Habari za Punde

Mtandao wa Asasi za kiraia Pemba PACSO wawazindua wananchi kuhoji matumizi ya fedha za umma

NA HAJI NASSOR, PEMBA

MADIWANI na wananchi wa wadi sita za mkoa wa kaskazini Pemba, wamesema kazi iliofanya na Mtandao wa Asasi za Kiraia Pemba, PACSO, ndio imaewaamsha na kutambua umuhimu wa kufuatilia kwa karibu, matumizi ya fedha za umma kwenye miradi mbali mbali ikiwemo ya barabara.

Walisema hawakuwa wakifikiria kuwa wanawajibu na haki ya kujua gharama za ujenzi wa miundombinu hiyo, hata inayopita kwenye maeneo yao, wakidhani kuwa kazi hiyo inawapasa watendaji wa taasisi za fedha pekee.

Wakizungumza kwenye kongamano lililofanyika Kituo cha elimu mbadala na watu wazima Wingwi wilaya ya Micheweni la kujadili ripoti ya awali ya kufuatilia matumizi ya fedha za umma, walisema utafiti huo umewapa taaluma.

Walisema wakati wanapitiwa kuhojiwa na watu waliondaliwa na PACSO, juu ya ikiwa wanafahamu lolote gharama ya ujenzi wa barabara na ubora wake, hawakuwa wakijua kuwa wana haki hiyo.

Farida Ali Saleh wa Wete, alisema wapo wananchi baadhi yao, walioshindwa kutaja gharama za ujenzi wa barabara zao za ndani, kwa vile walishazoea kuwa hayo hayawahusu.

“Utafiti uliofanya na PACSO, sasa wengi umetuzindua kuwa, tuna haki ya kuangalia matumizi ya fedha za umma na hata ujenzi wa barabara, hongera mtandao’’,alifafanua.

Nae Khamis Rashid, alisema wananchi walikuwa wamekosa uwelewa wa umuhimu wa kuzingalia na kuzifuatilia fedha zinazofikishwa kwenye maeneo yao kwa ajili ya miradi ya maendeleo.

Diwani wa wadi ya Jadida Wete Mwanaali Ali Salum, alisema, hata wananchi kabla ya kupita utafiti huo, hawakuwa wakifikiria kuwa, kuna umuhimu wakushirikishwa kwenye miradi ya barabara hasa za ndani.

“Utafiti huu wa mradi wa kufuatilia rasilimali za umma (fedha), naamini sasa umewapa mwanga wananchi, kwamba na wao ni sehemu ya kuifanikisha miradi ya ujenzi wa barabara na hata kuangalia kipaumbele chao”,alisema.

Akifungua kongamano hilo, Mratibu wa mradi huo Omar Ali Omar, alisema mradi huo wa miezi mitatu ambao umegharimu shilingi milioni 68, ulikuwa na lengo la kuangalia uwelewa wa wananchi juu ya rasilimali za umma.

Alieleza kuwa kwenye utekelezaji wa mradi huo, wananchi 36 kutoka wadi za Chimba, Kiuyu Maziwang’ombe, Micheweni, Mtambwe, Konde na Kiuyu Minungwini walipewa mafunzo juu ya ufuatiliaji wa fedha hizo.

“Baada ya mafunzo hayo, tuliwapa madodoso ya aina mbili, moja kwa ajili ya jamii na la pili kwa taasisi za fedha kama Halmashauri, baraza la mji na hata wizara inayosimamia majenzi na kilimo’’,alifafanua.

Hata hivyo Mratibu huyo alisema ripoti kamili ya utafiti huo, inatarajiwa kutolewa wakati wowote, ingawa mradi huo wa miezi mitatu, unatarajiwa kukamilika mwezi huu.


Mtandao wa Asasi za kiraia Pemba PACSO ambao umeanzishwa mwaka 2005, tayari umeshatekeleza miradi saba iliofadhiliwa na taasisi ya ‘the foundation for civil society’ ya Tanzania bara ukiwemo wa utoaji wa elimu ya katiba pendekezwa.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.