Habari za Punde

Wamiliki wa magari Chakechake watakiwa kuyatumia vyema maeneo ya maegesho

Na Hanifa Salim, Pemba

BARAZA la Mji Chake chake Pemba, limewataka wamiliki wa magari kuyatumia maeneo yalioandaliwa kwa ajili ya maegesho ya magari kwa kufuata utaratibu unaotakiwa ili kupunguza msongamano wa magari katika mji wa Chake chake.

Hayo yalielezwa na Mkurugenzi wa Baraza la Mji huo,   Nassor Suleiman Zaharani, wakati alipokua katika ziara ya siku moja na Mkuu wa Mkoa wa Kusini Pemba, ambapo akikagua   maeneo ya maegesho ya magari katika mji wa chake chake.

Alisema  lengo la kuanzisha maeneo hayo ni kuondosha msongomano wa magari uliopo katika mji wa chake chake kama alivyoagiza Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dkt, Ali Mohamed Shein.

“Tumeandaa eneo la kupaki gari za Teksi, karibu eneo la Soko la Qatar  ambapo litachukua gari 40 hadi 50 kwa wakati mmoja, tumeandaa maegesho ya gari za Wesha na Ndagoni ambalo limegharimu milioni 6,400,000/=  pamoja na eneo la maegesho ya gari za keri lililopo katika mji wa Chake chake”, alisema.

Sambamba na hayo, alisema Baraza la mji Chake chake limeandaa maegesho ya magari katika eneo la nyumba za fleti Madungu ambapo litakua ni egesho la gari za Mkoani ambapo litachukua gari 20 kwa wakati mmoja.

Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Kusini Pemba, Mwanajuma Majid Abdalla, alilipongeza baraza la mji Chake chake kwa kufanya juhudi hiyo ili kuitekeleza kauli ya Rais wa Zanzibar.

“ Mujue wajibu wa kazi zenu na kuweza kusimamia tusiwe na muhali tutakapokua na muhali hatutoweza kujenga nchi lengo letu ni kujenga nchi na kubadilisha mji wetu wa Chake chake” alisema Mkuu huyo.

Hata hivyo alilitaka Jeshi la Polisi kubadilika kwa kusimamia gari ambazo hupakiwa pembeni mwa Mji wa Chake chake ili kuwadhibiti wanaoegesha magari katika mji huo kwa kuweza kueka mji katika mandhari nzuri.

Nae, Mkuu wa Wilaya ya Chake chake, Salama Mbarouk Khatib, aliahidi kusimamia na kudhibiti watakao haribu mji wa chake chake kwa kuwachukulia hatua za kisheria ili kuondoa malalamiko na kuleta mafanikio yaliokusudiwa.


Katika ziara hiyo ya Mkuu wa Mkoa na Wilaya na watendaji wa baraza la mji walitembelea egesho ya magari katika Mji wa Chake chake , maegesho ya gari ta TAX karibu na Soko la Qatar, egesho la gari za Wesha na Ndagoni, Madungu katika egesho la gari za Mkoani na kukagua Soko la Quweit lililopo Michakaini ambalo linaendelea na ujenzi wake.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.