalum Mhe. Amina Saleh Mollel, kuhusu mpango wa Serikali katika kuhakikisha ATM zinakidhi mahitaji ya walemavu, Dkt. Kijaji alisema kuwa inaangalia namna ambayo itawezesha   mifumo ya miamala kwa njia ya ATM inakuwa Rafiki kwa makundi yote wakiwemo watu wenye ulemavu.
“Serikali inaendelea kufuatilia kwa karibu ili kuhakikisha ATM za mabenki zinawekewa mifumo inayokidhi mahitaji ya watu wenye ulemavu”, alisema Dkt. Kijaji.
Dkt. Kijaji alisema kuwa Mei 2017 Benki Kuu ya Tanzania ilitoa mwongozo wa mfumo wa malipo kwa njia ya mtandao ikiwa ni mpango wa Serikali wa kuhakikisha kuwa huduma za malipo kwa njia ya mtandao zinafanyika kwa usalama na kukidhi mahitaji ya makundi yote katika jamii.
Aidha pamoja na Serikali kutoa mwongozo huo Benki nchini hazijafanikiwa kusimika ATM maalum na rafiki kwa watu wenye ulemavu hususan watu wenye ulemavu wa macho hivyo Benki zinatakiwa kutatua changamoto hiyo.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.