Habari za Punde

Dk Shein Atembelea Kituo cha Damu Salama Amaan.

STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
  Zanzibar                                                                                                           30.10.2014
---
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amefanya ziara fupi ya kutembelea Kituo cha Damu Salama kiliopo Sebleni mjini Unguja pamoja na kutembelea Maabara ya Uchunguzi wa Maradhi katika hospitali Kuu ya Mnazi Mmoja na kupongeza hatua zilizofikiwa huku akieleza azma ya serikali katika kuviimarisha vitengo hivyo.

Dk. Shein alianza ziara yake katika Kituo cha Damu Salama kiliopo Sebleni mjini Unguja na kujionea kazi zinazofanywa katika kituo hicho pamoja na kupata maelezo kutoka kwa wataalamu mbali mbali wa kituoni hapo wakiongozwa na Dk. Mwanakheir Ahmed Mahmoud.

Mara baada ya kutembelea vitengo vilivyomo ndani ya kituo hicho, Dk. Shein alizungumza na wafanyakazi wa kituo hicho na kuwaeleza jinsi alivyofarajika na huduma zinazoendeshwa kituoni hapo ambazo zina umuhimu mkubwa  katika maisha ya jamii.

Katika maelezo yake Dk. Shein alieleza umuhimu wa kuchangia damu na kusisitiza kuwa bila ya kuchangia damu hakuna damu itakayopatikana, hivyo suala la kuchangia damu ili kuweza kukiimarisha kituo hicho ni jambo la msingi na linaumuhimu wake mkubwa ndani ya jamii.

Akizungumzia kuhusu suala zima la uhamasishaji juu ya kuchangia damu kwa lengo la kukiimarisha kituo hicho kama kinavyofahamika pia kuwa ni benki ya damu ni jambo muwafaka kwani ni jambo la nchi nzima kama ilivyo kwa uhamasishaji juu ya maambukizi ya UKIMWI.

Alisisitiza kuwa jambo la muhimu ni kuwekwa  maandalizi na mikakati endelevu ili kufikia lengo lililokusudiwa huku akisisitiza kuwahaheshimu sambamba na kuwapongeza wale wote wanaochangia damu kwani wamekuwa wakifanya jambo kubwa katika uhai wa mwanaadamu.

Aidha, Dk. Shein aliueleza uongozi pamoja na wafanyakazi wa Kituo hicho kuwa ataendelea kushirikiana na uongozi wa Wizara ya Afya ili kukiimarisha kituo hicho ili kiweze kupata mafanikio zaidi.

Nao, wafanyakazi wa Kituo hicho walimueleza Dk. Shein mafanikio yaliopatikana sambamba na changamoto zilizopo huku wakisisitiza  na kuwataka wananchi pamoja na viongozi wa ngazi zote kuwahamasisha wananchi juu ya umuhimu wa kuchangia damu.

Pamoja na hayo, wafanyakazi hao walimueleza Dk. Shein umuhimu wa kituo hicho kuunganishwa na maabara ya hospitali Kuu ya Mnazi mmoja  pamoja na  hospitali kuu za Chake, Wete na Mkoani Pemba ili kurahisisha utoaji huduma wa damu kwa wagonjwa.

Wakati huo huo, Dk. Shein alitembelea Maabara ya Uchunguzi wa Maradhi iliopo katika Hospitali Kuu ya Mnazimmoja na kujionea huduma mbali mbali za maabara zinazofanywa katika  Maabara hiyo pamoja na kupata maelezo ya kina juu ya kazi hizo kitaalamu.

Nao, wataalamu wa  kituo hicho chini ya  Mkuu wao Dk. Msafiri Marijani walimueleza Dk. Shein kuwa hivi sasa kituo hicho kimeweza kupiga hatua kubwa na kuweza kupata mashirikiano makubwa na hospitali ziliopo nje ya nchi hatua ambayo imepelekea hadi madaktari wanafunzi kutoka nje kama vile Hospitali ya Haukland ya Norway kufanya uchunguzi kupitia maabara hiyo.

Mara baada ya ziara yake hiyo, Dk. Shein akizungumza na wafanyakazi wa  Maabara hiyo ambayo yeye mwenyewe ni muasisi aliwaeleza wafanyakazi hao kuwa amefarajika na hatua iliyofikiwa hivi sasa katika Maabara ikilinganishwa na pale ilipoanzishwa.

“Nilipoondoka maabara  hii haikuwa hivi, mabadiliko makubwa yamefanyika...hongereni sana”,alisema Dk. Shein.

Katika maelezo yake Dk. Shein alisema kuwa huduma za hospitali haziendi bila ya kuwepo Maabara kwani Maabara ndiko kunakofanyiwa uchunguzi wa kutambulikana maradhi ya mgonjwa.

Dk. Shein alisema kuwa hatua hiyo ni kubwa na itambuliwe kuwa hizo ni juhudi za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar pamoja na Wafadhili mbali mbali waliyoiunga mkono Serikali katika kuiimarisha Maabara hiyo.

Aidha, Dk. Shein alisisitiza kuwa Sera ya Afya bado ni kuwa matibabu bure na kueleza haja kwa wananchi kuelimishwa namna ya kuchangia huduma hizo za afya hasa ikizingatiwa ongezeko kubwa la idadi ya watu hapa Zanzibar  hivi sasa ikilinganishwa na mara baada ya Mapinduzi ya mwaka 1964 wakati ilipotangaziwa huduma za afya.

Nao wataalamu wa kitengo hicho walimueleza Dk. Shein changamoto zilizopo huku uongozi wa  Wizara hiyo ukitoa pongezi kwa Dk. Shein kufuatia ziara yake hiyo.
Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.