Na Takdir Suweid
Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii Zanzibar, Mhe Nassor Ahmed Mazrui amewataka wazee kuchanja chanjo ya corona ili kujikinga na athari zinazoweza kujitokeza.
Ameyasema hayo huko katika ukumbi wa Hoteli ya Abla Mtoni wakati wa uzinduzi wa Baraza la Wazee Jimbo la Mtoni.
Amesema maradhi hayo yanawaathiri zaidi wagonjwa na wazee hivyo kuwapatiwa chanjo huyo kutawasaidia kupunguza nguvu za maradhi.
Aidha amesema matibabu ya maradhi hayo ni gharama kubwa hivyo hakuna budi kupatiwa chanzo hizo ili kuwaepushia wakati yatakapowapata.
Hata hivyo Serikali imejipanga kuwapatia chanjo hizo wazee popote walipo katika maeneo yao bila usumbufu wowote na kuwaomba wananchi kuunga mkono juhudi hizo ili ziweze kufanikiwa.
Kwa upande wake mwakilishi wa Jimbo la mtoni Hussein Ibrahim Makungu (BHAA) amesema wanachukua juhudi mbalimbali za kuboresha maisha ya wazee hao lakini baadhi yao wanakabiliwa na tatizo la kukosa matunzo ya uhakika na maradhi Mambo ambayo wanawaweka katika wakati mgumu.
Hata hivyo amewaomba viongozi wa majimbo kuandaa mikakati madhubuti ya kuweza kuwasaidia wazee katika maeneo yao kwani wametoa mchango mkubwa kwa familia na taifa kwa ujumla.
Katika uzinduzi huo mh Mazrui amekabidhi sh. Milioni 2, na Mwakilishi wa Jimbo la mtoni Hussein Ibrahim Makungu amekabidhi Milioni 2 na pia wazee hao walipatiwa chanjo ya corona na ziara ya utalii katika eneo Fumba.
No comments:
Post a Comment