Habari za Punde

Naibu Waziri wa Afya Zanzibar Mhe Mahmoud Akabidhi Pikipiki 10 kwa Maafisa wa Afya wa Wilaya.

Na Faki Mjaka-Maelezo Zanzibar.
Jumla ya Pikipiki 10 zenye thamani ya Shl.Million 42 zimegawiwa kwa Maafisa 10 wa Afya wa Wilaya za Unguja na Pemba.

Pikipiki hizo ni Msaada kutoka Shirika la Watu wa Marekani USAID kupitia Taasisi ya JSI wenye lengo la kusaidia Sekta ya Afya Zanzibar.

 Akikabidhi Pikipiki hizo Naibu Waziri wa Afya Zanzibar Mahmoud Thabit Kombo amewataka Maafisa Waliokabidhiwa kuzitumia vyema ili kutimiza lengo lililokusudiwa.

Amesema ana imani kubwa kuwa zitasaidia kwa kiasi kikubwa Usimamizi na usambazaji mzuri wa Dawa katika kila Wilaya ya Zanzibar.

 "Kwa kweli pamoja na kuwashukuru Wahisani wetu USAID na JSI tunaamini sasa Usimamizi na Usambazaji wa Dawa utakuwa bora na kwa wakati maana Pikipiki hizo ni usafiri wa Rahisi" Alisema Naibu Mahmoud.

Amewataka Maafisa hao kutoishia kusambaza Dawa tu bali wapitie kila kituo cha Afya kutafuta Matatizo na kuyaripoti Sehemu husika ili yaweze kushughulikiwa.

Aidha Naibu Mahmoud amewashauri Viongozi wa Wizara ya Afya kutoa Motisha kwa Watendaji wanaoweza kukabidhiwa Vitendea kazi na kuvitunza vyema.

 Kwa upande wao Maafisa waliokabidhiwa Pikipiki hizo wameishukuru Serikali kwa Juhudi zake za kutafuta mbinu mbali mbali za kukabiliana na Changamoto na kuzifanyia kazi.

Mmoja wa Maafisa hao Mayasa Othman Shariff kutoka Wilaya ya Chake Chake amesema Pikipiki hizo zitawarahisishia kazi zao ikiwa ni pamoja na kusambaza na kusimamia Dawa sambamba na kupeleka Ripoti mbali mbali sehemu husika.

 Awali akimkaribisha Mgeni Rasmi, Mfamasia Mkuu Dkt. Habib Ali Shariff alisema miongoni mwa Changamoto zinazokabili Sekta ya Afya ni pamoja na Usimamizi mbaya wa Dawa hivyo Pikipiki hizo zitasaidia kupambana na Changamoto hiyo.

 Hafla ya Kukabidhiwa Pikipiki hizo ilifanyika katika Viwanja vya Bohari kuu ya Madawa Maruhubi Zanzibar ambapo Wilaya zote 10 za Unguja na Pemba zilipatiwa Pikipiki moja na kukabidhiwa Maafisa wa Afya wa Wilaya husika.

 Wizara ya Afya imekuwa ikifanya Juhudi mbali mbali za kukabiliana na Changamoto za Sekta ya Afya Zanzibar ikiwa ni pamoja na kutafuta Wafadhili kutoka Nchi tofauti ambapo Shirika la Watu wa Marekani USAID ni mdau muhimu wa kusaidia Sekta hiyo Zanzibar.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.