Habari za Punde

Mhe.Kairuki Akutana na Rais wa Baraza la Utalii Duniani, Wajadili Kukuza Utalii Nchini

Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Angellah Kairuki (Mb) (kushoto) akizungumza na Rais na Mkurugenzi wa Baraza la Utalii Duniani (World Travel Tourism Council), Julia Simpson  (katikati) kuhusu kushirikiana katika kutangaza utalii katika kikao kilichofanyika kwenye ukumbi wa hoteli ya Four Seasons, jijini Riyadh Saudi Arabia.

Na. Riyadh, Saudi Arabia.

Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Angellah Kairuki (Mb) amekutana na kufanya mazungumzo  na Rais ambaye pia ni  Mkurugenzi Mkuu wa Baraza  la Utalii Duniani (World Travel Tourism Council (WTTC) , Bi. Julia Simpson kwa lengo la kujadili namna bora ya kushirikiana katika kutangaza na kukuza utalii endelevu nchini Tanzania.

Kikao hicho kilifanyika kwenye  ukumbi wa hoteli ya Four Seasons jijini Riyadh, Saudi Arabia.

Tanzania ikiwa mwanachama wa WTTC itaendelea kujitangaza Kimataifa  na itapata fursa ya kuwa mjumbe katika nafasi  mbalimbali.

Baraza hilo lina mtandao wa mashirika binafsi  zaidi ya 200 Duniani wanaotoa huduma mbalimbalia zenye lengo la kukuza utalii.

Aidha, katika kuendelea kutangaza utalii na kutafuta masoko mapya ya utalii, Mhe. Kairuki  amefanya mazungumzo na wadau wakubwa wa utalii duniani ikiwa ni pamoja na Meneja Masoko wa  Shirika la Ndege la Saudi Arabia, Abdulrahman Alabdulwahab kwa lengo la kuangalia namna bora ya kuitangaza Tanzania kupitia ndege za shirika hilo na  kushirikiana katika kutangaza vivutio vya Utalii nchini.

Pia, amekutana na Mkurugenzi Mkuu wa City Sightseeing World wide,  Enrique Ybarra kwa lengo la kuangalia namna bora ya kuweka matangazo ya vivutio vya Tanzania kwenye vyombo vyake vya usafiri, na katika tovuti maarufu duniani ijulikanayo kama Isango.

Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Angellah Kairuki (Mb)(wa pili kushoto)  akizungumza na Meneja Masoko wa Shirika la Ndege la Saudi Arabia, Abdulrahman Alabdulwahab (kushoto) kuhusu namna bora ya kutangaza vivutio vya utalii kupitia ndege za shirika hilo, katika kikao kilichofanyika kwenye ukumbi wa hoteli ya Four Seasons, jijini Riyadh Saudi Arabia.

Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Angellah Kairuki (Mb)(kulia) akizungumza na Mkurugenzi Mkuu wa City Sightseeing World wide, Enrique Ybarra  (katikati)uhusu kutangaza vivutio vya utalii kupitia vyombo vyake vya usafiri, na tovuti yake maarufu duniani ijulikanayo kama Isango, katika kikao kilichofanyika kwenye ukumbi wa hoteli ya Four Seasons, jijini Riyadh Saudi Arabia.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.