Habari za Punde

Rais Dk Shein atoa miezi miwili jengo la Ofisi ya Zimamoto likamilike




STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
Zanzibar                                      4.10.2016
---
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein ametoa miezi miwili kwa Taasisi zote zinazohusika na ujenzi wa ofisi ya Zimamoto zinazojengwa katika uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Abeid Amani Karume, Zanzibar ziwe zimeshakamilisha ujenzi huo.

Dk. Shein alitoa agizo hilo mara baada ya kutembelea eneo lililotengwa kwa ajili ya ujenzi wa Ofisi ya Zimamoto huko katika uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Abeid Amani Karume, ambapo ujenzi huo unaonekana kusuasua kwa muda mrefu.

Kutokana na kusuasua kwa ujenzi huo ndipo kulikompelekea Dk. Shein kutoa agizo hilo kwa Taasisi zote husika kukamilisha ujenzi huo ndani ya kipindi hicho hasa ikizingatiwa kuwa wahusika walipewa agizo hilo mwezi Mei mwaka jana wakati Mheshimiwa Rais alipofanya ziara kutembelea uwanja huo.

Dk. Shein alisema kuwa tokea kipindi hicho  hadi leo bado ujenzi huo haujaanza na kusisitiza ni lazima ukakamilike katika kipindi hicho hasa ikizingatiwa kuwa tayari serikali imeshatoa kiasi cha Dola za Kimarekani milioni 3.5 kwa ajili ya ununuzi wa gari za zimamoto pamoja na dola milioni 1.5 ambazo zimetolewa na Benki ya dunia kwa ajili ya nununuzi wa gari hizo.

Dk. Shein alisisitiza kuwa tarehe kama ya leo mwezi wa Disemba mwaka huu atarudi tena kwa ajili ya kuangalia jengo hilo likiwa limekamilika kwani anatambua kuwa Serikali ina fedha za kutosha kwa ajili ya ujenzi huo ila kuna changamoto ndani ya taasisi hizo zinazokwaza utekelezaji wa agizo lake.

“Tusifanye kazi kwa utamaduni tuliozoea, nimekupeni muda mrefu miezi miwili, malizeni mkimaliza nitakuja, hamkunialika nitakuja mkinialika nitakuja…pesa zipo lakini hamjaziomba”,alisema Dk. Shein.

Aidha, Dk. Shein alieleza kuwa kukamilika kwa ujenzi huo kutakuwa na tija kubwa Serikali hasa ikizingatiwa kuwa ujenzi wa jengo jipya la abiria katika uwanja huo linatarajiwa kukamilika hivi karibuni.

Nae Waziri wa Ncho Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Idara Maalum za SMZ Haji Omar Khair alimueleza Dk. Shein haja ya kuwepo kwa mashirikiano kati ya taasisi zote zinazosimamia ujenzi huo hasa kwa upande wa Wizara ya Mawasiliano, Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Zanzibar na Idara ya Zimamoto ili kufanikisha jukumu hilo.

Mapema Kamishna wa Idara ya Zimamoto Zanzibar Ali Abdalla Malimosi alimueleza Dk. Shein changamoto mbali mbali zinazoikabili kikosi hicho katika eneo hilo la uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Abeid Amani Karume.

Wakati huo huo, Dk. Shein alifika Mbweni kukagua eneo la mradi wa ujenzi wa nyumba za  kisasa zinazojengwa na Mfuko wa Hifadhi ya Jamii Zanzibar (ZSSF) na kupongeza juhudi zinazochukuliwa na Mfuko huo katika kuimarishaji miradi mbali mbali ya maendeleo yenye tija.

Dk. Shein alisema kuwa ndani ya miaka sita ya uongozi wake, Mfuko huo umeweza kufanya vizuri kwa kuanzisha miradi kadhaa ukiwemo ujenzi wa viwanja vya kufurahishia watoto Kariakoo Ungujua  na Tibirinzi Pemba, ujenzi wa mnara wa kumbukumbu ya miaka 50 ya Mapinduzi, pamoja na ujenzi wa jumba la treni unaotarajiwa kuanza mwezi ujao.

Katika maelezo yake Dk. Shein alisema kuwa ujenzi huo wa nyumba za kisasa una faida kubwa ambao unatarajiwa kuwa na nyumba 252 zikiwemo za vyumba vitatu, viwili na vinne.

Mapema Mkurugenzi Mtendaji wa Mfuko huo Abdulwakil Haji Hafidh alimueleza Dk. Shein kuwa ujenzi huo wa majengo 18 ya ghorofa unatarajiwa kukamilika mwishoni mwa mwaka 2018 na unatarajiwa kugharimu Tsh. bilioni 43.

Mkurugenzi huyo alieleza kuwa mradi huo utakuwa na Mabloki 18 ya Majengo ya Ghorofa Saba zenye Fleti 252 ambao utajengwa kwa awamu tatu tofauti ambapo tayari wameshaanza kujenga Mabloki Matano yenye Nyumba 70.

Alieleza pia kuwa tayari kwa hatua za awali shirika limeshatumia shilingi bilioni 8 ambapo tayari ujenzi huo ukiwa unaendelea nyumba 55 zimeshapata wanunuzi kutoka sehemu mbali mbali na hivi sasa wanafunga mikataba nao.

Mkurugenzi Mtendaji huyo alieleza kuwa mradi wa nyumba za Mbweni mwanzoni ulipangwa kwa ajili ya wananchi wenye vipato vya kati na chini ambazo zitauzwa kati ya shilingi milioni 168 hadi 249 lakini imebainika kuwa watu wengi hawatazimudu hivyo Mfuko umeamua kujenga za kipato cha chini huko eneo la Tunguu.

Alibainisha kuwa awamu ya kwanza ya mradi huo unaojumuisha ujenzi wa magorofa matano itakamilika mezi Aprili mwakani na kufuatiwa na ujenzi wa magorofa mengine 8 katika awamu ya pili na awamu ya tatu ni ya ujenzi wa magorofa yatakayo baki.

Alieleza kuwa tayari wameshaanza kutafuta wanunuzi na wameshatembelea sehemu mbali mbali za ndani na nje  kwa ajili ya kujitangaza huku akimueleza kuwa nyumba hizo zitakuwa na maeneo ya huduma muhimu yakiwemo maduka pamoja na ukumbi mkubwa wa kisasa ambao utajengwa katika eneo hilo.

Mkurugenzi huyo alisema kuwa juhudi za makusudi zimefanywa katika kuhakikisha ujenzi wa nyumba hizo unakuwa imara zaidi chini ya Kampuni ya ujenzi ‘Dezo Civil Construction Limited yenye makao makuu yake Jijini Dar-es Salaam.

“Ujenzi wetu tumeupanga kuutekeleza kwa awamu tatu ambapo awamu ya kwanza tutajenga Bloki Tano, ile ya Pili pia tutajenga Bloki Tano na ya mwisho tutamalizia kwa Bloki Nane “, alisema Mkurugenzi huyo wa Mfuko wa Hifadhi ya Jamii Zanzibar.

Akitoa maelezo wakati akimtembeza kwenye ujenzi wa nyumba hizo Meneja Mipango,Uwekezaji na Utafiti wa Mfuko wa Hifadhi ya Jamii Zanzibar Khalifa Muumin Hilal alimuhakikishia Dk. Shein  umadhubuti mkubwa wa nyumba hizo.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.