STATE
HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF
THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
Zanzibar 26.2.2017
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.
Ali Mohamed Shein amesema kuwa yeye ndio Rais wa Zanzibar na kueleza kuwa
hakuna Baraza la Wawakilishi linalovunjwa ndani ya mwaka mmoja na kiutaratibu
Baraza hilo huvunjwa baada ya miaka mitano kwa sheria, taratibu na kanuni zake.
Hivyo Dk. Shein
aliwataka wananchi na wanaCCM kuepuka kauli za upotoshwaji zinazosambazwa mitandaoni.
Dk. Shein aliyasema
hayo leo huko katika ukumbi wa CCM, Mkoa wa Mjini iliopo Amani mara baada ya
kukabidhi vifaa vya michezo kwa vijana kwa ajili ya maandalizi ya Ligi ya Mpira
wa Miguu kwa Timu 18 za Unguja.
Katika maelezo hayo
Dk. Shein alisema kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar anayoiongoza yeye
itaendelea kuwa madarakani na kueleza kuwa mazungumzo aliyoyafanya leo kati
yake na Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi ni mazungumzo ya kawaida baada ya
kumwita kwa lengo la kubadilishana mawazo na kueleza changamoto zilizpo
katika Majimbo yao.
Dk. Shein alisema kuwa
yeye akiwa ni Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Wawakilishi pia, ni
sehemu ya Baraza hilo na kwenda kuzungumza na Wajumbe wa Baraza hilo sio jambo
jipya kwani ameshawahi kufanya hivyo kutokana na taratibu na kanuni zilizopo.
Pamoja na hayo, Dk.
Shein aliwasisitiza wanaCCM na wananchi kuwa hakuna Baraza linalovunjwa asubuhi
hivyo kauli hizo zinazozungumzwa na zinazosambaa ni za upotoshaji na zisizo na
ukweli.
Aidha, Dk. Shein
aliwaeleza wanaCCM wakiwemo vijana waliohudhuria katika hafla hiyo kuwa
Mihimili mitatu iliyopo ikiwemo Mahakama, Serikali na Baraza la Wawakilishi
hakuna muhimili hata mmoja unaomshurutisha mwenziwe bali hufanya kazi kwa
mashirikiano ya pamoja ili kufikia malengo yaliokusudiwa katika nchi.
Nae Balozi Seif Ali
Idd Makamo wa Pili wa Rais alieleza kuwa uzushi unaosambazwa katika mitandao
hauna maana na kueleza kuwa amepokea simu nyingi kutoka kwa wananchi kutokana
na kauli hizo za mitandaoni ambazo si za msingi kuwa Dk. Shein leo anakabidhi
nchi kwani maneno hayo hayakuanza leo bali ni kawaida kwa wapinzani.
Hivyo aliwataka wanaCCM
na wananchi kupuuza kauli hizo.
Rajab Mkasaba, Ikulu
Zanzibar
Postal Address:
2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment