Mawaziri wa Kazi na Ajira kutoka Nchi za SADC wakinawa
maji ya kisima cha Baraka kisichokauka wala kuongezeka maji yake yaliyo mita
mbili kilichoko katika makumbusho ya KAOLE Bagamoyo walipotembelea baada ya
kumaliza Mkutano wa Mwaziri wa Kazi na Ajira na Wadau wa utatu wa Nchi za SADC
ulifanyika Machi 5, 2020 JNICC Jijini Dar es Salaam, Tanzania.
Na: Mwandishi Wetu
Mawaziri na
Wadau wa Utatu wa Nchi Wananchama wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika
(SADC) sekta ya kazi na ajira waipongeza Serikali ya Tanzania kwa mikakati
iliyojiwekea katika kuwajengea uwezo vijana kupitia Programu ya Taifa ya Kukuza
Ujuzi.
Pongezi
hizo zimetolewa na Mawaziri na Wadau wa utatu wa Jumuiya hiyo ikiwemo
Jukwaa la Vyama vya Waajiri Kusini mwa Afrika (SPSF), Shirikisho la Vyama vya
Wafanyakazi Kusini mwa Afrika (SATUCC), Shirika la Kazi Duniani (ILO) na
Shirika la Kimataifa linaloshughulikia masuala ya Uhamiaji kanda ya Kusini mwa
Afrika (IOM).
Akizungumza
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia Sera, Bunge, Kazi,
Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu Mhe. Jenista Mhagama (Mb) na waandishi wa habari
wakati wa ziara yake aliyoambatana na Mawaziri na Wadau wa Utatu wa SADC sekta
ya Kazi na Ajira walipotembelea Chuo cha Don Bosco Network kilichopo Oysterbay
Jijini Dar es Salaam na Maeneo ya Vivutio vya Utalii Bagamoyo alieleza kuwa
Serikali iliamua kuanzisha programu hiyo lengo ikiwa ni kutatua changamoto ya
ukosefu wa ajira kwa vijana kwa kuwajengea mazingira wezeshi na
yanayowahamasisha kuajiriwa au kujiajiri.
“Mawaziri
na Wadu wa Utatu wa SADC sekta ya Kazi na Ajira wamefurahia kuona namna
Serikali inavyotekeleza Programu ya Taifa ya Kukuza Ujuza kwa Vijana ambayo kwa
kiasi kikubwa itawawezesha vijana kupata uwezo na ujuzi unaohitajika katika
soko la ajira kwa nchi hizo wanachama,” alisema Waziri Mhagama.
“Zipo nchi
wananachama wameomba kukutana na Ofisi ya Waziri Mkuu ambayo inatekeleza
programu hiyo kwa lengo la kuweza kupata uelewa wa taratibu na namna ya
kutekeleza programu hiyo, nchi ya Eswatini tayari imeonyesha nia ya kukutana na
ofisi yangu ili nao waweze kuanzisha programu hiyo nchini kwao,” alieleza
Mhagama
Alieleza
kuwa wakati wa uzinduzi rasmi wa Mkutano huo wa Mawaziri na Wadau wa Utatu wa
SADC sekta ya Kazi na Ajira uliozinduliwa Machi 5, 2020 na Makamu wa Rais wa
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan, Serikali iliona
umuhimu wa kuzindua Programu mmoja wapo ambayo ni Programu ya Mafunzo ya
Vitendo Mahala pa Kazi (Internship) ili kuelezea nchi wanachama mikakati ambayo
Serikali imejiwekea katika kutatua changamoto ya ajira inayowakabili vijana kwa
kuwawezesha vijana kuwa na uzoefu katika utendaji kazi.
Aidha
aliongeza kuwa katika mkutano huo uliowakutanisha waliweza kujadili masuala
mbalimbali yanayohusu sekta ya Kazi na Ajira ambazo ni masuala ya Hifadhi ya
Jamii, Uhamishaji wa nguvu kazi, mapitio ya sera na miongozo iliyotungwa na
nchi wanachama kuhusu masuala ya kazi na ajira, haki na wajibu wa wafanyakazi,
mapitio ya mikataba ya kimataifa na mikataba ya Shirika la Kazi Duniani (ILO)
inayoongoza masuala ya ajira pamoja na kuwajengea uwezo vijana.
Kwa upande
wake Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Vijana na Ajira) Mhe. Anthony
Mavunde wakati akielezea kuhusu programu ya ukuzaji ujuzi kwa Mawaziri na Wadau
wa Utatu wa SADC sekta ya Kazi na Ajira alieleza kuwa Programu hiyo ya Taifa ya
Kukuza Ujuzi inafadhiliwa na Serikali kwa lengo la kuwawezesha vijana ambao kwa
asilimia kubwa ndio nguvukazi ya taifa wanapata ujuzi na uzoefu ambao
utawafanya waweze kujitegemea.
“Hii ni
habari njema kwa sisi Watanzania kutembelewa na Mawaziri na Wadau wa Utatu
ambao wamekuja kujionea namna serikali yetu inavyowajali vijana na jinsi
inavyowatumikia katika kuwawezesha kupata ujuzi ambao utawasaidia pindi vijana
hao wanapomaliza mafunzo waweze kujiajiri ama kuajiriwa,” alisema Mavunde
Alifafanua
kuwa Ofisi ya Waziri Mkuu inaratibu
Programu ya Ukuzaji Ujuzi ikiwemo Mafunzo kwa Njia ya Uanagenzi, Mafunzo ya
Urasimishaji Ujuzi uliopatikana Nje ya Mfumo Rasmi, Mafunzo ya Vitendo Mahala
pa Kazi kwa Wahitimu na Mafunzo ya Ukuzaji Ujuzi kwa walio Makazini na Mpango
huo wa Urasimishaji Ujuzi Uliopatikana Nje ya Mfumo Rasmi (Recognition of Prior
Learning).
Katika
ziara hiyo Mawaziri na Wadau wa Utatu wa SADC sekta ya Kazi na Ajira walipata
fursa ya kutembelea maeneo ya kihistoria yaliyopo Bagamoyo ikwemo Ngome Kongwe,
Soko la zamani la Watumwa, Bandari iliyokuwa inatumika kuwasafirisha watumwa,
eneo la Msalabani ambapo Ukristo ulianzia kuenezwa hapo na wakoloni, Magofu ya
Kaole lengo la ziara hiyo ilikuwa kutangaza maeneo ya vivutio vya kihistoria
vilivyopo hapa nchini.
Waziri wa
Kazi na Ajira Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo Mhe. Ilunga Nkulu Nene alieleza
kuwa wamevutiwa sana na maeneo ya kihistoria yaliyopo Tanzania kama vile mji wa
kihistoria wa Bagamoyo Pwani, ambayo unaifanya Tanzania iwe nchi ya kuigwa kwa
historia ya Nchi za Kusini mwa Afrika.
“Nchi ya
Kongo ina maeneo mengi ya kitalii lakini hatuyatangazi kama Tanzania
inavyofanya, kama kiongozi nimejifunza jambo katika ziara ya leo na hivyo
nitakaporudi Kongo nitahamasisha utangazaji wa maeneo ya kihistoria yaliyopo
kwa lengo la kuvutia watalii,” alisema Nene
No comments:
Post a Comment