Habari za Punde

Hakuna dakhalia iliyofungwa Pemba- Wizara elimu



Na Haji Nassor, Pemba

WIZARA ya Elimu na Mafunzo ya Amali wilaya ya Wete Pemba, imekanusha taarifa zilizosambaa mitandandaoni na baadhi ya watu kuwa, dakhalia za skuli za Chasasa na Utaani,  zimefungwa, kufuatia kuwepo kwa tendo la ulawiti skulini hapo.

Wizara hiyo imesema, wanafunzi kwenye skuli hizo wapo  kama kawaida wanaedelea na masomo yao na wala hakuna wanafunzi waliorejeshwa majumbani, kwa kuwepo dhana ya ulawiti kwenye skuli hizo.

Akizungumza na mwandishi wa habari hizi kwa njia ya simu Afisa elimu na mafunzo ya amali wilayani humo, Khamis Said Hamad, alisema taarirfa hizo hazina ukweli wowote.

Alisema hakuna dakhalia yoyote iliofungwa wilayani humo, na taarifa zilizosambaazwa juzi zinalengo la kupotosha umma jambo ambalo, sio jema.

“Wanafunzi waliopo dakhalia wanaendelea na kuishi hapo bila ya hofu na wanaendelea vyema na masomo yao na wala sisi hatujapokea taarifa za kuwepo kwa ulawiti wa kutisha kama inavyoelezwa’’,alifafanua.

Hata hivyo Afisa elimu huyo, amewataka wananchi kuacha kushabikia za kuziamini haraka, taarifa zinazorushwa kwenye mitandao ya kijamii.

Katika hatua nyengine alikiri kuwa, mwaka juzi alikuwepo mwanafunzi muathirika wa tendo hilo na alipokelewa kwenye skuli hizo akitokea Mkoani, ingawa baadae aliondolewa.

“Ni kweli aliwahi kuja mwanafunzi kusoma hapa alikuwa anafanya au anafanyiwa tendo la ulawiti, lakini tulipombana aliondolewa na sasa skuli hizo hali iko shuwari’’, alibainisha.

Baadhi ya wazazi na walezi wa mji Wete kisiwani Pemba, wameziomba taasisi husika kufanya utafiti wa kina, juu ya jambo hilo, kutokana kuwepo kwa tuhuma za muda mrefu.

“Hili jambo kwenye skuli zetu za Chasasa na Utaani limeshakuwa la muda mrefu sasa, lazima serikali itafute njia ya kutoa taarifa rasmi, badala ya taarifa za kudokoa dokoa kama ilivyo sasa’’,alishauri  Khamis Juma.

Nae Asha Makame Muhunzi, alisema taarifa za kuwepo kwa matendo ya ulawiti ndani ya wilaya ya Wete, halina shaka, ni vyema sasa hatua zikachukuliwa.

Nae Afisa huduma za wanafunzi kutoka wizara ya elimu kisiwani Pemba, Said Massoud Othaman alisema sio wilaya ya Wete tu lakini hakuna dakhalia yoyote iliofungwa kisiwani Pemba kwa tendo hilo.

Alieleza kuwa, ijapokuwa kuna taarifa za ulawiti kwenye baadhi ya skuli, lakini taarifa kuwa skuli za sekondari za Chasasa na Utaani zimefungwa kwa tatizo hilo, sio kweli.

“Tendo la ulawiti sasa limeenea kwenye vyuo vya kur-an, skulini, majumbani na maeneo mengine , hivyo ni jukumu letu wazazi kushirikiana ili kuliondoa’’,alifafanua.

Hata hivyo alisema wamekuwa wakipokea malalamiko juu ya shutuma za tendo hilo, ingawa hawajabaini kuwepo kwa udhalilishaji kama inavyoelezwa kwenye skuli hizo.

Afisa Ustawi wa Jamii wilaya ya Wete Haroub Suleiman Hemed, alisema, kitakwimu matendo hayo hayako juu wilayani humo, ingawa kimazungumzo hali huwa inatisha.

“Jamii tushirikiane katika kupambana na udhalilishaji wa aina yote, maana kama kuna tetesi basi ujuwe jambo lipo au linanyemelea kwenye mazingira yetu’’,alifafanua.

Mwanafunzi mmoja ambae hakupenda jina lake lichapishwe alisema kwa sasa hawajamgundua mwanafunzi mwenzao anaendesha vitendo hivyo, hasa baada ya aliekuwepo kuondolewa.


Juzi katika baadhi ya mitando ya kijamii na minong’ono ya watu kwenye mikusanyiko, kuliwa na taarifa ya skuli za sekondari na Chasasa ambazo zina dakhalia kufungwa, kutokana ongezeko la tendo la ulawiti kwa wanafunzi.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.