Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar Maalim Seif Sharif Hamad akiangalia “bango kitita” lililowasilishwa na muhasibu wa Idara ya dawa za kulevya Bw. Said Ali Salum, wakati alipotembelea Idara hiyo iliyoko Sogea, mjini Zanzibar. (Picha, Salmin Said, OMKR).
Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar Maalim Seif Sharif Hamad na Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais Dr. Islam Seif (kushoto), wakipata maelezo kutoka kwa Mkurugenzi Idara wa Watu Wenye Ulemavu Bi Abeida Rashid wakati wa ziara ya Makamu wa Kwanza wa Rais katika Idara hiyo.
Na Hassan Hamad (OMKR).
Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar Maalim Seif Sharif Hamad amewataka watendaji wa serikali kufuatilia matokeo ya tafiti mbali mbali zilizofanywa ili yaweze kusaidia mipango ya maendeleo.
Akizungumza na watendaji wa Idara ya watu wenye ulemavu ikiwa ni mfululizo wa ziara zake za kutembelea ofisi za serikali, Maalim Seif amesema taarifa za tafiti mbali mbali zikiwemo sensa ni muhimu katika kupanga shughuli za maendeleo kwa maidara ya serikali na taifa kwa jumla.
Makamu wa Kwanza wa Rais ametoa kauli hiyo baada ya kusikiliza maelezo ya kiutendaji kutoka kwa wafanyakazi wa Idara hiyo, sambamba na kukagua mpango kazi na utekelezaji wa majukumu kwa idara hiyo.
Pia ameelezea umuhimu wa mafunzo kazini katika jitihada za kuwajengea uwezo watendaji wa ngazi mbali mbali, pamoja na kuelezea haja kwa watendaji kufanya kazi kwa mashirikiano ili kuziba mapengo ya kiutendaji pale yanapojitokeza.
Kwa upande wake Mkurugenzi wa Idara ya watu wenye Ulemavu Zanzibar Bi Abeida Rashid amesema tayari idara yake imeshatekeleza mipango mbali mbali ikiwa ni pamoja na kuzindua muongozo wa lugha ya alama wenye lengo la kuiwezesha jamii kujifunza lugha hiyo na kuweza kuwasaidia watu wenye ulemavu wa kusikia.
Mpango mwengine uliotekelezwa katika Idara hiyo ni pamoja na kuundwa kwa kamati ya kutunisha mfuko wa watu wenye ulemavu yenye wajumbe wanane, lengo likiwa kutunisha mfuko wa watu wenye ulemavu nchini katika kuendeleza harakati zao za kujiletea maendeleo.
Wakati huo huo Makamu wa Kwanza wa Rais ametembelea Tume ya kuratibu na Udhibiti wa dawa za kulevya ambako amesema kuwa serikali inakusudia kuifanya Zanzibar kuwa eneo salama lisilokuwa na wasambazaji na watumiaji wa dawa za kulevya.
Amesema changamoto kubwa iliyopo hivi sasa ni kutoa mwamko kwa jamii ili kuchukia matumizi ya dawa za kulevya ikizingatiwa kuwa dawa hizo zinaweza kuiathiri kila familia.
Amesema iwapo jamii itachukia dawa za kulevya na kushirikiana katika kuzitokomeza, malengo ya kuifanya Zanzibar isiyokuwa na dawa za kulevya yanaweza kufikiwa kwa urahisi.
“Tukiamua sisi wananchi kuwa hatutaki dawa za kulevya katika maeneo yetu basi dawa haziingii na wala hazitumiwi, muhimu ni kushirikiana katika jambo hili na kwa kweli tunataka Zanzibar isiyokuwa na matumizi ya dawa za kulevya”, alisisitiza.
Pia Maalim Seif amehimiza haja ya kuwa na wataalamu wa fani mbali mbali katika taasisi hiyo ambao watasaidia kukuza uelewa kwa watendaji wa taasisi hiyo na wananchi kwa ujumla.
Nae Mkurugenzi wa Tume ya Kuratibu na Udhibiti wa Dawa za Kulevya Zanzibar Bw. Ahmed Awadh Salim amesema wanakusudia kushauriana na Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali ili kuangalia uwezekano wa kuliingiza suala la dawa za kulevya katika mtaala wa elimu Zanzibar.
Amesema mbali na malengo hayo, Idara hiyo inaendelea kufanya kazi kwa karibu na jamii kwa kutoa elimu juu ya athari za matumizi ya dawa hizo kwa jamii ambapo wameweza kuwashajiisha vijana kadhaa kuachana na dawa na kujiunga na sober houses.
Hata hivyo, Bw. Ahmed amesema Idara hiyo inakabiliwa na uhaba wa nyumba za kuwatunza watu walioamua kuachana na dawa hizo na kuiomba serikali na washirika wa maendeleo kuangalia namna na kupata nyumba nyengine ili kuwawezesha vijana hao kupata pahala pazuri pa kuishi na kujifunza tabia njema.
No comments:
Post a Comment