STATE
HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF
THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
Zanzibar 26.05.2017
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la
Mapinduzi Alhaj Dk. Ali Mohamed Shein amewataka wafanyabiashara kuwa waadilifu
katika kufanya biashara zao katika mwezi mtukufu wa Ramadhani kwani imekuwa ni
jambo la kawaida kwa baadhi yao kupandisha bei za bidhaa kila ifikapo mwezi
huu.
Alhaj Dk. Shein,
aliyasema hayo katika risala maalum aliyoitoa kwa wananchi kupitia vyombo vya
habari kwa ajili ya kuukaribisha Mwezi Mtukufu wa Ramadhani mwaka huu wa 1438
Hijria sawa na mwaka 2017 Miladiya.
Katika risala yake hiyo,
Alhaj Dk. Shein amesema kuwa imekuwa ni jambo la kawaida kwa baadhi ya
wafanyabiashara kupandisha bei za bidhaa kila unapofika Mwezi Mtukufu wa Ramadhani
jambo ambalo huleta usumbufu mkubwa kwa wafungaji na wananchi wote kwa jumla.
Hivyo, aliwasihi
wafanyabiashara wakubwa na wadogo, wanaouza bidhaa zao rejareja na jumla
wazingatie wito wake huo na nasaha anazozitoa kwa kuwahurumia wananchi wenzao
kwa kuwauzia bidhaa kwa bei za kawaida, zilizo nafuu kwani kwa kufanya hivyo
watakuwa wanazishukuru neema za Mwenyezi Mungu na Mola wao atawaongezea Baraka.
Alhaj Dk. Shein, alisema
kuwa ni wajibu kujiandaa na kuukaribisha mwezi wa Ramadhani kwa matumaini na
matarajio ya kunufaika na fadhila zake hivyo, ni vyema juhudi zikaongezwa
katika kutoa sadaka kwa kuwapa wale wanaostahili na wanaohitaji sadaka hizo
pamoja na kuwasaidia wenye uwezo mdogo kutafuta futari na daku katika mwezi huu
mtukufu.
Aidha, alieleza kuwa
ibada ya funga kwa kawaida ina mafundisho mengi ikiwa ni pamoja na kuitaka
jamii kuishi pamoja, kuheshimiana na kusaidiana, kustahilimiliana na
kuvumiliana, kuwa na subira pamoja na kuwa na uwezo wa kudhibiti matamanio ya
nafsi.
Akieleza athari za mvua
za masika, Alhaj Dk. Shein alitoa pongezi kwa wananchi wote wkwa imani, mapenzi
na huruma walizoonesha kwa kuwa pamoja na wale wote walaioathirika, kwa kuwapa
misaada na kuwapongeza wafanyabiashara na viongozi mbali mbali kwa kushirikiana
na Serikiali katika kuwapa ndugu zao hao misaada muhimu.
Hata hivyo, aliwaahidi
wananchi kuwa Serikali itahakikisha michango na misaada inayotolewa na
wananchi, viongozi pamoja na wafanyabiashara kwa ajili ya wananchi walioathirika
na maafa, inawafikia wanaostahiki na hatua kali za kisheria zitachukuliwa kwa
wale watakaokwenda kinyume na taratibu zilizopangwa za kufikisha na kuigawa
misaaada hiyo.
Alhaj Dk. Shein, pia,
alitumia fursa hiyo kuwataka wananchi kujiepusha kujenga katika sehemu za
mabondeni pamoja na maeneo ya njia muhimu za maji huku akiwataka wananchi
kushirikiana na Serikali yao katika kuvitunza na kuvilinda vianzio vya maji
vilivyopo.
Pamoja na hayo,
aliwahimiza wananchi pamoja na viongozi wa Manispaa na Halmashauri kuongeza juhudi
katika kudumisha na kusimamia usafi ili kuepuka miripuko ya maradhi mbali
mbali, hasa ya matumbo katika kipindi hiki cha mvua.
Alisisitiza kuwepo kwa
mashirikiano ya pamoja kwani ana taarifa kuwa kuna baadhi ya wafanyabiashara
wameshaanza kuipuuza miongozo wanayopewa na wataalamu pamoja na sheria za usafi
zilizopo kwani ni vyema ikumbukwe kuwa mitihani ya maradhi ikitokea watu wa
mwanzo ambao kipato chao huathirika ni wafanyabiashara.
Sambamba na hayo, Alhaj
Dk. Shein alisema kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Awamu ya Saba,
imekuwa ikiimarisha mipango na mikakati iliyokuwepo ya kujikinga na kukabiliana
na maafa pamoja na kufanya marekebisho ya sheria iliyokuwepo na kuziimarisha
taasisi husika.
Kwa mujibu wa maelezo ya
Alhaj Dk. Shein, hivi Serikali inaadaa mpango wa kuliondoa tatizo la mafuriko
katika eneo la Mwanakwerekwe na sehemu nyengine kupitia Awamu ya Pili ya Mradi
wa ZUSP sambamba na kujenga barabara imara katika barabara ya Kibonde Mzungu ili
iweze kupitika bila ya shida katika misimu yote.
Alhaj Dk. Shein, alitoa
shukurani zake kwa wananchi wote kwa kuendelea kushirikiana na Serikali katika
kudumisha umoja na mshikamano uliopo na kuwataka kuendeleza utamaduni wao wa
kuishi kwa pamoja bila ya kubaguana kwa dini ama kabila.
Aliongeza kuwa
mashirikiano ya pamoja yamewezesha kuongeza kasi ya ukuaji wa uchumi ambapo
katika mwaka uliopita, uchumi ulikuwa kwa asilimia 6.5 na mfumko wa bei ulibaki
katika tarakimu moja, asilimia 5.7 sambamba na kupiga hatua katika ukusanyaji
wa mapato.
Pia, Alhaj Dk. Shein,
aliikumbusha Wizara ya Ardhi, Maji, Nishati na Mazingira iendeleze utaratibu
kwa kusambaza maji katika Mwezi huu mtukufu wa Radhamani, katika maeneo mabli
mbali ambayo huduma za maji safi salama huwa zina upungufu na kuwataka wananchi
kushirikiana na na wafanyakazi wa Mamlaka ya Maji Zanzibar (ZAWA), ili kazi ya
kusambaza maji ifanyike vizuri.
Rajab
Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax:
024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment