Habari za Punde

Amewataka Wananchi Waendelee Kushirikiana Ili Wahakikishe Uchaguzi Mkuu Utakaofanyika Mwezi Oktoba Mwaka Huu Unafanyika Kwa Amani na Utulivu - Al Hajj. Dk.Shein.jwa


Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Alhajj Dk.Ali Mohamed Shein, akiwahutubia Wananchi katika hafla ya Baraza la Eid Al Hajj lililofanyika Kitaifa Wilaya ya Kaskazini "B" Unguja katika Ukumbi wa Mitihani wa Skuli ya Sekondari ya Bumbwini leo.

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Alhaj Dk. Ali Mohamed Shein amewataka wananchi waendelee kushirikiana ili wahakikishe kwamba uchaguzi Mkuu utakaofanyika mwezi Oktoba mwaka huu unafanyika kwa amani na utulivu.
Alhaj Dk. Shein aliyasema hayo leo katika hotuba yake aliyoitoa katika Baraza la Idd El Hajj lililofanyika huko katika skuli ya Bumbwini, Wilaya ya Kaskazini “B”, Mkoa wa Kaskazini Unguja ambalo lilihudhuriwa na viongozi mbali mbali pamoja na wananchi.
Alhaj Dk. Shein alisema kwa kufanyika kwa uchaguzi kwa amani na utulivu kutaipelekea Serikali ya Awamu ya Nane itakapoingia madarakani iweze kuyashughulikia maendeleo ya nchi kwa ufanisi zaidi.
Hivyo, aliwataka wananchi wahakikishe kwamba hatokei mtu au kundi lolote litakalojaribu kuharibu amani hapa nchini, kupandikiza chuki, uhasama na fitna miongoni mwa wananchi na ndani ya jamii yao.
Alhaj Dk. Shein aliwasihi viongozi wa vyama vyote vya siasa na wagombea wao wakati ukifika wajinadi kwa wapiga kura kwa kutangaza Ilani, Sera na Mipango ya vyama vyao.
Aliwasisitiza kuwa ni lazima wahubiri amani, umoja na mshikamano kwa maneno na vitendo, wakijuwa kwamba lengo lao ni kujinadi ili wachaguliwe kwa ajili ya kuiletea maendeleo nchi na kutoa huduma bora kwa wananchi.
Aidha, Alhaj Dk. Shein aliwaeleza wananchi kwamba ni wajibu wao kuzingatia, kuheshimu na kuzitii sheria na miongozo ya Uchaguzi inayotolewa na Tume zote mbili za Uchaguzi ambazo ni (ZEC na NEC).
“Hivi sasa tunaelekea kwenye Uchaguzi Mkuu utakaofanyika katika mwezi wa Oktoba mwaka huu hivyo, tunapaswa tukumbuke kwamba msingi wa mafanikio yote tuliyoyapata katika awamu zote ni juhudi zetu za pamoja katika kufanya kazi, kuilinda amani na utulivu pamoja na kudumisha umoja na mshikamano”,alisema Alhaj Dk. Shein.
Alieleza kuwa hadi sasa nchi iko shwari, harakati za kisiasa, kiuchumi na kijamii zinaendelea vizuri na kueleza mategemeo yake kwamba hali hiyo itadumu hadi siku ya uchaguzi na baada ya uchaguzi.
Alisisitiza kuwa iwapo wananchi watafanya hivyo watatoa fursa nzuri kwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar Awamu ya Nane ya kuanza utekelezaji wa mipango yake ya maendeleo kwa wepesi, hamasa zaidi na ari kubwa ili hatimae iweze kupata mafanikio makubwa zaidi.
Pamoja na hayo, Alhaj Dk. Shein alisema kuwa ili kudumisha na kuuendeleza umoja ni lazima wananchi wajiepushe na tabia mbaya kama kudharauliana,kusengenyana, kuhusudiana, kuhasimiana na kushwawishiana katika kufanya hujuma dhini ya wananchi na Serikali na badaya yake wafanye mambo mema.
Alhaj Dk. Shein alitumia fursa hiyo kutoa shukurani zake za dhati kwa wananchi wote wa Zanzibar na Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa jumla kwa mapenzi makubwa waliyomuonesha na kwa kuiunga mkono Serikali katika kuyatekeleza majukumu yake kwa vipindi vyote viwili vya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Awamu ya Saba.
Alhaj Dk. Shein alitoa shukurani hizo kutokana na kuwa shughuli hiyo ya Baraza la Idd el Hajj iliyofanyika leo huko Bumbwini, Mwenyezi Mungu akipenda itakuwa ni ya mwisho kwake kuhudhudhuria na kutoa hotuba akiwa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi.
“Sote tunafahamu kwamba baada ya kufanyika uchaguzi Mkuu wa mwaka huu wa 2020 na kupatikana Rais mwengine wa Zanzibar kwa mujibu wa Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984 ndio itakuwa mwisho wa uongozi wangu sitoongeza hata dakika moja seuze sekunde moja”alisema Alhaj Dk. Shein.
Aidha, Rais Dk. Shein alisema kuwa katika Ibada ya Hijja mafunzo mengi yanapatikana ikiwemo usawa mbele ya sheria na umuhimu wake katika kutekeleza na kufanikisha mambo mbali mbali katika maisha ya mwanaadamu.
Aliongeza kuwa miongoni mwa mafunzo makubwa yanayopatikana katika utekelezaji wa ibada ya Hijja ni utii wa sheria pamoja na kuimarisha umoja na mshikamano katika hali ya amani na utulivu kwani mambo hayo ndio msingi mkubwa wa mafanikio.
Sambamba na hayo, Rais Dk. Shein alitoa pongezi kwa viongozi na wananchi wa Bumbwini kwa kushirikiana na Halmashauri ya Wilaya ya Kaskazini “B” pamoja na Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali kwa ujenzi wa ukumbi uliofanyika Baraza hilo la Idd el Hajj.
Pia, aliuagiza Uongozi wa Wizara ya Elimu ushirikiane na uongozi wa Wilaya ya Kaskazini “B” na Mkoa huo wa Kaskazini kwa ajili ya kulikagua eneo linalokusudiwa kujengwa skuli ya Bumbwini Gongoni kwenye kijiji kipya kwa ajili ya kutatua changamoto ya msongamano wa wanafunzi katika skuli ya Bumbwini.
Hivyo, alisisitiza kwamba dhamira ya Serikali hivi sasa ni kujenga Skuli za ghorofa ili kuwepo kwa matumizi bora ya ardhi hivyo, ni vyema suala hilo likazingatiwa katika ujenzi wa skuli hio.
Pia, Alhaj Rais Dk. Shein alisema kuwa ikithibitika kwamba eneo la karibu na Skuli ya Pangatupu linafaa kwa kuzingatia mipango miji na vijiji iliyopo na maendeleo ya muda mrefu ya Mkoa huo, basi aliuagiza uongozi wa Mkoa uanze mradi huo japo kwa kujenga jengo moja dogo kama ni kielelezo cha utekelezaji wa dhamira hiyo.
Halikadhalika, alisema kuwa Mkoa wa Kaskazini Unguja hivi sasa unaongoza hapa Zanzibar kwa kuwa na barabara mpya, nzuri na za kisasa hivyo alitoa pongezi kwa wananchi waliokubali bila ya masharti kupitisha miradi ya ujenzi wa barabara katika mikoa yote ya Unguja na Pemba.
Alhaj Dk. Shein pia, alieleza  juu ya mpango wa ujenzi wa barabara ya Makoba hadi Kiongwe pamoja na barabara ya Bumbwini hadi Mahonda na kueleza kuwa hiyo ni ahadi ya Serikali na kwa vyovyote vile zitatekelezwa.
Kwa upande wa daraja la Mperura linalounganisha eneo la Bumbwini Misufini na Pangatupu lililoporomoka alisema kuwa Serikali inaandaa mipango ya kulifanyia matengenezo daraja hilo katika kipindi kifupi kijacho.
Katika hafla hiyo Alhaj Dk. Shein pia, aliwataka wananchi waliohudhuria Baraza hilo kusimama kwa muda wa dakika moja kwa ajili ya kumkumbuka Rais Mstaafu wa Awamu ya Tatu Marehemu Benjamin William Mkapa aliyefariki usiku wa tarehe 23 Julai na kuzikwa nyumbani kwao Lupaso hapo juzi tarehe 29 Julai, 2020.
Mapema Alhaj Dk. Shein alihudhuria sala la Idd el Hajj iliyosaliwa katika uwanja wa mpira Misuka hapo Mahonda na baadae alisalimiana na Masheikh katika ukumbi wa Halmashauri ya Wilaya hiyo huko Kinduni.
Viongozi mbali mbali walihudhuria katika Baraza hilo akiwemo Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassam, Balozi Seif Ali Idd Makamo wa Pili wa Rais, Dk. Hussein Ali Hassan Mwinyi, Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, ambaye pia, ni Mgombea Urais wa Chama Cha Mapinduzi (CCM),

Wengine ni viongozi wa dini, Jaji Mkuu wa Zanzibar Omar Othman Makungu, Mawaziri na Manaibu Mawaziri,Katibu Mkuu Kiongozi na Katibu wa Baraza la Mapinduzi Dk. Abdulhamid  Yahya Mzee, Wabunge, Wawakilishi Makatibu Wakuu na Manaibu Makatibu Wakuu, Wakuu wa Mikoa yote ya Zanzibar, Mabalozi na viongozi wengine wa Serikali, viongozi wa vyama vya siasa, wageni waalikwa na wananchi.    
Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.