Habari za Punde

Walioshindwa kulima watakiwa kuyarudisha mashamba


Na Mwandishi wetu, Hanang
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jakaya Mrisho Kikwete amesema kama watu waliobinafsishiwa mashamba ya kilimo cha ngano ya Basutu, wilayani Hanang, wameshindwa kulima ngano basi wayarudishe serikalini.

Aidha, Rais Kikwete alisema mashamba hayo hayakupewa watu binafsi ili nao watumie ardhi hiyo kuwakodishia wananchi bali walipewa kulima ngano.

Na ili kupata ufumbuzi wa matumizi ya mashamba hayo, Rais Kikwete alimwagiza Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Erasto Mbwilo kukaa chini na Kamati ya Maendeleo ya Mkoa (RDC) kujadili masuala yote yanayohusu mashamba hayo na kutoa mapendekezo kwa serikali.


Rais Kikwete aliyaeleza hayo kwenye mkutano wa hadhara wa wananchi wa Katesh, Hanang wakati aliposimama kwa muda mjini hapo akiwa njiani kutoka Babati, Manyara, kwenda Singida kwa ziara ya siku mbili kukagua miradi ya maendeleo.

Rais Kikwete wakati anataka waliopata mashamba hayo katika zoezi ya ubinafsishaji kulima ngano kama ilivyotakiwa lakini pia ametaka wananchi ambao aliwagawia mashamba mawili ya serikali katika eneo hilo nao wayatumie mashamba hayo kama walivyoomba.
“Napenda pia kuwataka wale wananchi waliopewa ardhi katika yale mashamba yaliyokuwa ya serikali nao wahakikishe kuwa mashamba hayo yanafanya kazi,” alisema Rais Kikwete.
Rais Kikwete alilizungumzia suala hilo baada ya Mbunge wa Viti Maalum wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Rose Kamili kulalamikia kutokutumika kwa mashamba hayo yaliyobinafsishwa kwa watu binafsi baada ya kushindwa kufanya kazi.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.