Habari za Punde

Dk Shein Afunga Mkutano wake wa Kampeni Pemba

Na Mwandishi Wetu Pemba.

Makamu Mwenyekiti wa CCM Zanzibar na Rais wa  Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein  amemuunga mkono Rais wa Jamhuri ya Muungao Dk. Jakaya Mrisho Kikwete kwa kuwathibitishia wananchi na wanaCCM kuondoa shaka na hofu kwani Serikali yao ipo na itaendelea kuwalinda siku ya uchaguzi Mkuu wa mwaka huu.

Dk. Shein ambaye ni Mgombea nafasi ya Urais wa Zanzibar kwa tiketi ya CCM aliyasema hayo katika hotuba yake aliyoitoa kwenye mkutano wa kufunga Kampeni ya chama hicho uliofanyika huko katika viwanja vya Gombani ya Kale, Chake Chake, Pemba uliohudhuriwa na maelfu ya wananchi na wanaCCM.

Dk. Shein alitoa shukurani kwa wanaCCM na wananchi kwa kuhudhuria kwa wingi katika mikutano yote tokea tarehe 13 mwezi huu zilipozinduliwa Kampeni za chama hicho.

Alisema kuwa katika mikutano hiyo ahadi kwa kila Jimbo, Wilaya hadi Wadi zilitolewa kwa mujibu wa utekelezaji wa Ilani ya CCM pamoja na kuelezea mambo makubwa kwa Zanzibar.

Alisema kuwa katika miaka mitano ijayo baada ya kuchaguliwa yeye na chama chake atayatekeleza yale yote yalioahidiwa na chama chake.

Dk. Shein aliahidi kutokana na Ilani ya chama hicho kuendeleza kusimamia  amani, utulivu na umoja kwani ndio njia pekee ya kuleta maendeleo.

"Anaezania ni zihaka na anataka kufanya fujo ajaribu aone",alisema Dk. Shein.


Akilizungumzia suala la karafuu, Dk. Shein alisema kuwa Ilaini ya CCM kama iluvyoelekeza mwaka 2010, Serikali ya SMZ italiendeleza zao la karafuu na halitobinafsishwa na kuwataka wananchi wa Pemba wasikubali kurejeshwa nyuma kwani wanapata asilimia 80 ya soko la dunia la karafuu zao wanazoziuza na Serikali italiendeleza zao hilo.

Alirejea ahadi yake ya kuwa endapo bei ya zao hilo itaendelea kuwa hivyo hivyo katika soko la dunia bei ya karafuu ataiongeza hadi kufikia kilo elfu 20,  badala ya elfu 14 ya bei ya sasa.

Alisema kuwa alitangaza kuwa siku ya tarehe 12 Januari mwaka huu, kuwa atafuta michango yote ya elimu ya msingi kuanzia Julai mwaka huu na katika Kampeni hizi alisema kuwa mitihani ya kidatu cha nne na Sita nazo ameamua wazee wasichangie atakapoingia madarakani.

Pia, arijea kauli yake kuwa mwaka wake wa mwanzo ataondoa michango ya Sekondari na kueleza kuwa  mwaka wa Pili katika uongozi wake atatangaza huduma za afya bure na kusema kuwa afya na elimu itakuwa bure kama alivyoasisi Mzee Karume kwani uwezo upo.

Dk. Shein baada ya kusema hayo alishangazwa na vyama vya upinzani kuhemkwa na kuiga kwa kila analoliahidi.

Alisema kuwa lengo la Serikali ni kuimarisha zaidi huduma za maji safi na salama ambazo kwa sasa ni alisilimia 87.7, kwa mijini na alisimia 70 vijiji, na kueleza lengo ni kufikia asilimia 97 mijini na  80 kwa vijiji na hilo linawezekana.

Aidha, Dk. Shein alieleza jinsi alivyojiandaa na suala la ajira kwa vijana sambamba na mikakati ya ujenzi wa vyuo vya amali kikiwemo kitakachojengwa huko Mtambwe kwa Pemba na Makunduchi kwa Unguja.

Pamoja na hayo, alisema kuwa Unguja na Pemba ni visiwa vilivyozungukwa na bahari na asilimia ya watu wake wengi ni wavuvi na kusema kuwa Serikali atakayoiongoza itaimarisha uvuvi wa bahari kuu kwa mashirikiano ya  Serikali mbili kwa nguvu zote ili kuitumia bahari kuu kwa kuweka miradi ikiwa ni pamoja na kuwakaribisha wawekezaji ili itoe tija ambapo Makao Makuu yake hivi sasa yapo Fumba Zanzibar.

Dk. Shein, aliwataka wana CCM na wananchi kuwachagua viongozi wa CCM, Pia, Dk. Shein alitumia fursa hiyo kutoa shukurani kwa Dk. Jakaya Mrisho Kikwete kwa mashirikiano makubwa aliyompa tokea wakiwa wote Mawaziri sambamba na kuusimamia Muungano katika kipindi chake chote cha urais.

Dk. Shein alisema kuwa Dk. Kikwete ametoa mchango mkubwa sana katika kuendeleza suala la mafuta na gesi kwa upande wa Zanzibar na kuwataka wananchi na WanaCCM kwenda kupiga kura kwa lengo la kuyalinda Mapinduzi pamoja na Muungano wa Tanganyika na Zanzibar.

Alisema kuwa yuko tayari kuiongoza Zanzibar na afya yake inamruhusu na kusisitiza kuwa mafanikio yote tokea 1964  yamefanywa kwa pamoja na kuwaeleza kuwa bila ya CCM yote hayo yasingelipatikana huku akiwaeleza wananchi kuwa  viongozi wa upinzani hawana vipaji vya kuongoza.

Nae Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mwenyekiti wa CCM Tanzania Dk. Jakaya Mrisho Kikwete alisema kuwa CCM itaendelea kuongoza Jamhuri ya Tanzania na pamoja na Zanzibar na kuwaombea kura wagombea wote wa CCM.

Aliwataka wananchi na wanaCCM kukichagua chama hicho kwani kimeongoza vizuri kwani nchi iko salama na imetulia na watu wanafanya shughuli zao bila ya bughuza na kueleza kuwa kama ingeongozwa vibaya hatua hiyo isingelifikia.

Alisema kuwa kuna kila sababu ya kumchagua Dk. Shein kuwa Rais wa Zanzibar kwani Zanzibar iko salama na ameiongoza kwa umakini sana na kwa upande wa Serikali ya Umoja wa Kitaifa Dk. Shein amekuwa makini katika serikali hiyo na kama si umakini wake hata miaka mitano isingelimaliza.

Alisema kuwa ameongoza kwa umakini Serikali hiyo na kusisitiza kuwa maendeleo yapo yanatyoonekana katika kila nyanja kwenye sekta zote na hata kwenye vipato vya watu.

Rais Kikwete alisisitiza kuwa hakuna mbadala wa Dk. Shein, na Maalim Seif si mbadala wa Dk. Shein kwani Maalim Seif angezoza Serikali hiyo hata siku tatu zisingefika kwani si mstahamilivu.
Alisema kuwa kiongozi huyo wa upinzania katika lugha zake anazozungumza haunganishi watu badala yake anawachonganisha na kusisitiza kuwa Dk. Shein ndio anaeweza kufanya kazi ya urais wa Zanzibar.

Rais Kikwete aliwataka wananchi na wanaCCM wamchague Dk. Shein pamoja na Wawakilishi, Wabunge na Madiwani wengi wa CCM ili aweze kuongoza vizuri, na wengine waendelee kuwa washiriki.

Alisema kuwa kwa upande wa mgombe nafasi ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa tiketi ya CCM, John Pombe Magufuli,  hilo ndio chaguo la wengi na kueleza kuwa wapinzani wake hivi sasa wamekalia kuti kavu na kuwataka wananchi wakitaka mambo mazuri kwa kuitaka Zanzibar na Tanzania kwa jumla ziendelee kustawi na kuwa na maendeleo wawachague Dk. Shein na Magufuli.

Alieleza kuwa CCM katika kumteua John Magufuli  haikufanya kosa kwani ni muadilifu kwani angekuwa na tatizo lolote la uadilifu asingelipata nafasi hiyo.

Alisema kuwa Dk. Magufuli ni hodari, muaminifu, muadilifu na wanaomsema vibaya ni wale waliojaa hofu katika maisha yao ya ujanja ujanja.

Alisema kuwa katika Wizara zote alizofanya kazi Magufuli,amethibitisha ukomavu wake pamoja na ujasiri na mvumilivu wake sambamba na hayo ni muumini wa  Muungano wa Tanzania na mpenda maendeleo kwani katika hotuba zake anaonesha jinsi anavyokereketwa na maendeleo na iwapo atapewa nafasi hiyo mafanikio makubwa yatapatikana Tanzania.

Dk. Kikwete alisema kuwa Magufuli anaamini umoja na tokea ameanza Kampeni zake hajajinadi juu ya dini yake wala ukabila wake na kusema kuwa Tanzania inataka kiongozi anaesema mamenao yake akayaamini yeye mwenyewe.

Alisisitiza kuwa uchaguzi utakuwa wa amani, na kueleza kuwa anaetayaarisha matayarisho ya Uchaguzi ni Tume ya Uchaguzi, na Serikali kazi yake ni kuwapa fedha kwa ajili ya shughuli zao lakini kuhakikisha kuna amani na utulivu siku ya kupiga kura ni jukumu la Serikali na yeye ndio amiri Jeshi Mkuu.

"Tutahakikisha kuwa uchaguzi utakuwa wa amani na utulivu na anayetaka kufanya majaribio ya utayari wetu na ajaribu, natakata Watanzania wapate fursa ya kuwachagua viongozi wanaotaka",alisema Dk. Kikwete.

"Tarehe 25 jitokezeni hakutatokea lolote...kuungana kwa vyama vinne ndio kuonesha dalili za kushindwa"alisema Rais Kikwete.

Aliwataka wanaCCM na wananchi kujitokeza kwenda kupiga kura na hakutatokea lolote na atakae jaribu ataona na kutumia fursa hiyo kuwaombea kura kutaka kupewa kura Dk. Shein, Dk. Magufuli, Samia, Wabunge, Wawakilishi na Madiwani.

Nae Mgombe Mwenza wa Urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, akitoa salamu za ndugu zao wa Tanzania Bara alisema kuwa wao wanasema kuwa CCM mbele kwa mbele na kusema kuwa Pemba ya 2010  si ya leo.

Alisema kuwa CCM mwaka huu wameamua kutimiza nembo ya Serikali ya Adama na Hawa na kusema kuwa Adama na Hawa ni Magufuli na Samia na wako yatayari kukabidhiwa Tanzania na mali asili zake kwa lengo la kuitumikia.

Aliwakataka akina mama bila ya kujali vyama vyao wapige kura CCM kwa sababu CCM imeamua mwaka huu kumpa heshima kubwa mwanamke kuwa Mgombea Mwenza.

Aliwataka akina mama kukamatana na kuuonesha ulimwengu kuwa wanawake wakipewa nafasi wanaweza kuiongoza Tanzania.

Aliishukuru amwamu ya nne ya Urais wa Dk. Kikwete kwa kujenga miundombinu kwa kutoa fursa kwa ajira na kusema kuwa Tanzania nzima imeunganishwa kwa barabara za lami na kueleza kuwa zikitoa huduma na kuwawezesha wananchi kusafirisha bidhaa zao, sambamba na kuinuka  kwa soko la ajira.

Alisema kuwa Ilani ya CCM imeonesha jinsi vijana wa wanawake walivyopewa kipaumbele ili kuweza kupata fursa na kueleza kwa upande wa walemavu nao watapewa nafasi bila ya ubaguzi.

Kwa upande wa wazee alisema kuwa, wazee wote ambao walikuwa wakulima na hawapati mafao watapewa sawa na wale waliokuwa wakifanya kazi Serikalini ambapo tayari kwa upande wa Zanzibar mchakato huo umeanza.

Alisema mkuwa CCM ina mpango kazi kwa yale yote ambayo yatafanywa katika awamu na kuonesha kuwa rasilimali fedha za kuendeleza ahadi hizo zitapatikana.

Alisema kuwa CCM ina mfumo na muuundo unaoelekewaka na kusisitiza kuwa mchakato ulioendeshwa katika chama hicho hadi kupatikanwa kwa wagombea na tofauti na jinsi walivyopatikana wagombea katika vyama vyengine vya siasa ambao ni wasanii na kusisitiza kuwa wapewe kura CCM wenye uzoefu wa kuongoza.

Samia alisema kuwa katika kuendesha Serikali hawezi kupewa mtu ambae sifa zake hazina uwezo, alisema kuwa CCM ina lengo la kulinda na kudumisha Mapinduzi na Muuungano wa Jamhuri ya Tanzania.

Mgombea huyo Mwenza wa CCM alisema kuwa ili walinde usalama wa Tanzania pamoja na kulinda Muungano na kwa umoja watu waweze kuishi kwa kusikilizana na kupendana. "Watanzania hawako tayari kuwapa kura wasanii"alisema Samia.

Mapema Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Idd akitoa salamu kwa wananchi aliwataka wajiandae kwa ushindi wakiwemo akina mama kwa kupaka hina na kutia wanja kusubiri ushindi wa CCM.

Alisema kuwa chama cha CUF katika uchaguzi wa mwaka huu kitashindwa na Katibu Mkuu wake utakuwa ndio mwaka wake wa mwisho wa siasa kama alivyoeleza mwenyewe aliposema kuwa hata Ukatibu Mkuu wa chama hicho anauwacha.

Alisema kuwa viongozi wa CUF wamekuwa wakiwadanganya sana wananchi na kuendedelea kueleza kuwa wafuasi wa chama hicho wamejiandaa kuleta vurugu na wamejiandaa kuleta mamluki kutoka nchi jirani kwa lengo la kuja kufanya vurugu kisiwani humo.

Kwa upande wa Unguja alisema kuwa tayari Serikali imeshapata taarifa kuwa kuna watu wamejificha kwenye nyumba ya kiongozi mmoja wa chama hicho huko Mombasa Unguja kwa lengo la kuja kufanya fujo siku ya uchaguzi na kusema kuwa hawatahi kufanya kwani taarifa zipo na watashughulikiwa na vyombo husika.

Aliwataka wanaCCM na wananchi kutoogopa kwenda kupiga kura kwani ulinzi utawekwa kila mahala ili kuhakikisha kila mtu mwenye haki ya kupiga kura anapiga kura kwa kupata haki yake hiyo ya msingi.

Balozi Seif alisema kuwa matusi anayotukanwa na viongozi wa CUF jibu lake ni siku ya tarehe 25 siku ya kupiga kura. Aidha, Balozi Seif alisema kuwa wenye familia ya Marehemu Mzee Karume hawataki kubandikwa picha zilizowekwa na CUF zinazomuonesha Maalim Seif na Marehemu Mzee Abeid Karume zikimuonesha Maalim Seif akisema kuwa atavaa viatu vya muasisi huyo.

Nae Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Vuai Ali Vuai alitoa shukurani kwa washiriki na jamii yote waliotoa misaada yao mbali mbali katika Kampeni hiyo  kwa  chama hicho kutokana na mashirikiano makubwa waliyoyatoa wananchi, wanaCCM, wasanii, waandishi wa habari na wengineo.

Vuai alisema kuwa Dk. Shein hana ubaguzi, hana choyo na muumini wa CCM ameweza kuwaunganisha wananchi wa Zanzibar, huku akimpongeza Dk. Jakaya Marisho Kikwete alimpongeza kwa kusimamia vyema kuondokana na migogoro ya Zanzibar.

Naibu Katibu Mkuu huyo, aliwataka wanaCCM kutochokozeka kwani wafuasi wa chama cha CUF wameamua kwa makusudi kufanya vurugu kwani wameshajua kuwa watashindwa katika uchaguzi mkuu wa mwaka huu.

Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Kaskazini Pemba, Mberwa Hamad aliwaeleza wanaCCM kuwa ushindi kwa chama hicho hauepukiki katika uchaguzi wa mwaka huu hivyo aliwaondoa hofu na kuwataka kwenda kuwachagua viongozi wa CCM siku ya Jumaapili ya tarehe 25, Oktoba mwaka huu.


No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.