Habari za Punde

Rais Shein Akutana na Waziri wa Mambo ya Nje wa Jamhuri ya Kiislam ya Iran.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein  akisalimiana na Waziri wa Mambo ya Nje wa Jamhuri ya  Kiislamu ya Iran Mohammed Javad  Zarif alipofika Ikulu Mjini Zanzibar leo akiwa na ujumbe aliofuatana nao
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein (kulia)  akizungumza na  Waziri wa Mambo ya Nje wa Jamhuri ya  Kiislamu ya Iran Mohammed Javad  Zarif (wa pili kulia) alipofika Ikulu Mjini Zanzibar leo akiwa na ujumbe aliofuatana nao
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein (katikati)  akizungumza na  Waziri wa Mambo ya Nje wa Jamhuri ya  Kiislamu ya Iran Mohammed Javad  Zarif (kulia kwa Rais ) alipofika Ikulu Mjini Zanzibar leo akiwa na ujumbe aliofuatana nao,[Picha na Ikulu.]

STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
  Zanzibar                                                                                                                                 5.2.2015
---
SERIKALI ya Mapinduzi ya Zanzibar imeeleza azma yake ya kuendelea kuimarisha uhusiano na ushirikiano wa kihistoria kati yake na Jamhuri ya Kiislamu ya Iran ambayo inaiunga mkono Zanzibar katika kuimarisha sekta mbali mbali za maendeleo.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein aliyasema hayo leo wakati alipofanya mazungumzo na Waziri wa Mambo ya Nje wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran, Mheshimiwa Javad Zarif, Ikulu mjini Zanzibar.

Katika mazungumzo hayo, Dk. Shein alisema kuwa Zanzibar ina mengi ya kujifunza kutoka kwa ndugu zao wa Iran na kutoa pongezi  kwa nchi hiyo kwa kuendelea kuiunga mkono Zanzibar katika sekta za maendeleo ikiwemo sekta ya elimu, afya na nyenginezo.

Dk. Shein alieleza kuwa Zanzibar inathamini uhusiano na ushirikiano wa kihistoria kati ya nchi bili hizo na kusisitiza kuwa nchi hiyo imekuwa ikitoa ushirikiano mkubwa katika sekta ya elimu kwa kutoa nafasi za mafunzo kwa vijana wa Zanzibar kwenda kusoma nchini humo.

Alisema kuwa Zanzibar imekuwa na mabadiliko makubwa ya kimaendeleo hivyo kuimarishwa kwa uhusiano kati yake na Iran  kutazidi kukuza maendeleo hayo hasa katika sekta ya kilimo mafunzo ya ufundi na afya ambapo Iran imeahidi kuiunga mkono Zanzibar.


Dk. Shein alisema kuwa katika sekta ya kilimo, hatua kubwa zinazochukuliwa hivi sasa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ni kuimarisha Chuo chake cha utafiti ili kuweza kufanya tafiti mbali mbali za kilimo hasa tafiti za mbegu bora, hivyo hatua hiyo ya Iran itasaidia kukuza sekta ya kilimo hapa nchini.

Aidha, Dk. Shein alisema kuwa mbali na hatua hiyo, Serikali ya Mapinduzi Zanzibar imekuwa ikifanya juhudi kubwa katika kuimarisha kilimo cha umwagiliaji maji ikiwa na lengo la kuhakikisha Zanzibar inazalisha kiwango kikubwa cha chakula ili kupunguza uagiziaji mkubwa wa chakula kutoka nje ya nchi.

Kwa upande wa sekta ya kilimo, Dk. Shein alitoa shukurani zake kwa ahadi za Serikali ya Iran ya kuisaidia Zanzibar vifaa ambavyo vitaingia nchini hivi karibuni, kwa ajili ya uimarishaji wa Vyuo vyake vya Amali vya Unguja na Pemba kwa lengo la kuinua sekta hiyo na hatimae kuwasaidia vijana katika kukabiliana na soko la ajira.

Pamoja na hayo, Dk. Shein alisema kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imekuwa ikitilia mkazo kwa kiasi kikubwa na tayari imeweka mikakati yake katika uimarishaji wa sekta ya uvuvi hasa ule wa bahari kuu.

Kutokana na hatua hiyo, Serikali ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran ina nafasi nzuri ya kuiunga mkono Zanzibar katika juhudi hizo hasa ikizingatiwa kuwa nchi hiyo imepiga hatua kubwa katika sekta ya uvuvi.

Akizungumzia juhudi za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuimarisha sekta ya afya, Dk. Shein alisema kuwa tayari hatua nzuri za matibabu ya maradhi yakiwemo upasuaji wa maradhi ya ubongo na uti wa mgongo zimeshafikiwa hapa Zanzibar huku juhudi zikiendelea za kuhakikisha maradhi ya mfumo wa utoaji wa haja ndogo nao tiba yake inaendelea kupatikana hapa nchini.

Kwa kuzingatia hilo, Dk. Shein alisema kuwa hivi sasa Serikali kupitia Wizara ya Afya imo katika mikakati ya kuhakikisha tiba ya maradhi ya Saratani pamoja na maradhi ya Ini nayo inapatikana hapa Zanzibar, juhudi ambazo zinahitaji kuungwa mkono na nchi wahisani pamoja na washirikika wa maendeleo ikiwemo Iran.

Alisema kuwa tayari Serikali imeshawapeleka vijana nchini Norway pamoja na Tanzania Bara kwa ajili ya kujifunza juu ya maradhi ya Saratani na kueleza kuwa kwa matibabu hayo hapa Zanzibar kutaipunguzia Serikali gharama kubwa za fedha inazotoa kwa ajili ya wagonjwa ambao huwapeleka nchini India ama Afrika ya Kusini.

Nae Waziri wa Mambo ya Nje wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran, Mheshimiwa Javad Zarif aliupongeza uhusiano na ushirikiano wa kihistoria uliopo kati ya nchi hiyo na Zanzibar na kusisitiza kuwa ziara yake ni miongoni mwa hatua za kukuza uhusiano huo.

Waziri Zarif alimueleza Dk. Shein kuwa Iran itaendelea kuiunga mkono Zanzibar katika kuimarisha sekta za maendeleo zikiwemo elimu, afya, uvuvi, kilimo na nyenginezo huku akisisitiza haja ya kukuza mahusiano kati ya Wizara ya Kilimo ya Zanzibar na ile ya Iran kwa lengo la kuinua sekta hiyo kwa pande zote mbili.

Pamoja na hayo, Waziri huyo alimuhakikishia Dk. Shein kuwa Serikali ya Iran itahakikisha inaendelea kuiunga mkono Elimu ya Vyuo vya Amali na kuahidi kusaidia vifaa kwa ajili ya vyuo hivyo ambavyo vitawasili hivi karibuni kutokea nchini humo.

Aidha, Waziri Zarif aliahidi kukuza ushirikiano na Zanzibar katika kuimarisha sekta ya  utamaduni na kuahidi kuwa Jumuiya inayohusiana na Urithi wa Utamaduni ya Iran itakuja Zanzibar kwa lengo la kukuza uhusiano.
Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.