Habari za Punde

Pato la taifa lafikia 26.8tr/-

Na Mwanajuma Abdi, Dar es Salaam
Waziri wa Fedha, Saada Mkuya Salum, amesema  pato la taifa la bei za bidhaa na huduma limekua hadi kufikia shilingi trilioni 26.8 kwa mwaka 2007 ikilinganishwa na shilingi trilioni 20.9 mwaka 2001.

Hayo aliyasema jana wakati akizindua usambaji wa takwimu za pato la taifa zilizorekebishwa kwa mwaka wa 2007 Tanzania Bara, uzinduzi ambao ulifanyika ukumbi wa Karimjee, Dar es Salaam.

Alisema takwimu hizo zitatumika katika bajeti kuu ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano Tanzania ya mwaka 2015-2016.

Alisema ukuaji huo ni sawa na ongezeko la ukubwa wa pato la taifa kwa kiasi cha asilimia 27.8 ambapo ni wastani wa pato la mwananchi kwa mwaka 2013 kwa kutumia takwimu zilizorekebishwa ni shilingi 1,561,050, ambazo ni sawa na dola za Marekani 977 ikilinganishwa na shilingi 1,186,200 kwa kutumia takwimu za pato la taifa za bei kwa mwaka 2001.


Alisema ukubwa wa pato hilo ni juhudi za serikali za kutengeneza fursa kwa wananchi za kukuza uchumi wa mwananchi mmoja mmoja, ambapo alisisitiza kwamba kuongezeka kwa pato la taifa haina maana kuwa Serikali ina uwezo wa kuwajaza wananchi fedha mifukoni mwao bila ya wao kufanya kazi.

Alisema kwa mujibu wa sensa ya watu na makazi ya mwaka 2012 zaidi ya asilimia 63 ya wananchi wa Tanzania Bara wanamiliki simu za kiganjani, hivyo ukuaji wa sayansi na teknologia umetoa fursa kwa wananchi kujiongezea kipato kutokana kurahisisha mawasiliano.

Aidha alifahamisha kuwa, kuongezeka thamani ya pato la Taifa kunaiongezea Serikali uwezo wa kimapato kupitia kodi, hivyo inasaidia kugharamia ujenzi wa miundombinu na utoaji wa huduma mbali mbali za wananchi ikiwemo ujenzi wa barabara, huduma za maji safi na salama ambapo zaidi ya asilimia 60 ya kaya zote nchini zinapata huduma.

Alisema hayo ni baadhi ya matokeo na fursa ya ukuaji wa uchumi ambao umepelekea umasikini wa kipato kupungua kutoka asilimia 35 mwaka 2007 hadi kufikia asilimia 28.2 mwaka 2012.

Mapema Mkurugenzi Mkuu wa Ofisi ya Taifa ya Takwimu, Dk. Albina Chuwa, alisema kazi za marekebisho ya takwimu za pato la Taifa kwa Tanzania Bara imetumia tafiti za taifa zilizofanyika kwa kipindi cha mwaka 2001 hadi mwaka 2007.

Alisema takwimu hizo  ni pamoja na utafiti wa mapato ya matumizi ya kaya, sensa ya kilimo iliyofanyika mwaka 2008 na takwimu nyengine za utawala kutoka wizara na idara za serikali.

Akitoa shukurani, Naibu Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania, Juma Reli, alipongeza uzinduzi akisema huo ni muhimu katika kukuza maendeleo ya uchumi wa taifa sambamba na kuishukuru Benki ya Dunia na IMF kwa kusaidia mafunzo ya marekebisho hayo.

Uzinduzi kama huo utafanyika Januari mwakani  Zanzibar.

1 comment:

  1. wewe zitangazie tu, mpaka wajanja waje kuzichota

    ReplyDelete

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.