Habari za Punde

Makatibu wa Uenezi CCM Zanzibar wapigwa msasa

KATIBU wa Kamati Maalum ya NEC,Idara ya Itikadi na Uenezi CCM Zanzibar Ndg.Mbeto Khamis Mbeto(wa pili kulia),Katibu wa Kamati Maalum ya NEC,Idara ya Organazesheni Zanzibar Ndg.Omar Ibrahim Kilupi(kushoto) na Katibu Msaidizi Mkuu Idara ya Itikadi na Uenezi Ndg.Daud Ismail Juma (kulia) wakizungumza na Makatibu wa siasa na uenezi(hawapo pichani) huko Afisi Kuu ya CCM Kisiwandui.
Katibu wa Kamati Maalum ya NEC,Idara ya Organazesheni Zanzibar Ndg.Omsr Ibrahim Kilupi akizungumza na Makatibu hao.(PICHA NA IS-HAKA OMAR).

NA IS-HAKA OMAR,ZANZIBAR.

MAKATIBU wa Siasa na Uenezi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Zanzibar wametakiwa kuwa wabunifu na wachapakazi katika kueneza na kutangaza utekelezaji wa miradi ya maendeleo.

Rai hiyo imetolewa na Katibu wa Kamati Maalum ya NEC,Idara ya Itikadi na Uenezi CCM Zanzibar Ndg.Khamis Mbeto Khamis wakati akizungumza na makatibu hao wa ngazi za majimbo hadi mikoa huko Afisi Kuu ya CCM Kisiwandui Zanzibar.

Amewakumbusha makatibu hao kuwa wanatakiwa kutangaza utekelezaji wa Ilani ya CCM ya mwaka 2020/2025 inayotekelezwa katika maeneo yao.

Alieleza kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ya awamu ya nane chini ya uongozi wa Rais Dk.Mwinyi inatekeleza kwa ufanisi mkubwa Ilani ya CCM.

Katika maelezo yake Mbeto,aliwambia watendaji hao kuwa wanatakiwa kubadilika kiutendaji na kufanya kazi kwa bidii ili waende sambamba na kasi ya CCM kiutendaji.

“Makatibu nyinyi ndio mdomo wa Chama chetu mliopewa dhamana ya kusema na kufafanua mambo yote mazuri yanayofanywa na Chama pamoja na Serikali zetu kwa ujumla.

Tuna kazi kubwa ya kueneza na kuwambia wananchi mafanikio yanayopatikana katika maeneo yenu kunajengwa barabara za lami,maji safi na salama,hospitali zenye hadhi ya kimataifa,shule za kisasa na mengine mengi yanayotakiwa kujulikana kwa umma.”,alieleza Mbeto,

Alisema wananchi wanatakiwa kujua kwa kina utekelezaji wa ahadi zilizotolewa na CCM katika kampeni za uchaguzi mkuu uliopita ili wajiridhishe.

Alisema Zanzibar inaendelea kupiga hatua kubwa katika sekta za utalii,afya,kilimo,uvuvi,maji safi na salama,miundombinu ya umeme,usafiri wan chi kavu na baharini,usafiri wa anga,uwezeshaji wananchi kiuchumi pamoja na ustawi wa jamii.

Pamoja na hayo alieleza kuwa CCM itaendelea kufanya siasa za kisayansi zinazobeba dhana ya kumiza ahadi kwa vitendo badala ya maneno.

Naye Katibu wa Kamati Maalum ya NEC,Idara ya Organaizeshe CCM Zanzibar Ndg.Omar Ibrahim Kilupi, alisema kipaumbele chake ni kutekeleza ibara ya tano ya Katiba ya CCM ya mwaka 1977 toleo la mwaka 2022,kuhakikisha Chama kinashinda kwa kishindo kwa kila uchaguzi.

Alisema ushindi wa CCM utapatika kutokana na juhudi kubwa za kutangaza fursa na maendeleo yanayofanywa na serikali ili wananchi wajue na kuendelea kujenga imani kwa Chama walichokipa ridhaa ya kuongoza dola.

Kupitia kikao hicho Ndg.Kilupi, aliwataka wabunge,wawakilishi na madiwani kutatua changamoto mbalimbali zinazowakabili wananchi majimboni.

 

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.