Na Mwandishi wetu,Singida
RAIS Jakaya Kikwete ameweka jiwe la
msingi kwenye mradi mkubwa wa maji unaolenga kumaliza tatizo la maji mjini
Singida.
Rais Kikwete aliweka jiwe la msingi
katika sherehe ya kufana iliyofanyika katika eneo la mradi la Mwankoko, nje ya
mji wa Singida, mara baada ya kuwasili mkoani Singida kuanza ziara ya siku
mbili kukagua na kuzindua miradi ya maendeleo akitokea mkoani Manyara ambako
alifanya shughuli hizo hizo kwa siku mbili pia.
Mradi huo ulioanza kujengwa Novemba 2,
mwaka 2009, umekamilika kwa kiasi cha asilimia 80 na unatarajiwa kukamilika
ifikapo Disemba 31, mwaka huu.
Kwa mujibu wa maelezo ya wasimamizi wa mradi
wa SUWASA, mradi huo unagharimu dola za Marekani milioni 19.7 sawa na shilingi
bilioni 31.126.
Kati ya fedha hizo, Serikali ya Tanzania
imetoa dola za Marekani milioni 10.42 sawa na shilingi 16, 463,600,000, Benki
ya Maendeleo ya Nchi za Kiarabu (BADEA) imetoa dola za Marekani milioni 4.57
sawa na shilingi 7,220,600,000 na Mfuko wa OPEC kwa Maendeleo ya Kimataifa wa
OFID umetoa dola za Marekani milioni 4.7 sawa na shilingi 7,426,000,000.
Mradi huo unaotekelezwa na kampuni ya
Spencon Services Limited unatarajiwa kutoa lita 17,208,000 kwa siku kutokana na
visima viwili vilivyoko Mwankoko vyenye uwezo wa kuzalisha lita 292,000 kwa saa
na visima viwili vilivyoko eneo la Irao vyenye uwezo wa kuzalisha lita 425,000.
Mradi huo unatarajiwa kutoa huduma kwa
jumla ya wateja 3,500 kati yao
2,500 katika awamu ya kwanza na wengine 1,000 katika awamu ya pili.
Aidha utaongeza upatikanaji wa maji kwa karibu kiasi
cha asilimi 100 kwa wakazi wa mji wa Singida na utaongeza muda wa kupatikana
maji kutoka saa tano za sasa kwa siku hadi saa 24 kwa siku.
No comments:
Post a Comment