Habari za Punde

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Azindua Ndege Maalum ya Utafiti wa Mafuta na Gas Asilia Zanzibar.


Na Othman Khamis OMPR. 
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi
ametahadharisha Wananchi kwamba itakapofikia hatua ya kupatikana kwa rasilmali ya Mafuta na Gesi Asilia Visiwani Zanzibar isijekuwa chanzo
cha sababu ya Wananchi kubeteka na mradi huo kwa kuacha shughuli zao
za Kiuchumi ambazo huwapatia riziki zao za kila siku.
Alisema Rasilmali hiyo endapo itapatikana kufuatia utafiti unaoanza kufanywa hivi sasa itasaidia kwa kiwango kikubwa kupunguza changamoto nyingi zinazoikabili Serikali Kuu pamoja na Wananchi kwa ujumla.

Balozi Seif Ali Iddi alitoa tahadhari hiyo wakati wa hafla maalum ya uzinduzi wa Ndege itakayofanya Utafiti na hatimae  uchimbaji wa Rasilmali ya Mafuta na Gesi Asilia Zanzibar iliyofanyika katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Abeid Aman Karume nje kidogo ya Kusini ya Mji wa Zanzibar.

Alisema yapo Mataifa mengi Duniani yakiwemo yale ya Bara la Afrika yaliyoanza kuzalisha miradi hiyo kwa matumaini makubwa ya kuimarisha Uchumi wao lakini hivi sasa zimekuwa na changamoto zaidi za Kiuchumi hali ambayo Zanzibar na Wananchi wake wanapaswa kuwa makini na kujifunza matukio hayo.

Hata hivyo Balozi Seif alisema safari ya Zanzibar kuelekea kwenye uchumi Mkuu imeanza mara baada ya Baraza la Wawakilishi Zanzibar kupitisha Mswaada wa kuanzisha sheria inayoiruhusu Zanzibar kutafuta na kuchimba mafuta yake yenyewe na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Braza la Mainduzi kusaini Sheria hiyo.

Alisema busara za Rais Mstaafu wa Serikali ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Dr. Jakaya Mrisho Kikwete za kusimamia utaratibu wa kupelekwa mswada Bungeni zimepelekea suala la mafuta na Gesi Asilia hivi sasa kutoka katika mambo ya Muungano.

Balozi Seif alifahamisha kwamba Zanzibar na Wananchi wake wamefarajika na mwanzo mzuri wa hatua za awali za utafiti na baadaye uchimbaji wa Mafuta na Gesi Asilia ndani ya mipaka yake ya Visiwa vya Zanzibar.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar alieleza kwamba Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itaendelea kushirikiana na Kampuni ya Utafiti na Uchimbaji wa Mafuta na Gesi Asilia ya Nchini Ras Al – Khaimah { RAKGAS } kwa juhudi zake zilizoonyesha nia safi ya kushirikiana na Zanzibar katika Mradi huo mpya wa Mafuta na Gesi.

Alisema Rak Gas imekuwa mshirikia mkubwa wa Zanzibar katika harakati za kuwaondoshea dhiki ya huduma za Maji safi na salama Wananchi wa Zanzibar ambapo tayari Kampuni hiyo imeshafadhili nuchimbwaji wa visima 100 Unguja na Pemba.

“ Tumeshuhudia juhudi kubwa zinazochukuliwa na Serikali ya Rais Al –Khaimah  Kupitia Kampuni ya Rak Gas katika kuunga mkono harakati za Kijamii Visiwani Zanzibar ”. Alisema Balozi Seif.

Balozi Seif aliwataka Wananchi wote kutokuwa na hofu kwa ndege itakayohusika na utafiti wa Mafuta na Gesi katikia maeneo yanayodhaniwa kuwa na Rasilmali hiyo kwa vile itaruka katika maeneo ya chini zaidi na kuwataka waendelee na shughuli zao kama kawaida.

Mapema Mhandisi Muandamizi wa Kampuni ya Rak Gas kutoka Nchini Ras Al – Khaimah Dr. Osama Abdd – AAL ameipongeza Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa kuanza  kuweka Historia mpya  katika muelekeo wake wa mradi wa Kiuchumi wa Mafuta na Gesi Asilia.

Dr. Osama alisema Wananchi wa Zanzibar na ndugu zao wa Ras Al – Khaimah tayari wamekuwa na uhusiano wa Kihistoria uliopelekea kujenga ushirikiano zaidi katika uanzishwaji wa utafiti wa Mafuta na Gesi Asilia Zanzibar.

Alisisitiza kwamba utiaji Saini Mkataba wa Utafiti wa Rasilmali hiyo uliofanywa na Serikali zote mbili Nchini Ras Al – Khaimah karibu miaka miwiliiliyoita ni uthibitisho wa uhusiano huo wa pande hizo mbili.

Naye Msimamizi wa Kampuni ya Bell Geosace Interrises Limited inayofanya Utafiti huo Bwana Stephane Kunar  alisema ataalamu wa Taasisi hiyo wako makini katika suala ya uhifadhi wa mazingira wakati wanapoendesha tafiti zao.

Bwana Kunar alisema hatua hiyo inakuja kutokana na uzoefu mkubwa waliyonao wahandisi hao  kwa karibu miaka 70 sasa tokea kuanzishwa kwake ambapo Barani Afrika kazi hiyo wanaiendeleza kwa zaidi ya miaka 15 sasa.

Alisema utafiti wao ambaowanaufanya kwa zaidi ya Mita 100 chini ya ardhi pamoja na maeneo ya Bahari  kwa Afrika umeshafanyikka Afrikka kwa Nchi ya  Botswana Brazil Barani Amerika ya Kusini.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.