6/recent/ticker-posts

Zanzibar yapongezwa kwa kutekeleza vyema programu ya huduma za kilimo na maendeleo ya sekta ya mifugo

Na Said Ameir, Ikulu
 
Mkurugenzi wa  IFAD wa Kanda ya Kusini na Mashariki mwa Afrika Bwana  Perin Saint ameipongeza Serikali ya Mapinduzi Zanzibar kwa kutekeleza vyema  programu ya Huduma za Kilimo na Maendeleo ya sekta ya Mifugo (ASSP/ASDP–L)
nchini.
 
Mkurugenzi huyo ambaye alifika Ikulu kusalimiana na Rais wa Zanzibar na  Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein alimueleza azma ya  IFAD YA kufanya mkutano wake mkuu wa mwaka huu hapa Zanzibar kutokana na  Mfuko huo kuridhika na mazingira yaliyopo nchini.
 
Amesema Zanzibar imekuwa nchi ya mfano katika kutekeleza programu  za  Huduma za Kilimo na Maendeleo ya sekta ya Mifugo (ASSP/ASDP–L)  zinazogharamiwa na mfuko huo katika Kanda ya Kusini na Mashariki mwa Afrika,  na kwamba IFAD imeridhishwa na hatua ya serikali katika kusimamia programu  hizo.
 
Amesema kutokana na mafanikio ya utekelezaji wa program hizo, Shirika lake  linatarajia kuongeza muda wa miradi hiyo hapa Zanzibar. Programu hizo ambazo  zimegharimu kiasi ya dola milioni tisa za Marekani (USD milioni 9), zilianza  kutekelezwa mwaka 2007 na zinatarajiwa kumalizika mwaka 2014.

Bwana Perin L. Saint Ange amesema ameshuhudia maendeleo makubwa katika  sekta mbali mbali siyo tu katika kilimo, lakini vile vile katika sekta za utalii, mazao  ya viungo na mazao ya baharini, jambo ambalo amesema ni ishara ya mafanikio  makubwa katika kukuza uchumi wa Zanzibar.
1
Aidha, amesema ameona mafanikio yaliyopatikana katika mazao mbali mbali  lakini hasa zao la vanila ambalo alisema  litasaidia katika kuongeza idadi ya viungo  na hivyo kuifanya Zanzibar kuongeza umaarufu wake katika mazao ya viungo.
 
Hata hivyo, amesisitiza kuwa huu ni wakati muafaka kwa Zanzibar kuelekeza  nguvu zake katika mazao ya baharini kwani alisema, nchi za visiwa zina fursa ya  kipekee katika kuendeleza uchumi huo, na kwamba Mfuko wa Kimataifa Kanda  ya Kusini na Mashariki mwa Afrika imeweka kipaumbele kwenye uchumi wa aina  hiyo.
 
Ameongeza kuwa jumuiya za kimataifa zimeonesha hamu kubwa ya kuendeleza  na kusaidia nchi za visiwa katika kuwekeza kwenye uchumi wa baharini hivyo  ameitaka Zanzibar kuichangamkia fursa hiyo.
 
Naye Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed  Shein amesema mafanikio makubwa yanayoonekana katika kuimarisha kilimo na  mazao ya baharini yanatokana na utekelezaji wa mpango wa miaka mitano wa  serikali ya Mapinduzi Zanzibar.
 
Akizungumza na ujumbe huo, Dk. Shein amesema serikali imejipanga vizuri  katika kuleta Mapinduzi ya kilimo na Mapinduzi ya uvuvi ambapo mkazo zaidi
umewekwa katika kuimarisha ukulima wa mwani, ufugaji wa samaki na uvuvi wa
bahari kuu.
Amesema uimarishaji wa sekta ya uvuvi ulianza zamani kwenye miaka ya sabiini,
lakini ulionekana kupungua kasi kwa kipindi kirefu kutokana na changamoto mbali
mbali kabla ya serikali anayoiongoza kuamua kuishughulikia kikamilifu sekta ya
kilimo na uvuvi.
“Serikali ilidhamiria kuiendeleza sekta ya uvuvi tokea kwenye miaka ya 70, lakini
kutokana na changamoto mbali mbali ikiwemo fedha, tulishindwa kufanya vizuri
kwa muda mrefu, na sasa tumeanza kupata matumaini katika utekelezaji wa
mpango wa serikali wa miaka mitano” alisema Dk. Shein.
Amesema tafiti zinaonesha kuwa kuna samaki wengi katika bahari ya Zanzibar
kama vile Jodari ambao wanahitajika sana kwenye soko la dunia, lakini wavuvi
2
wa Zanzibar wanashindwa kuwavua samaki hao kutokana na kushindwa kuvua
kwenye maji ya kina kikubwa na kutokuwa na vifaa vinavyohitajika kuvua samaki
hao.
Aliufahamisha ujumbe huo kwamba serikali tayari imeshachukua juhudi mbali
mbali za kuimarisha sekta ya uvuvi ikiwa ni pamoja na kutiliana saini makubaliano
ya kuiendeleza sekta hiyo na nchi ya China na Vietnam.
Kuhusu zao la mwani, Rais wa Zanzibar amesema maendeleo makubwa yameanza
kupatikana katika zao hilo kutokana kuweza kuongezewa thamani, ambapo
mwani umekuwa malighafi ya kutengenezea supu, keki na vitu vingine mbali
mbali.
Katika ujumbe wake Bwana Perin Saint Ange alifuatana na Mkurugenzi wa
Divisheni ya Ufundi anayefanyia kazi zake nchini  Italia Bwana Adolf Bizzi, Mratibu
Mkuu wa Masuala ya Uchumi wa Kanda Bwana Godfrey Livingstone, Mratibu
mkuu wa Mradi nchini Tanzania Bwana Francisco Pichonkuu, Meneja wa Mradi
nchini Tanzania Bibi Mariam Okongo na Afisa wa mradi huo nchini Tanzania Dr.
Mwatima Abdalla  Juma.
Postal Address: 2422 Tel.+255 776 613 015, Fax: 024 2231822    E-mail:
saidameir@ikuluzanzibar.go.tz & sjka1960@hotmail.com

Post a Comment

0 Comments