Kaimu Mkuu wa Kitengo cha Mazingira cha Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), Maxmilian Mahangila (mwenye koti jeupe kushoto), mwishoni mwa wiki akiwasilisha kwa Bodi ya Ushauri (MAB) ya TAA, ripoti ya madhara ya ugonjwa wa homa kali ya mapafu (COVID19) unaoambukizwa na virusi vya corona kwa upande wa uendeshaji wa viwanja vya ndege.
Na. Bahati Mollel,TAA
BODI
ya Ushauri (MAB) ya Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), imeiangukia
serikali iisaidie TAA kuigharama huduma mbalimbali za uendeshaji kwenye viwanja
vya ndege kutokana na kuathiriwa kwa asilimia 100 na ugonjwa wa homa kali ya
mapafu (COVID19), inayoambukizwa na virusi vya corona.
Mwenyekiti
wa MAB, Dkt. Masatu Chiguma, ametoa kauli hiyo mwishoni mwa wiki kwenye kikao
cha dharura cha Bodi hiyo, kilichofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Jengo la
Watu Mashuhuri lililopo katika Jengo la Pili la Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa
cha Julius Nyerere (VIP-TB2-JNIA.
Dkt.
Chiguma amesema ugonjwa huu ambao upo nchini ulianzia nchini China mwishoni mwa
mwaka 2019 na tarehe 11 Machi, 2020 Shirika la Afya Duniani (WHO), kuutangaza
rasmi kuwa ni janga lililoikumba dunia nzima, baada ya kusambaa kwenye nchi
kadhaa na wananchi wake kupata maambukizi na wengine kupoteza maisha. Tanzania
hadi sasa ina maambukizi 147 na waliofariki ni watano.
“Imetulazimu
kuitisha kikao hiki cha dharura haraka ili kupata tathmini ya madhara
yaliyoikumba TAA kutokana na huu ugonjwa wa COVID19 baada ya kusimamishwa kwa
ndege za abiria za nje ya nchi kuingia nchini. Hii ni kuzingatia kuwa asilimia 70
ya bajeti ya TAA inatokana na makusanyo yake ya ndani yanayotokana tozo mbali
mbali za kuhudumia ndege na abiria viwanjani na asilimia 30 inatolewa na
Serikali. Aidha TAA ni mmoja ya taasis za umma zinazotoa changia vizuri pato la
taifa” alisema Dkt Chiguma.
Amesema
ugonjwa huu umeathiri hata safari za ndege zinazofanywa ndani ambazo zimeshuka
kwa asilimia 40, ambapo kwa ndege za Shirika la ndege la Tanzania (ATCL),
Precision Air, Coastal Aviation, Auric na nyingine zimepungua safari zao
kutokana na kupungua au kutokuwepo kwa abiria wanaotoka nje ya nchi waliokuwa
wakisafiri kwenda mikoa mbalimbali yenye vivutio vya asili.
Dkt.
Chiguma amesema bado ugonjwa huu upo nchini, hivyo wanatarajia kuwasilisha
rasmi maombi serikalini ya kuisaidia TAA iendelee kuhudumia viwanja vyetu
kulingana na viwango vya kimataifa vinavyotakiwa.
Hatahivyo,
ameipongeza menejimenti ya TAA, kuchukua hatua za haraka za kwa kufuta baadhi
ya matumizi yasiyo ya lazima kwa kuzingatia miruko ya ndege imepungua na
maelekezo ya Serikali ya kupambana na ugonjwa wa COVID 19 na kuzielekeza kwa
utunzaji na uendeshaji wa viwanja vya ndege na mapambano dhidi ya virusi vya
CORONA
Awali
Mkurugenzi Mkuu wa TAA, Mhandisi Mshauri Julius Ndyamukama aliiambia MAB kuwa
baada ya kusitishwa kwa safari za ndege za nje ya nchi na hata baadhi ya ndege
za ndani kupunguza miruko yake kwa asilimia 40, kutasababisha Mamlaka
kukabiliwa uhaba mkubwa wa fedha za uendeshaji wa shughuli mbalimbali na
kufanya zishindwe kufanyika kwa wakati, kutokana na kutegemea mapato yatokanayo
na ada za kutua na kuruka kwa ndege, maegesho ya ndege, tozo za abiria, pango
na maegesho ya magari.
Amesema
hadi sasa TAA imepoteza mapato makubwa ya zaidi ya asilimia 64.7 kwa kuwa
wanategemea zaidi Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA),
ambacho kinatumiwa asilimia 43 ya abiria wote Tanzania na asilimia 40 ya
Watalii wanaotoka nje ya nchi wanatumia kiwanja hiki. Kwa kuonyesha jinsi hali
ilivyo kwa sasa alisema mwezi Februari JNIA ilihudumia miruko ya ndege za nje 158,
hapa nchini (domestic) 167 na ndogo ndogo (general aviation) 465; ambapo kwa
mwezi Machi kabla ya kusitishwa kwa ndege za nje ya nchi abiria kutoka nje ya
nchi walipungua kwa asilimia 95 na wa ndani ya nchi walipungua kwa kiasi cha asilimia
60.
Aidha
katika utekelezaji wa maelekezo ya Serikali kupambana na virusi vya Corona
vinavyosababisha ugonjwa wa homa kali ya mapafu (COVID 19) TAA imehakikisha
wafanyakazi na wadau wake waliopo katika mazingira ya viwanja wanafuata
maelekezo ya kutaka kila mmoja anachukua hatua ya kujikinga ikiwa na kuepuka
mikusanyiko, kutumia zaidi simu za mezani, mawasiliano ya kieletroniki, kunawa
mikono mara kwa mara kwa kutumia maji tiririka na yenye dawa ya chlorine, pia
kumewekwa mabango yenye ujumbe wa namna ya kujikinga maeneo mbalimbali, pia TAA
wamenunua vifaa tiba kwa ajili ya watumishi wake zikiwemo barakoa, vitakasa
mikono na kipimia joto la mwili (thermostats), ambapo kabla ya kuingia ofisini
wanapimwa. Tunamshukuru Mungu hadi sasa hatuna Mtumishi aliyeathirika na
ugonjwa huu.
No comments:
Post a Comment