Habari za Punde

NAIBU WAZIRI CHUMI APONGEZA MABORESHO YANAYOENDELEA AICC


Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Cosato Chumi akimsikiliza Mkurugenzi Mtendaji wa AICC Bi. Christine G. Mwakatobe alipotembelea moja ya ukumbi wa mkutano ulifanyiwa maboresho.

Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Cosato Chumi akiwa akimsikiliza Mkurugenzi Mtendaji wa AICC Bi. Christine G. Mwakatobe alipotembelea eneo la ujenzi wa mradi wa ukumbi mpya wa kisasa uliopo mbioni kuanza kutelezwa.

Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Cosato Chumi, amepongeza jitihada kubwa za maboresho ya miundombinu na uendeshaji zinazoendelea katika katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Arusha (AICC) jijini Arusha.

Naibu Waziri Chumi amebainisha hayo wakati wa ziara yake ya kikazi aliyofanya katika kituo hicho cha mikutano tarehe 14 Agosti 2025 ambapo pia alipata fursa ya kutembelea eneo la ujenzi wa mradi wa ukumbi mpya wa kisasa uliopo mbioni kuanza kutelezwa.

Ziara hiyo iliyolenga kujionea hatua iliyofikiwa katika maboresho ya kituo hicho katika nyanja mbalimbali ikiwemo marekebisho ya miundombinu ya msingi ikiwemo kumbi za mikutano, maeneo ya mapokezi ya wageni, ujenzi wa lifti mpya za kisasa, pamoja na vifaa vya kisasa vinavyotumika katika mikutano ya kimataifa.

“Nimefurahishwa sana na hatua kubwa ambayo AICC 

imefikia katika maboresho ya huduma na miundombinu 

yake. Mageuzi haya yaliyofanyika katika kituo hiki muhimu 

kwa Taifa na Afrika Mashariki yanaakisi maono na dhamira 

ya dhati ya Serikali ya awamu ya sita katika kuhakikisha 

taasisi zake zinatoa huduma bora zinazokidhi viwango vya 

kimataifa” alisema Mhe. Chumi.


Vilevile Mhe. Chumi alieleza kuridhishwa kwake na kasi ya 

utendaji na weledi wa Menejimenti ya kituo hicho ikiongozwa 

Mkurugenzi Mtendaji Bi. Christine G. Mwakatobe, katika 

utekelezaji wa maboresho hayo ambayo yana lengo la 

kuimarisha uwezo wa AICC katika kuhudumia mikutano ya 

kitaifa na kimataifa kwa ufanisi mkubwa zaidi.

Aidha, Naibu Waziri alisisitiza kuhusu umuhimu wa AICC 


kwenye utekelezaji wa dhana ya diplomasia ya uchumi na 


nafasi yake kama lango la kukuza ushirikiano wa kikanda 


kupitia mikutano ya kimataifa na shughuli za kidiplomasia. 


Aliendelea kubainisha kuwa uboreshaji wa miundombinu hiyo 


unakwenda sambamba na mkakati wa serikali wa kuvutia 


wawekezaji na watalii kutoka mataifa mbalimbali duniani.



Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa AICC 


Bi. Christine G. Mwakatobe alieleza kuwa maboresho hayo 


yanajumuisha ukarabati wa ukumbi wa Simba, matumizi ya 


teknolojia ya kisasa katika mifumo ya mawasiliano na 


uendeshaji wa mikutano, ulinzi na usalama, maboresho ya 


huduma za afya katika hospitali ya AICC, pamoja 


na kuboresha mazingira ya kazi kwa watumishi.


“Tumejipanga kuwa kituo kinachoongoza kwa ubora wa huduma Afrika Mashariki. Tunawashukuru viongozi wetu kwa kutupa msukumo wa maendeleo na kutufuatilia kwa karibu,” alisema Bi. Mwakatobe.


Ziara ya hiyo ya Mhe. Chumi imekuja wakati ambapo AICC imeongeza kasi ya utekelezaji wa miradi ya maboresho, ikiwa ni sehemu ya mikakati ya kujiweka katika nafasi nzuri ya ushindani wa kimataifa kama kituo bora cha mikutano barani Afrika.


Mbali na hayo, Mhe. Chumi akizungumza na menejimenti ya AICC, amewahimiza kuendelea kubuni mikakati ya kuvutia matukio makubwa ya kimataifa na kuwashirikisha wadau mbalimbali ili kuongeza tija na mchango wa kituo hicho katika pato la taifa na maendeleo ya mkoa wa Arusha kwa ujumla.

Katika ziara hiyo, Mhe. Chumi alipokelewa na uongozi wa juu wa AICC ukiongozwa na Mkurugenzi Mtendaji Christine G. Mwakatobe pamoja na maafisa wengine waandamizi.  

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.