Habari za Punde

Zeco yakanusha uvumi kwamba litasitisha huduma ya kuuza umeme













Meneja Mkuu Shirika la umeme Zanzibar (ZECO) Hassan Ali Mbarouk alipokuwa akizungumza na wandishi wa Habari kuhusu uvumi ulionea kwamba litasitisha  huduma ya kuuza umeme kwa siku kadhaa katika Mkutano uliofanyika Ofisi za ZECO ziliopo Gulioni Mjini Zanzibar.

Na Ramadhani Ali. Maelezo Zanzibar.

Shirika la umeme Zanzibar (ZECO) limekanusha uvumi ulionea kwamba litasitisha  huduma ya kuuza umeme kwa siku kadhaa na kusababisha ghofu kwa wateja  na kupelekea msongamano katika vituo vya kununulia umeme vya Shirika hilo katika siku za karibuni.

Akizungumza na waandishi wa Habari Ofisini kwake Makadara, Meneja Mkuu wa ZECO ndugu Hassan Ali Mbarouk amesema kuongezeka kwa wateja katika vituo vya kuuzia umeme vya Shirika hilo kumesababishwa kukosekana huduma hiyo kwa kutumia simu za mkononi za Zantel kwa Easy pesa.

Ndugu Mbarouk amesema huduma ya kununua umeme katika vituo vyote vya ZECO itaendelea kama kawaida kwa siku zote na hakutakuwa na kuzimika wala kusita kuuza umeme katika vituo hivyo.

Hata hivyo amesema huduma ya kununua umeme  kwa kutumia  simu za mkononi kwa njia ya easy pesa itaendelea kukosekana  na amewataka wananchi kuwa wavumilivu wakati huu ambapo ZECO na Zantel  wanaendelea kulitafutia ufumbuzi tatizo lililojitokeza.

Amesema kukosekana  huduma hiyo  kwa njia ya easy pesa imesababishwa na mfumo  huo  kupata matatizo kuanzia tarehe 20 mwezi uliopita.

Amewahakikisha watumiaji wa umeme kwamba tatizo hilo litapatiwa ufumbuzi katika kipindi kifupi kijacho kwani mkataba wa mwanzo wa miaka miwili wa ZECO na Zantel utakapo malizika  mkataba mpya utatoa fursa kwa mashirika mengine ya simu kuingia mkataba wa kuuza umeme.

Akizungumzia zoezi linaloendelea la kubadilisha mita za zamani na kuweka mita za Tukuza, Menaja Mkuu amesema  Shirika limepanga itakapofika  mwishoni mwa mwaka 2017  wateja wote wa umeme watakuwa wanatumia mita za  Tukuza.

Amesema pamoja na mafanikio makubwa waliyopata ya kubadilisha mita za zamani wanawasi wasi kwa baadhi ya wateja wasiowaaminifu kuzihujumu mita za Tukuza na kulikosesha fedha shirika kwani mita hizo zinachukua muda mkubwa kukaguliwa baada ya kuwekwa tafauti na mita za zamani ambazo hukaguliwa kila mwezi.

Meneja Biashara wa Shirika la umeme Zanzibar ndugu Thabit Salum Khamis amewaeleza waandishi wa habari kuwa usambazaji umeme katika visiwa vya Unguja na Pemba umefikia asilimia 86 lakini watumiaji umeme ni chini ya asilima 50.

Ndugu Thabit amewataka wananchi kubadili mfumo wa maisha kwa kutumia  zaidi  umeme kwani ni rahisi  kwa matumizi ya nyumbani ikilinganishwa na nishati ya kuni na mkaa.       

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.