Habari za Punde

SUZA kuongeza kozi tano shahada ya kwanza

Na Juma Khamis
Chuo Kikuu cha Taifa cha Zanzibar (SUZA) kinatarajia kuanzisha skuli nyengine tano kikianzia na mwaka wa masomo 2015/2016.

Akitoa muhtasari wa mipango ya baadae ya chuo hicho kwa wajumbe wa Baraza la Ushauri la chuo hicho jana, Naibu Makamu Mkuu wa chuo hicho (Fedha, Utawala), Dk. Zakia Aboubakary, alisema skuli hizo ni pamoja na skuli ya Kompyuta, 

Mawasiliano  na Habari (SCCM) itakayoanza mwaka ujao wa masomo.

Alisema skuli nyengine ni Uhandisi wa mafuta, Biashara, Utalii na Kilimo.

Hata hivyo, uanzishwaji wa skuli hizo mpya unakabiliwa na changamoto kubwa ikiwemo ufinyu wa miundombinu hasa majengo na kwamba chuo kinahitaji dola za Marekani milioni 64 kumaliza changamoto za miundombinu.

Wakati huo huo, Naibu  Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais, Dk. Islam Seif, amekitaka Chuo hicho, kupeleka matokeo ya utafiti zinazofanywa kwa wananchi.

Alisema hayo kampasi ya SUZA Vuga katika maonesho ya utafiti, yanayokwenda sambamba na maadhimisho ya mahafali ya 10 ya chuo hicho, yanayotarajiwa kufanyika Disemba 20.

Alisema utafiti ndio unaoweza kuleta mageuzi ya kiuchumi na kijamii na kuwataka wanafunzi na wasomi kujikita katika kufanya tafiti zitakazojibu changamoto zinazowakabili wananchi.

Alikipongeza chuo hicho kwa juhudi inazochukua katika kufundisha na kufanya tafiti na kwamba kimejibu kilio cha muda mrefu cha Zanzibar kukosa chuo kikuu chake cha taifa.

Mapema Makamu Mkuu wa SUZA, Prof. Idris Rai, alisema chuo kitaendelea kutoa mchango wake katika kusaidia maendeleo ya taifa na jamii.

Maonesho hayo yalivutia idadi kubwa ya wanafunzi na wananchi yaliyonesha tafiti mbali mbali zilizofanywa na chuo hicho hasa katika masuala ya sayansi ya mazingira na bahari.

Kwa upande mwengine  SUZA kimetiliana saini ya mkataba wa maelewano (MoU) na Chuo Kikuu cha Sayansi ya Viumbe (NMBU) cha Norway.


Hafla ya utiaji saini hiyo ilifanyika kampasi ya SUZA Vuga ambapo Makamu Mkuu wa SUZA, Prof. Idris Rai, alisaini kwa niaba ya chuo chake na Mkuu wa Idara ya Sayansi ya Mazingira na Teknolojia wa NMBU, Prof. Oystein Johnsen, alisaini kwa niaba ya chuo hicho.

Akizungumza katika hafla hiyo, Prof. Rai alisema SUZA inaendelea kuimarisha ushirikiano na vyuo vikuu mbali mbali duniani na vimefika vyuo vikuu 32.


Alisema kwa kuwa SUZA ni chuo kichanga kitaendelea kujifunza kutoka kwa vyuo vyenye uzoefu kikiwemo chuo hicho na kusema ni matarajio ya chuo kwamba ushirikiano huo utadumu kwa muda mrefu. 

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.