Habari za Punde

Dk Shein Aweka Jiwe la Msingi Maskani Mpya ya Ukombozi wa Vijana Muyuni.

Na Mwandishi Wetu,

MAKAMU Mwenyekiti wa CCM Zanzibar Dk. Ali Mohamed Shein ameweka jiwe la msingi katika Maskani mpya ya Ukombozi wa Vijana iliyopo Muyuni na kusema kuwa Maskani ni sehemu ya kujenga umoja na mshikamano huku akieleza kuwa CCM itaendelea kuwa namba moja katika kuongoza na kuleta maendeleo hapa nchini.

Dk. Shein ambaye pia, ni Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi aliyasema hayo mara baada ya kuweka jiwe la msingi katika Maskani hiyo iliyopo Muyuni, Jimbo la Makunduchi Mkoa wa Kusini Unguja na kusema kuwa CCM haina mbadala.

Katika maelezo yake Dk. Shein alisema kuwa CCM itabaki kuwa namba moja kwani hakuna chama hata kimoja kinachoweza kufanana nacho kutokana na kuimarika kwake, historia yake na sambamba na maendeleo inayoendelea kuwaletea wananchi.

"Chama cha Mapinduzi kitaendelea kuwa imara na hakuna wa kukichezea hata mmoja kwani chama hichi si chama cha mchezo" Alisema Dk.Shein.

Aidha,  Dk. Shein alisema kuwa ujenzi wa maskani ni miongoni mwa hatua za kuimarisha chama hivyo kuna kila sababu za kujenga maskani nzuri na za kisasa ambazo zitawasaidia wanaCCM kukaa na kujadili mambo yao ya maendeleo ya chama chao.


Sambamba na hayo, Dk. Shein aliwahakikishia wanamaskani wa Ukombozi wa Vijana kuwa atawaunga mkono katika ujenzi wa maskani yao hiyo ili iwe kubwa na ya kisasa na kuwa ya mfano katika Jimbo hilo.


Mapema Wanamaskani hao walieleza kuwa maskani yao hiyo ilianza na wanachama 27 na hivi sasa wapo wanachama 55 ambao kila kukicha wanaendelea kujiunga na maskani hiyo ambapo pia walitumia fursa hiyo kutoa shukurani kwa wale wote waliochangia ujenzi wao huo akiwemo Mwakilishi wa Jimbo hilo Haroun Ali Suleiman.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.