Habari za Punde

NEC yawataka maofisa na maofisa wasaidizi wa uchaguzi kuzingatia matakwa ya Katiba, Sheria na Kanuni


Na Jaala Makame Haji - ZEC

TUME ya Taifa ya Uchaguzi Tanzania  (NEC), imewataka maofisa na maofisa wasaidizi wa uchaguzi Unguja, kuhakikisha wanazingatia matakwa ya katiba, Sheria na kanuni zinazosimamia uchaguzi.

Kauli hiyo ilitolewa na Makamo Mwenyekiti wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi Jaji mstaafu wa rufaa Mbarouk Salim Mbarouk, wakati akifungua mafunzo ya siku tatu kwa maofisa hao katika ukumbi wa Shekh Idrissa Abdulwakil Kikwajuni.

Alisema pamoja na baadhi ya maofisa hao kuwa na uzoefu katika kuendesha uchaguzi lakini wanatakiwa kuzingatia maelekezo watakayopewa na Tume badala ya kufanya kazi hizo za uchaguzi kwa mazoea.

Aidha, alisema uchaguzi ni mchakato unaojumuisha hatua na taratibu mbalimbali za kufuatwa na kuzingatia kwani hatua na taratibu hizo ndio msingi wa uchaguzi kuwa mzuri wenye ufanisi na kuondoa malalamiko au vurugu wakati wote wa mchakato wa uchaguzi.

Makamo huyo, alisema Nec imewaamini kuwateuwa kwa sababu wanao uwezo wa kufanya kazi hiyo hivyo ni jambo la muhimu kujiamini na kujitambua kwamba wanapaswa kuzingatia katiba ya nchi, sheria za uchaguzi, kanuni zake na maadili ya Uchaguzi.

Hata hivyo, alibainisha kuwa kwa mujibu wa katiba ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania ibara ya 74 (6) tume imepewa jukumu la kusimamia na kuratibu uendeshaji wa uchaguzi wa Rais na wabunge wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania na madiwani kwa Tanzania bara.

"Tume imewateuwa nyinyi kwa mujibu wa sheria na kuzingatia utendaji na uzoefu wenu katika masuala ya Uchaguzi," alisema.

Hivyo aliwasisitiza kuwa katika utekelezaji wa majukumu yao ni muhimu kuzishirikisha vyama vya siasa na wadau wengine wa uchaguzi katika masuala ambayo yanastahili kushirikishwa.

Sambamba na hayo alisema ni muhimu kuyajua na kuyatambua vyema maeneo yao wanayofanyia kazi ikiwemo miundombinu ya kufika katika kata na vituo vya kupigia kura.

Aliwasisitiza kuzingatia mafunzo watakayopewa na kutosita kutoa uzoefu wa usimamizi wao ili iwe ni somo kwao wote katika utekelezaji wa jukumu hilo.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Idara ya Sheria NEC, Emmanuel Kawisha, alisema chini ya kanuni ya 16 (1) (b) na (3) ya kanuni za uchaguzi wa Rais na wabunge 2020 na kanuni ya 14 (1) (b) na (3) ya kanuni za uchaguzi wa serikali za mitaa msimamizi yoyote hatotakiwa kuwa mfuasi wa chama chochote cha siasa na kufanya hivyo ni kwenda kinyume na sheria ya uchaguzi.

Hivyo aliwasisitiza maofisa hao kuhakikisha hawavai sare za chama wala kushabikia chama chochote cha siasa kuanzia sasa na yoyote atakaebainika kufanya hivyo atavuliwa cheo chake na kupewa mtu mwengine atakaeweza kutunza kiapo cha uchaguzi.

Alisema kwa mujibu wa kifungu cha 89 a na b cha sheria ya uchaguzi mtendaji au msimamizi yoyote atakaesababisha uchaguzi kuharibika basi atatozwa faini ya shilingi 1,000,000 au miaka miwili jela au vyote viwili kwa pamoja.

Mbali na hayo aliwasihi kutunza siri za kiapo kwa kuzingatia katiba na sheria ya uchaguzi.

Hata hivyo alisema kuna makosa ambayo yanafanywa na watendaji wa uchaguzi wakati wa uchaguzi ikiwemo usimamizi hafifu wa maofisa katika vituo vya kupigia kura na kukosa umakini katika kuchagua watendaji mbalimbali wa uchaguzi.

Mkurugenzi wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi Zanzibar, Hamidu Mwanga, aliwaomba maofisa hao kuimarisha mahusiano ya karibu katika kuhakikisha zoezi la uchaguzi linafanyika kwa urahisi Oktoba 28 mwaka huu.

Katika Mkutano huo mada mbalimbali ziliwasilishwa ikiwemo mambo muhimu ya kuzingatia katika kutoa mafunzo kwa watendaji wa uchaguzi, majukumu ya watendaji wa uchaguzi na mambo muhimu ya kuzingatia, uteuzi wa wagombea na wajibu na majumu ya watendaji wa vituo na mawakala wa vyama vya siasa.


No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.